Waefeso 2:19–20; 4:11–14
Katika Umoja wa Imani
Yesu Kristo analiongoza Kanisa Lake kupitia mitume na manabii.
Mitume wa Yesu waliihubiri injili Yake katika nchi nyingi. Watu walioiamini injili walibatizwa. Mtume Paulo alitaka kila mtu ajisikie kukaribishwa katika Kanisa la Mwokozi, hata kama walikuwa wanatoka sehemu tofauti tofauti.
Mathayo 28:19–20; Waefeso 2:19
Paulo aliandika barua kwa Watakatifu katika Efeso. Alisema kwamba Yesu alipokufa kwa ajili yetu, ilikuwa ni kama Yeye alivunja ukuta ambao uliwatenganisha watoto wa Mungu. Bila kujali chimbuko lao, hawakuwa wageni tena. Wangeweza kuipokea injili na kuwa sehemu ya “nyumba ya Mungu,” kama familia moja kubwa!
Waefeso 2:11–19
Paulo alisema kwamba Kanisa ni kama jengo imara. Majengo yanahitaji msingi imara. Jiwe muhimu zaidi katika msingi ni jiwe kuu la pembeni. Mawe mengine yote yanapangwa kufuata jiwe la pembeni. Yesu Kristo ni jiwe kuu la pembeni la Kanisa Lake.
Waefeso 2:20
Sehemu iliyobakia ya msingi wa Kanisa ni manabii na mitume, ambao wanamshuhudia Yesu Kristo. Bwana pia anatualika sote kusaidia kulijenga Kanisa Lake—kwa kufundisha, kwa kuhudumu, kwa kushiriki injili, na katika njia zingine nyingi.
Waefeso 2:20; 4:11–12
Kanisa linahitajika, Paulo alisema, ili kumsaidia kila mtu kumjua Yesu Kristo. Kanisa la Yesu Kristo lipo duniani leo, likiwa na msingi imara wa Yesu Kristo na manabii na mitume Wake. Kupitia Kanisa Lake, tunaweza kukua “katika umoja wa imani” na kuwa zaidi kama Yesu.
Waefeso 2:21–22; 4:13