Mathayo 5–7
Kristo Anafundisha Mahubiri ya Mlimani
Kutusaidia kuwa zaidi kama Baba yetu wa Mbinguni
Yesu na wanafunzi Wake walienda mlimani karibu na Bahari ya Galilaya. Huko Yesu aliwafundisha wao jinsi tunavyoweza kuwa na furaha na kuwa zaidi kama Baba yetu wa Mbinguni.
Mathayo 5:1–2
Yesu alifundisha kwamba watu wanabarikiwa na kuwa na furaha wanapokuwa wanyenyekevu, wasafi moyoni, na wanapojaribu kufanya kilicho sahihi. Watu wanaowasamehe wengine wanaweza kusamehewa. Watu wapatanishi wataitwa watoto wa Mungu.
Mathayo 5:3–9
Yesu alisema kwamba wanafunzi Wake ni nuru ya ulimwengu—kama mji juu ya mlima ambao kila mtu anaweza kuuona. Hatupaswi kuficha nuru yetu.
Mathayo 5:14
Tunapomfuata Yesu, tunakuwa kama mshumaa ambao unatoa nuru kwa kila mtu chumbani. Matendo yetu mema yanaweza kuwasaidia watu kuamini katika Baba wa Mbinguni.
Mathayo 5:15–16
Yesu alisema kwamba tunapaswa kumpenda kila mtu—hata watu ambao hawatupendi. Tunapaswa kusali kwa ajili yao. Yesu alifundisha kwamba tunapaswa kujaribu kuwa kama Baba yetu wa Mbinguni. Yeye alifundisha kwamba tunapowasaidia watu, hatupaswi kumwambia kila mtu kile tulichokifanya. Mungu huona mambo mazuri tunayofanya, na Yeye atatubariki.
Mathayo 5:38–48; Mathayo 6:1–4
Tunaposali, hatupaswi kuwa na wasiwasi kuhusu kile watu wengine wanachofikiria juu yetu. Hatupaswi kusema maneno yale yale kila wakati kama kweli hatuyamaanishi. Tunapaswa kuzungumza kutoka mioyoni mwetu. Baba wa Mbinguni husikia sala zetu na anajua kile tunachohitaji. Hata kama hakuna yeyote mwingine anayeweza kutusikia, Yeye atatusikia.
Mathayo 6:5–8
Yesu alifundisha kwamba hatupaswi kufikiri sisi ni bora kuliko watu wengine. Tunapaswa kukumbuka kwamba sote tuna changamoto. Badala ya kuwahukumu wengine, tunapaswa kufikiria kuhusu jinsi tunavyoweza kufanya vizuri zaidi. Tunapaswa kuwatendea watu jinsi tunavyotaka kutendewa.
Mathayo 7:1–5, 12
Yesu kisha alisimulia hadithi kuhusu mtu mpumbavu aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga na mtu mwenye hekima ambaye alijenga nyumba yake juu ya mwamba. Mvua iliponyesha, nyumba juu ya mchanga ilianguka chini, na nyumba juu ya mwamba ikabaki imesimama. Yesu alisema kama tutasikia mafundisho Yake na kuyafuata, tunakuwa kama mtu mwenye hekima.
Mathayo 7:24–28