Msishupaze Mioyo Yenu
Ikiwa tutatubu kwa dhati, kujinyenyekeza na kumtumaini na kumtegemea Bwana, mioyo yetu italainishwa.
Urejesho wa injili ya Yesu Kristo ulianza wakati Mungu Baba na Mwanaye Mpendwa walipomtokea kijana Joseph Smith, wakijibu sala yake ya unyenyekevu. Kama sehemu ya Urejesho, Joseph Smith alitafsiri kumbukumbu ya kale kwa kipawa na uwezo wa Mungu. Kumbukumbu hii ina “matendo ya Mungu kwa kikundi cha wakazi wa kale wa bara la Amerika na inayo utimilifu wa injili isiyo na mwisho.”
Nilipokuwa kijana mdogo, wakati nikisoma Kitabu cha Mormoni, mara nyingi nilijiuliza kwa nini Lamani na Lemueli hawakuamini kweli zilizotolewa kwao, hata wakati malaika wa Bwana alipowatokea na kuzungumza nao moja kwa moja. Kwa nini Lamani na Lemueli hawakuweza kuwa wanyenyekevu na watiifu kwa mafundisho ya Lehi, baba yao na Nefi, mdogo wao?
Nilipata moja ya majibu ya swali hili katika 1 Nefi, ambayo inasema kwamba Nefi “alihuzunishwa na ugumu wa mioyo yao.” Nefi aliwauliza kaka zake, “Je, kwa nini mna ugumu mioyoni mwenu na upofu katika akili zenu?”
Inamaanisha nini kuwa na ugumu wa moyo?
Tafsiri ya Kikorea ya “ugumu” katika Kitabu cha Mormoni ni 완악 (Wan-Aak: 頑惡). Kirai hiki kinatumia herufi za Kichina “Wan” (頑), ikimaanisha “msumbufu,” na “Aak” (惡), ikimaanisha “mwovu.” Tunaposhupaza mioyo yetu, tunapofushwa macho na mambo mazuri hayawezi kuja ndani ya mioyo yetu au akili zetu. Tunakuwa wasumbufu na kuanza kuweka fokasi zaidi kwenye matamanio ya ulimwengu, tukiifunga mioyo yetu dhidi ya mambo ya Mungu. Tunachagua kufokasi kikamilifu kwenye mawazo yetu wenyewe na kutokubali maoni na mwongozo wa wengine. Tunachagua kutoifungua mioyo yetu kwa mambo ya Mungu lakini badala yake kwenye ushawishi wa mambo ya ulimwengu na adui. Mioyo yetu inaposhupazwa, tunapinga ushawishi wa Roho Mtakatifu. Tunakuwa “wanyonge kumkumbuka Bwana,” na baada ya muda “tunakufa ganzi” kwenye maneno Yake.
Alma aliwafunza watu katika Amoniha kwamba wengine “wangemkataa Roho wa Mungu kwa ajili ya ugumu wa mioyo yao.” Alifundisha pia kwamba “wale watakaoshupaza mioyo yao, watapewa sehemu ndogo ya neno hadi wasijue lolote kuhusu siri zake.” Hatimaye, Roho huondoka, na Bwana “ataondoa neno [Lake]” kutoka kwa wale walioshupaza mioyo yao, kama vile Lamani na Lemueli. kwa sababu Lamani na Lemueli mara nyingi walishupaza mioyo yao, walikataa hisia za Roho Mtakatifu na kuchagua kukataa maneno na mafundisho ya baba yao na Nefi, hatimaye walikataa kweli za milele kutoka kwa Mungu.
Kinyume cha Lamani na Lemueli, Nefi mara zote alijinyenyekeza, akitafuta mwongozo kutoka kwa Roho wa Bwana. Kama matokeo, Bwana aliulainisha moyo wa Nefi. Nefi anashiriki kwamba “nilimlilia Bwana, na tazama akanijia mimi, na akanigusa moyo wangu kwamba nikaamini maneno yote ambayo baba yangu alikuwa ameyazungumza.” Bwana alimsaidia Nefi kukubali, kuelewa na kuamini siri zote za Mungu na maneno Yake. Nefi aliweza kuwa na wenza wa daima wa Roho Mtakatifu.
Ni kipi tunaweza kufanya ili tusishupaze mioyo yetu?
Kwanza, tunaweza kufanyia kazi toba ya kila siku.
Mwokozi wetu alifundisha, “Yeyote anayetubu na kuja kwangu kama mtoto mdogo, yeye nitampokea.” Nabii wetu mpendwa Rais Russell M. Nelson, amefundisha:
“Kutubu ni ufunguo wa maendeleo. Imani safi hutufanya tusonge mbele kwenye njia ya agano.
“Tafadhali usiogope au usichelewe kutubu. Shetani anafurahia huzuni yako. … Anza leo kupata uzoefu wa shangwe ya kumvua mtu wa tabia ya asili. Mwokozi anatupenda siku zote lakini hasa wakati tunapotubu.”
Tunapopata uzoefu wa shangwe ya kulainisha mioyo yetu na kuja kwa Bwana, tunakuwa “kama mtoto mdogo, mtiifu, mpole, mnyenyekevu, mvumilivu, mwenye upendo tele, aliye tayari kukubali vitu vyote ambayo Bwana anaona sahihi kuviweka juu yake, hata kama vile ambavyo mtoto hunyenyekea kwa baba yake.”
Pili, tunaweza kufanyia kazi unyenyekevu.
Toba ya kila siku italeta unyenyekevu kwenye mioyo yetu. Tunataka kuwa wanyenyekevu mbele za Bwana, kama vile mtoto mdogo anavyomtii baba yao. Kisha tutakuwa na Roho Mtakatifu pamoja nasi na mioyo yetu italainishwa.
Mimi na mke wangu Sue, tumewajua wanandoa wa kupendeza kwa miaka minne iliyopita. Mara ya kwanza kukutana nao, mume alikuwa muumini mpya wa Kanisa na mkewe alikuwa akikutana na wamisionari ili kujifunza injili. Wamisionari wengi walikutana naye ili kumsaidia aje kwa Kristo. Tulihisi kwamba alikuwa na ushuhuda hai wa injili na alijua kwamba Kanisa lilikuwa la kweli. Alimhisi Roho mara zote wakati wa matembezi yetu na alishiriki kikamilifu katika mikutano yote. Alipenda kuchangamana na waumini wema wa kata. Hata hivyo, alipata ugumu sana kujiwekea msimamo wa kuingia kwenye maji ya ubatizo. Siku moja alikuwa akisoma Moroni 7:43–44, ambayo inasomeka:
“Na tena, tazama ninawaambia kwamba hawezi kuwa na imani na tumaini, isipokuwa awe mnyenyekevu, na mpole katika moyo.
“Ikiwa hivyo, imani na tumaini [lako] ni bure, kwani hakuna yeyote anayekubaliwa mbele ya Mungu, isipokuwa yule aliye myenyekevu na mpole katika moyo.”
Baada ya kusoma mistari hii, alitambua kile alichopaswa kukifanya. Alidhani kwamba alikuwa ameelewa maana ya kuwa mpole na mnyenyekevu. Hata hivyo, uelewa wake haukutosha kuwa na imani na tumaini kwenye kutii amri za Mungu. Ilibidi aachilie usumbufu wake na hekima yake mwenyewe. Alianza kujinyenyekeza kupitia toba ya dhati. Alianza kuuelewa unyenyekevu katika mtazamo wa macho ya Mungu. Alimtegemea Baba wa Mbinguni na alisali ili kuulainisha moyo wake mwenyewe. Kupitia sala hizi, alimhisi Roho akimshuhudia kwamba Baba wa Mbinguni alimtaka abatizwe.
Wote mume na mke walishiriki kwamba kadiri walivyokuwa wanyenyekevu, ndivyo zaidi walivyoelewa maneno ya Mungu na mioyo yao ililainishwa ili kufuata mafundisho ya Bwana, Yesu Kristo.
Tatu, tunaweza kumtumaini na kumtegemea Mwokozi wetu.
Nefi alikuwa mfano mkuu wa kuuruhusu moyo wake ulainishwe kwa kumtumaini Bwana. Alifundisha, “Nimekutumaini, na nitakutumaini milele. Sitaweka tumaini langu kwenye mkono wa mwanadamu.” Kadhalika, katika ufunuo uliotolewa kwa Nabii Joseph Smith, Bwana alisema, “Weka tumaini lako katika Roho yule ambaye huongoza kufanya mema—ndiyo, kufanya haki, kutembea kwa unyenyekevu.” Tunapoweka tumaini letu kwa Bwana na kumtegemea Yeye, atailainisha mioyo yetu na tutasaidiwa katika majaribu yetu, magumu yetu na masumbuko yetu.
Ikiwa tutatubu kwa dhati, kujinyenyekeza na kumtumaini na kumtegemea Bwana, mioyo yetu italainishwa. Ndipo Yeye ataimimina Roho Yake na kutuonesha siri za mbinguni. Tutaamini maneno yote ambayo Ameyafundisha na uelewa wetu utaongezeka.
Mwokozi wetu Yesu Kristo alikuwa mfano wa juu zaidi wa unyenyekevu. Katika 2 Nefi 31:7, tunasoma, “Lakini ingawa alikuwa mtakatifu, anawaonyesha watoto wa watu kwamba, kulingana na mwili anajinyenyekeza mbele ya Baba, na kumshuhudia Baba kwamba yeye atakuwa mtiifu kwake katika kutii amri zake.” Japokuwa alikuwa mtakatifu na mkamilifu, Yeye alijinyenyekeza mbele ya Baba na alikuwa mtiifu Kwake kwa kubatizwa.
Mwisho wa maisha Yake, Yesu Kristo aliweka mapenzi Yake chini ya mapenzi ya Baba Yake kwa kukinywea kikombe kichungu. Mateso haya yalimsababisha Yeye “kutetemeka kwa sababu ya maumivu, na kutoka damu kwenye kila kinyweleo, na kuteseka mwili na roho.” Mwokozi aliomba kwamba “asinywe kikombe kichungu na kusita.” Hata hivyo, Yeye alisema, “utukufu na uwe kwa Baba, na [Yeye] akachukua na kukamilisha maandalizi [Yake] kwa ajili ya watoto wa wanadamu.”
Akina kaka na akina dada, tumepewa haki ya kujiamulia. Tunaweza kuchagua kuishupaza mioyo yetu au tunaweza kuchagua kuilainisha mioyo yetu. Katika maisha yetu ya kila siku, tunaweza kuchagua kufanya mambo yanayomwalika Roho wa Bwana kuja na kukaa ndani ya mioyo yetu. Ninajua kwamba katika chaguzi hizi, kuna amani na shangwe.
Acha tufuate mfano wa Mwokozi wetu Yesu Kristo, ambaye alifuata mapenzi ya Baba. Tunapofanya hivyo, Bwana ametuahidi, “Kwani, tazama, nitawakusanya wao kama vile kuku avikusanyavyo vifaranga vyake chini ya mabawa yake, kama hawataishupaza mioyo yao.” Katika jina la Yesu Kristo, amina.