Kushiriki kwenye Kujitayarisha Kwa ajili ya Ujio wa Kristo
Miito na njia zingine tunazotumia katika kazi ya Mungu kiupekee hututayarisha kukutana na Mwokozi.
Miezi michache iliyopita, nilikuwa nimesimama kwenye ukumbi wakati Mzee Neil L. Andersen alipopita. Ilikuwa si muda mrefu tangu nilipoitwa kama kiongozi Mkuu mwenye Mamlaka. Pengine akihisi hisia zangu za kujiona kutotosha, alitabasamu na kusema, “Inaonekana kuna mtu ambaye hajui anachofanya.”
Ndipo niliwaza, “Kuna nabii na mwonaji wa kweli.”
Mzee Andersen kisha alinong’ona, “Usijali, Mzee Shumway. Utakuwa bora—katika miaka mitano au sita.”
Je, umewahi kujiuliza ni kwa nini tunaombwa kufanya mambo katika ufalme wa Mungu ambayo yanaonekana kuwa nje ya uwezo wetu? Pamoja na mahitaji ya maisha, je, umejiuliza hata kwa nini tunahitaji miito katika Kanisa? Mimi nimejiuliza.
Nilipata jibu katika mkutano mkuu wakati Rais Russell M. Nelson aliposema, “Sasa ni wakati wako na wangu kujiandaa kwa ajili ya Ujio wa Pili wa Bwana na Mwokozi wetu, Yesu Kristo.” Aliposema hivi, Roho alinifundisha kwamba tunaposhiriki katika kazi ya Mungu, tunajitayarisha wenyewe na kuwatayarisha wengine kwa ajili ya kurudi kwa Kristo. Ahadi ya Bwana inatoa msukumo kwamba miito, kuhudumu, ibada ya hekaluni, kufuata maongozi, na njia zingine tunazozitumia katika kazi ya Mungu kwa njia ya kipekee hututayarisha kukutana na Mwokozi.
Mungu Hufurahia Tunapojihusisha Kwenye Kazi Yake
Katika “ukuu wa wakati huu,” wakati ufalme wa Mungu unatanuka na mahekalu yanaenea duniani, kuna ongezeko la uhitaji wa nafsi zilizo tayari kushiriki katika kazi ya Mungu. Kutumikia pasipo ubinafsi ni kiini hasa cha uanafunzi kwa Kristo. Lakini kutumikia si mara zote kitu kipendwacho. Hii ndio sababu ninavutiwa nanyi wanafunzi wenye kushika agano ambao mnaweka kando matamanio na changamoto zenu ili kumtumikia Mungu kwa kuwahudumia watoto Wake. Mungu “hufurahia kuwaheshimu [wale wanaomtumikia Yeye] kwa haki.” Yeye anaahidi, “Tuzo [lao] litakuwa kuu na utukufu [wao] utakuwa wa milele.” Tunapoitikia ndiyo katika kutumikia, tunasema ndiyo kwa Yesu Kristo. Na tunaposema ndiyo kwa Kristo, tunasema ndiyo kwa maisha tele zaidi kadiri iwezekanavyo.
Nilijifunza haya nilipokuwa nikifanya kazi na kusomea uhandisi wa kemikali chuoni. Niliombwa kuwa mratibu wa shughuli kwenye kata ya waseja. Huu ulikuwa wito wangu wa kuogopesha. Bado, nilikubali na hapo mwanzoni ulikuwa mgumu. Kisha katika shughuli moja msichana mrembo alipovutiwa na namna nilivyogawa ice cream. Alirudi mara tatu, akitumaini kupata umakini wangu. Tulipendana, na tuliingia kwenye uchumba wiki mbili baadaye. Sasa, labda haikuwa haraka kiasi hicho, na mimi ndiye niliyependekeza, lakini ukweli ni kwamba: ninatetemeka kufikiria kukosa kukutana na Heidi ikiwa ningekataa wito ule.
Kushiriki Kwetu ni Kujitayarisha Kwa ajii ya Ujio wa Kristo
Tunajishughulisha na kazi ya Mungu si kwa kuwa Mungu anatuhitaji isipokuwa sisi tunamhitaji Mungu na baraka zake. Yeye anaahidi, “Kwani, tazama, Mimi nitawabariki wale wote watakaofanya kazi katika shamba langu la mzabibu kwa baraka kuu.” Acha nishiriki kanuni tatu ambazo zinafundisha jinsi ushiriki wetu katika kazi ya Mungu hutubariki na kutusaidia kujitayarisha kukutana na Mwokozi.
Kwanza, tunaposhiriki, tunasonga mbele kuelekea “kipimo cha uumbaji [wetu]”
Tunajifunza muundo huu katika tukio la Uumbaji. Baada ya kila siku ya kazi, Mungu alikubali maendeleo yaliyofanywa kwa kusema “ilikuwa njema.” Hakusema kazi ilimalizika au kukamilika. Lakini alichosema kilikuwa kwamba kulikuwa na maendeleo, na machoni pa Mungu hiyo ni njema!
Miito haiamui au kuidhinisha thamani au ustahili wa mtu. Hakika, tunapofanya kazi pamoja na Mungu katika njia yoyote ile , tunakua katika kipimo cha uumbaji wetu wenyewe.
Mungu anafurahia maendeleo yetu, na sisi pia tunapaswa kufurahia hata kama bado tunayo kazi ya kufanya. Wakati fulani, tunaweza kukosa nguvu au njia za kutumikia katika wito. Bado, tunaweza kujishughulisha katika kazi na kuulinda ushuhuda wetu kupitia njia za maana kama vile sala na kujifunza maandiko. Baba yetu wa Mbinguni mwenye upendo hatuhukumu tunapokuwa na utayari lakini tunashindwa kutumikia.
Pili, kutumikia huinua nyumba zetu na makanisa hadi mahali patakatifu ambapo tunaweza kujifunza kuishi kimaagano.
Kwa mfano, agano letu la daima kumkumbuka Kristo hufanywa binafsi, lakini agano hili tunaliishi tunapowatumikia wengine. Miito hutuzunguka kwa fursa za “kubebeana … mizigo, na hivyo kutimiza sheria ya Kristo.” Tunapotumikia kwa sababu tunampenda Mungu na kutaka kuyaishi maagano yetu, huduma ambayo ilionekana kama wajibu na yenye kuchosha inakuwa ya furaha na ya kuleta mabadiliko.
Ibada hazituokoi kwa sababu zinatimiza orodha ya ukaguzi ya mbinguni. Hakika, tunapoishi maagano yaliyounganishwa na ibada hizi, tunakuwa aina ya mtu anayetaka kuwa katika uwepo wa Mungu. Uelewa huu hushinda kusitasita kutumikia au upendeleo wa kutokutumikia. Matayarisho yetu ya kukutana na Yesu Kristo huarakishwa tunapoacha kuuliza kile ambacho Mungu ataruhusu na kuanza kuuliza kile ambacho Mungu angependelea.
Tatu, kushiriki katika kazi ya Mungu hutusaidia kupokea zawadi ya Mungu ya neema na kuhisi upendo Wake mkuu.
Hatupokei fidia ya kifedha kwenye kutumikia. Badala yake, maandiko yanafundisha kwamba kwa ajili ya “taabu [yetu] tunapaswa kupokea neema ya Mungu, ili [sisi] tupate kuwa na nguvu katika Roho, [kuwa] na ujuzi wa Mungu, [na] kufundisha kwa nguvu na mamlaka kutoka kwa Mungu.” Hiyo ni biashara nzuri sana!
Kwa sababu ya neema ya Mungu, uwezo wetu au kutoweza kwetu sio kanuni ya msingi ya kutoa au kukubali wito. Mungu hatarajii utendaji mkamilifu au talanta ya kipekee ili kushiriki katika kazi Yake. Kama ingekuwa hivyo, Malkia Esta asingeliokoa taifa lake, Petro asingeongoza Kanisa la mwanzo, na Joseph Smith asingekuwa Nabii wa Urejesho.
Tunapotenda kwa imani kufanya jambo lililo nje ya uwezo wetu, udhaifu wetu unafichuliwa. Hili si jambo la kufurahisha kamwe, lakini ni muhimu kwa ajili yetu “kujua kwamba ni kwa neema [ya Mungu], … kwamba tuna uwezo wa kufanya mambo haya.”
Tutaanguka mara nyingi tunaposhiriki katika kazi ya Mungu. Lakini katika juhudi zetu Yesu Kristo hutushika mkono. Taratibu hutuinua ili kupata uzoefu wa ukombozi kutoka kushindwa na woga na kutoka kuhisi kama kamwe hatutaweza kutosha. Tunapoweka wakfu juhudi yetu ndogo lakini bora zaidi, Mungu huikuza. Tunapojitoa dhabihu kwa ajili ya Kristo, Yeye hututakasa. Hii ni nguvu ya mabadiliko ya neema ya Mungu. Tunapotumikia, tunakua katika neema hadi tutakapokuwa tayari “kuinuliwa na Baba, kusimama mbele ya [Yesu Kristo].”
Wasaidie Wengine Kupokea na Kufurahia Zawadi ya Miito
Sijui yote ambayo Mwokozi ataniuliza nitakaposimama mbele Yake, lakini labda swali moja litakuwa, “Ni nani uliyemleta pamoja nawe?” Wito ni zawadi takatifu kutoka kwa Baba wa Mbinguni mwenye upendo ili kusaidia kuleta wengine pamoja nasi kwa Kristo. Kwa hiyo ninawaalika viongozi na kila mmoja wetu kwa kukusudia zaidi kuwatafuta wale wasio na miito. Wahimize na uwasaidie kujishughulisha katika kazi ya Mungu ili kuwasaidia kujiandaa kwa ujio wa Kristo.
John hakuwa mhudhuriaji Kanisani wakati askofu wake alipomtembelea na kumwambia kwamba Bwana alikuwa na kazi kwa ajili yake ya kufanya. Alimwalika John aache kuvuta sigara. Ingawa John alikuwa amejaribu mara nyingi kuacha, wakati huu alihisi nguvu zisizoonekana zikimsaidia.
Wiki tatu tu baadaye, rais wa kigingi alimtembelea John. Alimwita kutumikia katika uaskofu. Johna alishtuka. Alimwambia rais wa kigingi kwamba alikuwa hivi karibuni ameacha kuvuta sigara. Ikiwa hii ilimaanisha kwamba angelazimika kuachana na utamaduni wake wa kuhudhuria michezo ya soka ya siku ya Jumapili, basi hilo lilikuwa ni jambo kubwa sana kuombwa. Jibu la rais wa kigingi lilikuwa rahisi: “John, si mimi nikuombaye; ni Bwana.”
Ambapo John alijibu, “Ikiwa ni hivyo, nitatumikia.”
John aliniambia dhabihu hizi za kutumikia zilikuwa sehemu za mabadiliko ya kiroho kwake na familia yake.
Ninajiuliza kama tuna upofu, na kushindwa kutoa miito kwa watu binafsi ambao, kwa mtazamo wetu wa maisha ya kibinadamu, wanaonekana kutowezekana au kutostahili. Au tunaweza kuhusika zaidi na utamaduni wa utendaji kuliko fundisho la kupiga hatua, tukipuuza kuona jinsi Mwokozi anavyoongeza uwezo kwa wale wanaoonekana kutowezekana na kutothibitishwa kwa kuwapa fursa za kutumikia.
Mzee David A. Bednar anafundisha umuhimu wa agizo la kimaandiko la “kumruhusu kila [mwanamke na] mwanamume wajifunze wajibu [wao], na kutenda.” Je, tunalifanya hili? Viongozi na wazazi wanapowaruhusu wengine kujifunza na kujitenda wao wenyewe, watu hao huchanua na kustawi. Wakati njia rahisi inaweza kuwa kuwapa waumini waaminifu wito wa pili, njia bora zaidi ni kuwaalika wasiotarajiwa kutumikia na kuwaruhusu wajifunze na kukua.
Kama Kristo angekuwa hapa kimwili, Angewatembelea wagonjwa, kufundisha darasa la Shule ya Jumapili, kuketi na msichana aliyevunjika moyo, na kuwabariki watoto. Anaweza kuifanya kazi Yake Mwenyewe. Lakini Yeye anaishi kanuni hii ya kutuacha tutende na tujifunze, hivyo Yeye anatutuma kwa niaba yake.
Pamoja na kushiriki katika kazi ya Mungu huja “haki, fursa na jukumu la kumwakilisha Bwana [Yesu Krosto].” Tunapotumikia ili kumuweka Kristo mbele na si nafsi zetu, huduma yetu huwa ya shangwe. Wakati wengine wanaondoka kwenye darasa letu, mkutano, ziara ya kuhudumu, au shughuli wakimkumbuka Kristo zaidi kuliko wanavyotukumbuka sisi, kazi hiyo inatia nguvu.
Katika kutafuta kwa dhati kumuwakilisha Mwokozi, tunakuwa zaidi kama Yeye. Hayo ni maandalizi bora zaidi kwa wakati mtakatifu ambapo kila mmoja wetu atapiga magoti na kukiri kwamba Yesu ndiye Kristo, ambapo ninashuhudia kwamba Yeye ndiye, na kwamba Rais Russell M. Nelson ni “sauti Yake … hata miisho ya dunia” ili kutusaidia “kujitayarisha … kwa yale yajayo.” Katika jina takatifu la Yesu Kristo, amina.