“Mzee Wan-Liang Wu,” Liahona, Mei 2025.
Mzee Wan-Liang Wu
Sabini Mkuu mwenye Mamlaka
Wakati Mzee Wan-Liang Wu alipokuwa na miaka 10, familia yake ilihama kutoka Taiwan kwenda Bolivia. Ilikuwa hapo ambapo dada zake walikutana na wamisionari kupitia marafiki. Alianza kukutana na wamisionari na alibatizwa akiwa naumri wa miaka 11.
Kuzoea makazi mapya kulithibitika kuwa changamoto, lakini anashukuru kuhama kwa familia yake. “Nilipoteza kitu fulani ili kuwa na vitu vizuri zaidi katika njia bora ya Bwana,” alisema.
Wan-Liang Wu alizaliwa mjini Taipei, Taiwan, mnamo Desemba 22, 1970, mtoto wa mwisho wa Chang Yung Wu na Bao Guey Lin. Ana dada watatu na kaka mmoja.
Baada ya familia yake kuhamia Santa Cruz, Bolivia, walihamia Buenos Aires, Ajentina, alipokuwa na umri wa miaka 14. Baada ya huduma katika Misioni ya China Hong Kong, alimuoa Marcela Beatriz Castellani mnamo Machi 17, 1995, katika Hekalu la Buenos Aires Ajentina. Wana watoto watatu.
Yeye na Marcela walimiliki na kusimamia duka la familia yao la vyakula huko Buenos Aires. Amelifanyia kazi Kanisa tangu mwaka 2007, kwanza katika Idara ya Nyumba za Mikutano na kisha, mwaka 2016, kama meneja wa uendeshaji na matengenezo katika Amerika ya Kusini Eneo la Kusini.
Mzee Wu alipata shahada ya kwanza katika utawala wa biashara kutoka Chuo Kikuu cha Ajentina de la Empresa mwaka 2014 na shahada ya uzamili ya utawala wa biashara kutoka Universidad del CEMA huko Buenos Aires mwaka 2020.
Wakati wa wito wake, Mzee Wu alikuwa akihudumu kama rais wa Misioni ya Chile Antofagasta. Pia amehudumu kama rais wa kigingi, mshauri katika urais wa kigingi, askofu, rais wa akidi ya wazee, karani wa kata, mshauri katika urais wa akidi ya wazee, na mhudumu wa ibada za hekaluni.