Mathayo 10; Luka 5:1–11; 6:12–16
Yesu Anawachagua Mitume Wake
Mwaliko wa kuwa “wavuvi wa watu”
Siku moja, watu walikuja katika Bahari ya Galilaya kumsikiliza Yesu akifundisha. Yesu aliwafundisha kutoka kwenye mashua wakati wakisikiliza ufukweni. Mashua ilimilikiwa na mvuvi aliyeitwa Simoni.
Luka 5:1–3
Wakati Yesu alipomaliza kufundisha, Yeye alimwomba Simoni apeleke mashua sehemu ya kina kirefu cha bahari. Alimwambia Simoni aweke nyavu yake majini ili avue samaki kiasi fulani. Simoni alisema kwamba amekuwa akivua samaki usiku mzima na hakuvua samaki yeyote. Lakini kwa sababu Yesu alimwambia, basi angejaribu tena.
Luka 5:4–5
Simoni alivua samaki wengi sana kiasi kwamba nyavu yake ilikatika! Aliwaita rafiki zake katika mashua nyingine kuja kumsaidia. Punde mashua zilikuwa zimejaa samaki, wakaanza kuzama. Simoni na rafiki zake walishangaa!
Luka 5:6–7, 9
Simoni alipiga magoti mbele ya Yesu. Alisema, “Mimi ni mtu mwenye dhambi, Ee Bwana.” Alijua kwamba Yesu alitumwa kutoka kwa Mungu. Yesu alimwambia asiwe na hofu.
Luka 5:8
Yesu alimwalika Simoni, Andrea kaka yake, na rafiki zake, Yakobo na Yohana, wamfuate Yeye. Badala ya kuvua samaki, wangewasaidia watu kuja kwa Yesu.
Marko 1:16–17; Luka 5:10–11
Simoni, Yakobo, na Yohana waliacha mashua zao za kuvua samaki na wakawa Mitume wa Yesu. Baadaye, Yesu alimpa Simoni jina Petro. Mtume ni shahidi maalum wa Yesu Kristo. Yesu aliwaita wanaume 12 kuwa Mitume Wake. Yeye alisali ili kujua ni nani alipaswa kumwita. Aliwapa Mitume Wake mamlaka ya ukuhani ili kuliongoza Kanisa Lake.
Mathayo 10; Luka 6:12–16; 9:1–2
Kwa sababu Mitume walikuwa na nguvu za Mungu, wangeweza pia kuwaponya watu waliokuwa wagonjwa, kuwafufua watu baada ya kufa, na kufanya miujiza mingine.
Mathayo 10:8
Yesu aliwatuma Mitume Wake kwenye miji mingi kuwafundisha watu injili Yake. Yeye alisema kwamba Roho Mtakatifu angewasaidia kujua nini cha kusema. Yesu alisema baadhi ya watu wasingependa kile walichokifundisha, lakini wanapohudumu kwa uaminifu, Mungu angekuwa pamoja nao.
Mathayo 10: 5–7, 19–22