Hadithi za Maandiko
Barua kutoka kwa Yakobo—Mwaliko wa kutii, siyo tu kusikia, neno la Mungu


Yakobo1–3

Barua Kutoka kwa Yakobo

Mwaliko wa kutii, sio tu kusikia, neno la Mungu

Yakobo akiandika barua.

Yakobo alikuwa mwana wa Mariamu na mmoja wa kaka zake Yesu Kristo. Yakobo pia alikuwa kiongozi wa Kanisa huko Yerusalemu. Aliandika barua kwa watu wa Mungu kote ulimwenguni ili kuwasaidia kuishi injili ya Yesu Kristo.

Yakobo1:1

Joseph Smith akisoma Biblia

Yakobo aliandika, “Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu.” Miaka mingi baadaye, mvulana aliyeitwa Joseph Smith alisoma maneno haya na kuamua kusali kuhusu maswali yake. Joseph Smith baadaye alisema, “Niligundua ushuhuda wa Yakobo kuwa ni wa kweli.” Mungu alijibu sala ya Joseph, na atajibu zetu pia.

Yakobo 1:5; Joseph Smith—Historia ya 1:11–17, 26

Yakobo akifundisha kikundi cha watu.

Yakobo pia aliandika kwamba tunapaswa kusikiliza kwa makini kile watu wengine wanachosema na kujaribu kutowakasirikia. Tunapokuwa na hasira, hatuwezi kumtumikia Mungu.

Yakobo 1:19–20

Mvulana na msichana wanazungumza na mwanamke aliye na mtoto anayelia.

Yakobo alisema kwamba haitoshi tu kusikia neno la Mungu; tunahitaji kuliishi pia. “Iweni watendaji wa neno,” aliandika, “wala si wasikiaji tu”

Yakobo 1:22

Mvulana na msichana wamemwalika mwanamke na mtoto wake kuja ndani ya hema lenye joto pamoja na familia yao.

Kuwa mfuasi wa Yesu Kristo ni zaidi ya kuamini tu katika Mungu, Yakobo alieleza. Hata ibilisi anajua kwamba Mungu ni halisi. Tunapowaona watu walio na baridi au wenye njaa, tunapaswa kuwapa nguo na chakula. Tunapaswa kuwatembelea wajane na yatima. “Imani pasipo matendo imekufa.” Yakobo aliandika.

Yakobo 1:27; 2:14–20

Mtu akimwongoza farasi mbali na hatari.

Yakobo pia alitaka kuwafundisha Watakatifu kuzungumza na watu kwa ukarimu. Alisema kwamba kuwa makini na maneno yetu ni kama kumwongoza farasi. Tunaweza kumwongoza farasi mkubwa kwa hatamu, ambayo imeunganishwa kwenye kipande kidogo cha chuma katika mdomo wa farasi. Maneno yetu yanaweza pia kuonekana madogo, lakini yanaweza kuwa yenye nguvu.

Yakobo 3:2–3

Merikebu katika dhoruba, ikiongozwa njia na usukani mdogo.

Yakobo alisema kwamba kudhibiti maneno yetu ni kama kuongoza merikebu. Hata kama merikebu ni kubwa na upepo ni mkali, tunaweza kuiongoza merikebu kwa kudhibiti usukani mdogo sana. Usukani ni kama maneno yetu. Kama tunaweza kudhibiti kile tunachokisema, tunaweza kuleta tofauti kubwa!

Yakobo 3:4–5

Watu wakibishana na askari wa Kirumi, ambaye amegonga matunda.

Maneno yasiyo ya ukarimu, Yakobo alieleza, yanaweza kuwa kama moto mdogo ambao huanzisha moto mkubwa. Yanaweza kuenea haraka na kusababisha maumivu mengi. Hii ndiyo sababu ni muhimu kuwa makini na maneno yetu.

Yakobo 3:5–6

Watoto wakimpa askari matunda.

Yakobo aliandika kwamba tunatumia vinywa vyetu kusali kwa Baba wa Mbinguni. Lakini wakati mwingine pia tunatumia vinywa vyetu kusema mambo mabaya kwa watu wengine, ambao ni watoto wa Baba wa Mbinguni. Yakobo alisema haipaswi kuwa hivyo.

Yakobo 3:9–10

Mandhari ya amani karibu na chemchemi, huku Yakobo akiwafundisha watu kuhusu injili.

Ili kuwafundisha Watakatifu kuzungumza maneno ya ukarimu, Yakobo alifundisha kwamba chemchemi haiwezi kutoa maji safi na maji machungu. Mti wa mtini hauwezi kuzaa mizeituni, na mzabibu hauwezi kuzaa mitini. Kwa njia hiyo hiyo, kama tuna wema na upendo katika mioyo yetu, maneno yetu yanapaswa kuwa mazuri na ya upendo pia!

Yakobo 3:11–18