Hadithi za Maandiko
Mwokozi Anazaliwa—Ahadi ya Mungu inatimizwa


Luka 2; Mathayo 2:1–15

Mwokozi Anazaliwa

Ahadi ya Mungu inatimizwa

Yusufu na Mariamu wanasafiri kwenda Bethlehemu

Yusufu na Mariamu waliishi Nazareti. Mariamu alikuwa punde anakaribia kupata mtoto. Kila mtu ilibidi aende kwenye mji wao wa nyumbani ili kuandikishwa. Hii ilimaanisha kwamba Yusufu na Mariamu walitakiwa kwenda Bethlehemu, mji wa Yusufu. Iliwabidi wasafiri safari ndefu kufika huko.

Luka 2:1–5

Mariamu na Yusufu katika Bethlehemu.

Safari haikuwa rahisi kwa Mariamu. Kwa sababu watu wengi walikuwa wamekuja Bethlehemu, Mariamu na Yusufu hawangeweza kupata mahali pa Mariamu kujifungua mtoto wake.

Luka 2:6–7

Mariamu na Yusufu wakiwa wamembeba mtoto mchanga Yesu.

Walipata mahali ambapo wanyama kwa kawaida waliwekwa. Katika sehemu hii ya unyenyekevu, Yesu alizaliwa. Mariamu na Yusufu walimpenda na kumtunza mtoto Yesu. Walimfunika Yeye kwa nguo ili kumsaidia kuwa na joto na faraja. Walimlaza kulala horini, ambapo kwa kawaida lilikuwa likitumika kuwalisha wanyama.

Luka 2:6–7

Malaika akitokea kwa kundi la wachungaji.

Katika eneo la karibu, wachungaji walikuwa wakiwalinda kondoo wao wakati wa usiku. Ghafla, mwanga mkali uliangaza kote kuwazunguka, na malaika akatokea. Wachungaji waliogopa.

Malaika akiwaambia wachungaji kwamba Yesu amezaliwa.

Malaika aliwaambia wasiogope, kwa sababu alikuwa na habari njema! Mwokozi alikuwa amezaliwa Bethlehemu, na wangeweza kumkuta amelala horini. Kisha malaika zaidi walikuja, wakisema, “Atukuzwe Mungu juu mbinguni, na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia.”

Luka 2:10–15

Wachungaji wakimsalimia mtoto Yesu.

Wachungaji waliharakisha kwenda Bethlehemu na kumpata mtoto Yesu, kama vile malaika alivyosema. Waliwaambia watu kuhusu mambo ya kupendeza waliyokuwa wameyaona na kusikia. Walijua Yesu alikuwa mtoto maalum.

Luka 2:16–17

Simeoni akiwa amembeba mtoto Yesu.

Mariamu na Yusufu walimpeleka mtoto Yesu hekaluni ili kumkabidhi Yeye kwa Mungu. Hapo walikutana na mtu mmoja aliyeitwa Simeoni. Roho Mtakatifu alikuwa amemwambia Simeoni kwamba angekuja kukutana na Mwokozi kabla ya yeye kufa. Alimbeba mtoto na kusema Yesu angewaokoa watoto wote wa Mungu. Yusufu na Mariamu walistaajabishwa na yale aliyoyasema.

Luka 2:22–35

Anna akikutana na mtoto Yesu.

Hekaluni kulikuwa na mtu mwingine aliyeitwa Anna. Mume wake alikuwa amefariki miaka mingi iliyopita. Sasa Anna alitumia muda wake wote kumwabudu Mungu hekaluni. Alimshukuru Mungu kwa nafasi ya kukutana na Mwokozi. Wakati wowote alipokutana na mtu aliyekuwa akimsubiri Mwokozi, aliwaambia kuhusu Yesu.

Luka 2:36–38

Mamajusi wakiona nyota mpya ikitokea angani.

Wakati Yesu alipozaliwa, mamajusi katika nchi nyingine waliiona nyota mpya. Walijua ilimaanisha kwamba mtoto maalum alizaliwa ambaye angekuwa Mwana wa Mungu na Mwokozi wa ulimwengu. Walianza safari ndefu kumtembelea mtoto huyu na kumwabudu Yeye. Walitaka kumletea Yeye zawadi ili kuonyesha upendo wao Kwake.

Mathayo 2:1–7; ona Tafsiri ya Joseph Smith katika maelezo, 2a

Mamajusi wakimtafuta Mwokozi huko Yerusalemu.

Baada ya kusafiri kwa muda mrefu, mamajusi walikuja Yerusalemu. Walisema kwamba mfalme mpya wa Wayahudi, Mwokozi, alikuwa amezaliwa, na walikuwa wamekuja kumsujudia. Waliuliza wapi wangeweza kumpata mfalme mpya.

Mathayo 2:1–2

Herode akiwaambia watu wake wamtafute mfalme mpya.

Mfalme aliyeitwa Herode alisikia kwamba mamajusi walikuwa wanamtafuta mfalme mpya. Alikuwa na wasiwasi. Makuhani wake na waandishi walimwambia kwamba maandiko yalisema mfalme mpya angezaliwa Bethlehemu. Herode aliwaambia mamajusi watafute katika Bethlehemu na kisha warudi na kumwambia watakapompata mfalme mpya.

Mathayo 2:3–8

Mamajusi wakimsujudia mtoto Yesu.

Mamajusi walikuja Bethlehemu. Waliifuata nyota, ambayo iliwaongoza kwa Yesu. Walipompata Yeye na Mariamu na Yusufu, walimpa Yesu zawadi tatu maalum na kumsujudia. Mungu aliwaonya wasirudi kwa Herode, hivyo walienda nyumbani kwa njia nyingine.

Mathayo 2:9–12

Malaika akimwambia Yusufu kwamba anahitaji kuipeleka familia yake Misri.

Baada ya mamajusi kuondoka, Yusufu alipata ndoto. Katika ndoto, malaika alimwambia Yusufu kwamba Herode alikasirika. Yusufu alihitaji kuwapeleka Mariamu na Yesu hadi Misri ili kuwaweka salama.

Mathayo 2:13

Yusufu, Mariamu, na Yesu wakiondoka kwenda Misri.

Yusufu aliamka mara moja. Aliondoka kwenda Misri pamoja na Mariamu na Yesu wakati bado ni usiku.

Mathayo 2:14

Yusufu, Mariamu, na mtoto Yesu nyumbani.

Mariamu, Yusufu, na Yesu walikaa Misri mpaka malaika alipowaambia kwamba Herode alikuwa amekufa na ilikuwa salama kurudi. Kisha walirudi na kuishi katika Nazareti.

Mathayo 2:15, 19–23