2025
“Nirudie Mimi … Ili Niweze Kukuponya”
Mei 2025


11:3

“Nirudie Mimi … Ili Niweze Kukuponya”

Kuna furaha mbinguni juu ya wale wanaorudi. Bado hujachelewa kwa ajili yako kurudi.

Tuliwahi kuishi katika nyumba iliyozungukwa na miti mikubwa. Kando ya mlango huo kulikuwa na mti wa muerebi mzuri. Usiku mmoja wa huzuni dhoruba kali ilivuma, na muerebi ukaanguka chini. Ulilala chini na mizizi yake kung’olewa na ilikuwa hali ya kuhuzunisha.

Nilikuwa tayari kuwasha msumeno na kuukata mti huo kwa ajili ya kuni wakati jirani yetu alipotoka mbio kunizuia. Alinionya kwa kukata tamaa juu ya ule mti, na yeye akatusihi kwa msisitizo tusiuondoe. Kisha akaonyesha mzizi mmoja uliokuwa chini na kusema kwamba tukiuegemeza mti huo juu, tukate matawi yake, na kuulisha, mizizi itatokezea tena.

Mti wa muerebi alioanguka chini.
Mzizi mmoja wa mti uliobaki mchangani.

Sikuwa na hakika na nilitilia shaka jinsi mti ulioanguka na kuwa na matatizo, ungeweza kunusurika na kufufuka. Niliwaza kwamba hata kama ungeanza kukua tena, hakika hautahimili dhoruba inayofuata. Lakini kwa kujua jirani yetu aliamini mti bado una kesho yake, tulikubaliana na mpango huo.

Shina tupu la mti.
Ishara za ukuaji kwenye mti.

Na matokeo? Baada ya muda, tuliona dalili za uhai pale mti huo ulipoanza kuota. Sasa, miaka 12 baadaye, mti huo unachangamka na umejaa uhai, na mizizi yenye nguvu na kwa mara nyingine tena unachangia uzuri wa mazingira.

Mti uliochangamka na wenye afya.

Wakati ninapokutana na Watakatifu kote ulimwenguni, ninakumbushwa juu ya mti wa muerebi huu na kwamba kuna matumaini hata wakati yote yanaonekana kupotea. Baadhi wakati fulani walikuwa na ushuhuda wa injili ambao ulikuwa na nguvu na mahiri kama mti wa muerebi. Kisha, kwa sababu za kipekee za kibinafsi, shuhuda hizo zikadhoofika, na kusababisha kupoteza imani. Wengine huning’inia na mizizi dhaifu zaidi iliyoshikilia kwenye udongo wa injili.

Bado tena na tena, nimetiwa moyo na hadithi za wengi sana ambao wamechagua kufanya upya uanafunzi wao na kurudi kwenye nyumba zao za Kanisa. Badala ya kutupa imani yao kama kuni zisizofaa, badala yake wameitikia misukumo ya kiroho na mialiko ya upendo ya kurudi.

Nilihudhuria mkutano wa kigingi nchini Korea ambapo mshiriki aliyerejea alishiriki: “Ninawashukuru akina kaka kwa utayari wao wa kukubali ukosefu wangu wa imani na udhaifu wangu, kwa kunifikia, na kwa waumini ambao daima wamekuwa wema kwangu. Bado nina marafiki wengi karibu nami ambao hawahudhurii kikamilifu. Inachekesha, lakini wanaambiana warudi Kanisani ili kurudisha imani yao. Nadhani labda wote wanatamani imani.”

Kwa wote wanaotamani imani, tunawaalika mrudi. Ninaahidi imani yako inaweza kuimarishwa unapoabudu tena pamoja na Watakatifu.

Mmisionari wa zamani kutoka Afrika alimwandikia kiongozi mwandamizi wa Kanisa, akitubu na kuomba msamaha kwa kukerwa na mafundisho yake kuhusu desturi fulani ya kitamaduni, ambayo yalimfanya aachane na Kanisa. Alisema kwa unyenyekevu: “Inasikitisha, uhalisia kwamba nilikereka miaka 15 iliyopita imenifanya nilipe gharama kubwa sana. Nilipoteza sana—zaidi ya nilivyowahi kufikiria. Nimeaibishwa sana na madhara ambayo huenda nimesababisha njiani, lakini zaidi ya yote ninafurahi kwamba nimepata njia yangu ya kurudi.”

Kwa wote wanaotambua kile ambacho mmepoteza, tunawaalika mrudi ili muweze kuonja tena matunda ya furaha ya injili.

Dada mmoja huko Marekani alikuwa ametoka Kanisani kwa miaka mingi. Hadithi yake ya kurudi ni pamoja na masomo ya nguvu kwa wazazi na wanafamilia ambao wana huzuni juu ya wapendwa wao wanaoondoka. Aliandika:

“Ningeweza kuorodhesha maelfu ya sababu za kwa nini nilienda mbali na Kanisa, injili na kwa njia fulani, familia yangu. Lakini kwa kweli haijalishi. Sikufanya uamuzi mmoja mkubwa wa kuacha Kanisa—pengine nilifanya chaguzi elfu moja. Lakini jambo moja ambalo nimekuwa nikijua ni kwamba wazazi wangu walifanya uamuzi mmoja mkubwa, na waliushikilia kikamilifu. Waliamua kunipenda.

“Nisingeweza kujua ni machozi mangapi yamemwagika, siku ngapi za kukosa usingizi, wala ni maneno mangapi ya kusihi ya kutoka moyoni ambayo yamesemwa kwa niaba yangu. Hawakunikosoa mimi kwenye dhambi zangu; bali walikosoa hali yangu ya dhambi. Hawakunifanya nihisi kutokubalika nyumbani kwao na kwenye mikusanyiko ya familia; hisia zozote zile zilikuwa zangu mwenyewe. Badala yake, waliendelea kunikaribisha. Lazima wangeiona nuru yangu ikififia kwa muda. Lakini walijua kwamba mtu niliyekuwa wakati huo alikuwa kivuli tu cha nani ningekuwa bado.

“Kama vile njia yangu kutoka kwa Kanisa ilikuwa tata, ndivyo ilivyokuwa njia yangu ya kurudi. Lakini jambo moja ambalo halikuwa gumu kurudi ni hisia ya kurudi nyumbani mahali pangu.”

Ujumbe wangu leo hasa ni kwa wote waliowahi kuhisi Roho lakini wanahoji kama kuna njia ya kurudi au nafasi kwenu katika Kanisa la urejesho la Yesu Kristo. Vile vile ni kwa wale wote ambao wananing’inia tu au wale ambao wanajaribiwa kuondoka.

Ujumbe huu sio changamoto, na sio lawama. Ni mwaliko, unaotolewa kwa upendo na nia ya dhati ya kukukaribisha tena kwenye nyumba yako ya kiroho.

Nimeomba kwamba mtahisi ushuhuda wa Roho Mtakatifu mnaposikia sasa mwaliko huu wa upendo na ahadi kuu kutoka kwa Mwokozi wetu, Yesu Kristo:

”Je, mtarudi kwangu sasa, na kutubu dhambi zenu, na kugeuka ili niwaponye?”

Kila wiki wengi wanaitikia mwaliko wa Mwokozi kwa kurudi kwenye uanafunzi na shughuli za Kanisa, kwa utulivu na unyenyekevu wakitafuta uponyaji ambao Yesu anaahidi. Na kinyume na masimulizi ambayo nyakati fulani husambaa, idadi kubwa ya vijana wetu wanachagua kuwa imara na kukuza imani yao katika Yesu Kristo.

Wakati baadhi ya wafuasi wa Yesu huko Kapernaumu walipoona mafundisho Yake kuwa magumu na wakachagua kuondoka, Yeye aliwageukia Mitume Wake na kuwauliza, “Je, ninyi pia mtaondoka?”

Hili ndilo swali ambalo kila mmoja wetu anapaswa kujibu tunapokabiliana na nyakati zetu binafsi za majaribio. Jibu la Petro kwa Yesu ni la kudumu na linalojulikana sana: “Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.”

Kwa hivyo unapofikiria mwaliko wa Mwokozi wa kurudi Kwake, unaweza kujifunza nini kutoka kwenye hadithi ya mti wa muerebi?

  1. Safari ya kurudi mara nyingi si rahisi au ya kufariji, lakini inafaa. Mti wa muerebi ulisimamishwa, matawi yake yote yalikatwa. Haukuwa vizuri. Sisi pia huenda tukahisi hatari tunapoziacha njia za zamani na kuvua kiburi. Fokasi imani yako kwa Yesu Kristo na injili Yake—shina na mizizi—kutakupa tumaini na ujasiri wa kuchukua hatua hiyo ya kwanza ili kurejea.

  2. Ilichukua miaka mingi kwa mti wetu wa muerebi kupata nguvu na uzuri wake wa zamani. Sasa ni imara zaidi na mzuri zaidi kuliko hapo awali. Kuwa mvumilivu kadiri imani yako na ushuhuda unavyokua. Hii inajumuisha kutokerwa na maoni yasiyo na maana kama vile “Umekuwa wapi miaka hii yote?”

  3. Muerebi usingeweza kuishi bila utunzaji na lishe ya kila wakati. Utalisha imani yako na ushuhuda wako unapokula kwenye meza ya sakramenti kila wiki na unapoabudu katika nyumba ya Bwana.

  4. Kama vile muerebi ule ulihitaji mwanga wa jua kwa matawi na majani yake kukua tena, vivyo hivyo ushuhuda wako utakua unapoendelea kuwa makini kwa hisia na ushuhuda wa Roho. Jifunze kutoka kwa Amuleki, ambaye alielezea muda wake kama muumini asiyeshiriki kikamilifu kwa kusema, “Niliitwa mara nyingi na sikusikia.”

  5. Jirani yangu alijua kile muerebi ungeweza kuwa siku moja. Hivyo pia Bwana anajua uwezo wako wa kiungu na imani yako na kile ushuhuda wako unaweza kuwa. Kamwe Yeye hatakata tamaa juu yako. Kupitia Upatanisho wa Yesu Kristo, yote ambayo yamevunjwa yanaweza kuponywa.

Ninashuhudia kwamba kuna furaha mbinguni juu ya wale wanaorudi. Unahitajika, na unapendwa. Ninashuhudia kwamba Yesu Kristo ni Mwokozi wetu na kwamba Yeye hubariki wote ambao wanarudi Kwake kwa amani kuu na shangwe kuu. Mikono yake ya rehema haijakunjwa bali iko wazi na imenyooshwa kwako. Bado hujachelewa kwa ajili yako kurudi. Kwa upendo wote katika mioyo yetu, tunawakaribisha nyumbani. Katika jina la Yesu Kristo, amina.

Muhtasari

  1. Hili lilikuwa na bado ndilo makao ya misheni kwa Misheni ya Washington Spokane. Picha za mti wa Muerebi zilipigwa na mke wangu, Jacqui.

  2. 3 Nefi 9:13. Kumbuka kwamba mwaliko wa kutubu unatuhusu sisi sote. Ona 1 Yohana 1:8 (“Tukisema kwamba hatuna dhambi, tunajidanganya wenyewe,”) na mwaliko wa Rais Russell M. Nelson wa kutubu kila siku, “Nguvu ya Msukumo wa Kiroho,” Liahona, Mei 2022, 98–99.

  3. Ona Quentin L. Cook, “Facing Life and Faith Challenges” (worldwide devotional for young adults, Nov. 14, 2023),“Kwa taarifa yako, vijana na watu wazima vijana hawana kiwango cha chini ya uhudhuriaji au hawanaachi Kanisa kwa idadi kubwa kuliko ilivyokuwa zamani kama ilivyosambazwa sana. Idadi ya wamisionari walioitwa kuhudumu imeongezeka sana. Asilimia ya ushiriki wa Kanisa kwa kizazi kinachoinuka inaonyesha mwelekeo unaoendelea wa kupanda. Zaidi ya hayo, idadi ya vijana wanaohudhuria chuo pia imekuwa ikiongezeka.”

    Ona pia D. Todd Christofferson and Clark G. Gilbert, “Video: Elder Christofferson Challenges Narrative, Says Spirit Working in Youth,” Church News, Dec. 13, 2024, newsroom.ChurchofJesusChrist.org.

  4. Yohana 6:67.

  5. Yohana 6:68.

  6. Ona Alma 5:28.

  7. Ona Dieter F. Uchtdorf, “Lisha Mizizi, na Matawi Yatakua,” Liahona, Nov. 2024, 102: “Yesu Kristo na dhabihu Yake ya upatanisho ni mizizi ya ushuhuda wetu. Vitu vingine vyote ni matawi. … Pale inapohusiana na kulisha shuhuda zetu za Yesu Kristo, huenda wakati mwingine tunakosea matawi kwa mizizi. … Lisha mizizi, na matawi yatakua.”

  8. Ona Alma 32:41.

  9. Ona Russell M. Nelson, “Fikiria Selestia!,” Liahona, Nov. 2023, 119: “Kutumia muda zaidi hekaluni hujenga imani. Na huduma na kuabudu kwenu hekaluni vitawasaidia kufikia selestia.

    Ona Russell M. Nelson, “Shangilia katika Zawadi ya Funguo za Ukuhani,” Liahona, Mei 2024; 3 Nefi 27:9–11: Hapa kuna ahadi. Hakuna kitakachokusaidia ushikilie kwa nguvu zaidi kwenye fimbo ya chuma kuliko kuabudu hekaluni. … Hakuna kitakachoimarisha ushuhuda wako juu ya Bwana Yesu Kristo na Upatanisho Wake au kukusaidia uelewe mpango mkuu wa Mungu vizuri zaidi.

  10. Ona Alma 32:28.

  11. Alma 10:6

  12. Ona Patrick Kearon, “Kusudi la Mungu Ni Kukuleta Nyumbani,” Liahona, Mei 2024, 87.

  13. Ona Jeffrey R. Holland, “Mambo Yaliyovunjika Yatarekebishwa,” Liahona,Mei 2006, 69–71.

  14. Ona Luka 15:11–32; Mafundisho na Maagano 18:13.

  15. Ona Yohana 15:9.

  16. Ona Alma 5:33.

  17. Ona Russell M. Nelson, “Bwana Yesu Kristo Atakuja Tena,” Liahona, Nov. 2024, 122: “Si mapema wala muda haujapita wa wewe kuwa mwanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo. Kisha utapata uzoefu mkamilifu wa baraka za Upatanisho Wake.

    Ona pia Russell M. Nelson, “Nguvu ya Msukumo wa Kiroho,” 99: “Ikiwa unahisi umepotoka nje ya njia ya agano kitambo sana au kwa muda mrefu sana na hauna njia ya kurudi, hiyo si kweli.”