Hadithi za Maandiko
Yesu Anafundisha Mahubiri ya Mlimani—Kutusaidia kuwa zaidi kama Baba yetu wa Mbinguni


Mathayo 5–7

Kristo Anafundisha Mahubiri ya Mlimani

Kutusaidia kuwa zaidi kama Baba yetu wa Mbinguni

Yesu akifundisha karibu na Bahari ya Galilaya.

Yesu na wanafunzi Wake walienda mlimani karibu na Bahari ya Galilaya. Huko Yesu aliwafundisha wao jinsi tunavyoweza kuwa na furaha na kuwa zaidi kama Baba yetu wa Mbinguni.

Mathayo 5:1–2

Yesu akifundisha kuhusu jinsi ya kuwa wapatanishi kwa wengine.

Yesu alifundisha kwamba watu wanabarikiwa na kuwa na furaha wanapokuwa wanyenyekevu, wasafi moyoni, na wanapojaribu kufanya kilicho sahihi. Watu wanaowasamehe wengine wanaweza kusamehewa. Watu wapatanishi wataitwa watoto wa Mungu.

Mathayo 5:3–9

Tunapaswa kuwa kama nuru kwa ajili ya ulimwengu.

Yesu alisema kwamba wanafunzi Wake ni nuru ya ulimwengu—kama mji juu ya mlima ambao kila mtu anaweza kuuona. Hatupaswi kuficha nuru yetu.

Mathayo 5:14

Matendo yetu mema yanaweza kuwa kama nuru kwa wengine.

Tunapomfuata Yesu, tunakuwa kama mshumaa ambao unatoa nuru kwa kila mtu chumbani. Matendo yetu mema yanaweza kuwasaidia watu kuamini katika Baba wa Mbinguni.

Mathayo 5:15–16

Yesu akifundisha kwamba tunapaswa kumpenda kila mtu.

Yesu alisema kwamba tunapaswa kumpenda kila mtu—hata watu ambao hawatupendi. Tunapaswa kusali kwa ajili yao. Yesu alifundisha kwamba tunapaswa kujaribu kuwa kama Baba yetu wa Mbinguni. Yeye alifundisha kwamba tunapowasaidia watu, hatupaswi kumwambia kila mtu kile tulichokifanya. Mungu huona mambo mazuri tunayofanya, na Yeye atatubariki.

Mathayo 5:38–48; Mathayo 6:1–4

Tunapaswa kusali kutoka mioyoni mwetu.

Tunaposali, hatupaswi kuwa na wasiwasi kuhusu kile watu wengine wanachofikiria juu yetu. Hatupaswi kusema maneno yale yale kila wakati kama kweli hatuyamaanishi. Tunapaswa kuzungumza kutoka mioyoni mwetu. Baba wa Mbinguni husikia sala zetu na anajua kile tunachohitaji. Hata kama hakuna yeyote mwingine anayeweza kutusikia, Yeye atatusikia.

Mathayo 6:5–8

Tunapaswa kuwatendea wengine jinsi ambavyo sisi tungependa kutendewa.

Yesu alifundisha kwamba hatupaswi kufikiri sisi ni bora kuliko watu wengine. Tunapaswa kukumbuka kwamba sote tuna changamoto. Badala ya kuwahukumu wengine, tunapaswa kufikiria kuhusu jinsi tunavyoweza kufanya vizuri zaidi. Tunapaswa kuwatendea watu jinsi tunavyotaka kutendewa.

Mathayo 7:1–5, 12

Yesu akifundisha kuhusu nyumba iliyojengwa juu ya mwamba.

Yesu kisha alisimulia hadithi kuhusu mtu mpumbavu aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga na mtu mwenye hekima ambaye alijenga nyumba yake juu ya mwamba. Mvua iliponyesha, nyumba juu ya mchanga ilianguka chini, na nyumba juu ya mwamba ikabaki imesimama. Yesu alisema kama tutasikia mafundisho Yake na kuyafuata, tunakuwa kama mtu mwenye hekima.

Mathayo 7:24–28