“Ufunuo kwa ajili ya Emma,” Hadithi za Mafundisho na Maagano (2024)
“Ufunuo kwa ajili ya Emma,” Hadithi za Mafundisho na Maagano
Julai 1830
Ufunuo kwa ajili ya Emma
Aliteuliwa na Bwana ili kufanya kazi Yake
Maisha yalikuwa yakibadilika haraka sana kwa Emma na Joseph. Bwana alimwambia Joseph kwamba anapaswa kuacha kufokasi kwenye kilimo. Badala yake, Joseph anapaswa kutumia muda wake kuwafundisha watu kuhusu Yesu Kristo na kusaidia Kanisa la Bwana kukua.
Mafundisho na Maagano 24:7–9; Saints, 1:96
Emma alikuwa na maswali mengi kuhusu badiliko hili. Hakujua kile alichopaswa kufanya wakati Joseph alipokuwa akimtumikia Bwana. Je, yeye pia angemsaidia Bwana na Kanisa Lake?
Saints, 1:96
Bwana aliongea na Emma kupitia ufunuo uliotolewa kwa Joseph. Alimwita “Emma Smith, binti yangu.” Alimwambia Emma kwamba alikuwa amemteua na kumwita kufanya kazi Yake. Alikuwa mwanamke maalumu, na alikuwa na mambo makubwa ya yeye kufanya.
Bwana alimwomba Emma kusafiri pamoja na Joseph. Bwana alisema kwamba Emma angeelezea maandiko na kuwafundisha waumini wa Kanisa. Alimwambia Emma amweke Yeye kwanza katika maisha yake na kushika maagano yake. Alimuahidi Emma angekuwa na Roho Wake. Alimtaka ajifunze, akue, na kupokea baraka Zake.
Mafundisho na Maagano 25:2, 6–10, 15.
Bwana pia alimwambia Emma kwamba Yeye anapenda kuwasikia watoto Wake wakiimba. Alisema nyimbo za Watakatifu Wake ni kama sala Kwake. Alimwomba Emma kutengeneza kitabu cha nyimbo ambazo Watakatifu wangeweza kuimba kutoka humo kwa pamoja. Emma alipata nyimbo nyingi nzuri kuhusu Bwana na injili Yake na kuziweka kwenye kitabu cha nyimbo za dini.
Mafundisho na Maagano 25:11–12; Saints, 1:221–22
Maisha ya Emma na Joseph yaliendelea kubadilika, lakini Emma alijua kwamba Bwana alimpenda na alikuwa na lengo kwa ajili yake. Alimtumikia Bwana na watu waliomzunguka. Alisaidia Kanisa la Yesu kukua.
Mafundisho na Maagano 25:13–15; Saints, 1:221–23