Mpango wa Rehema
Bwana ni mwenye rehema na mpango wa wokovu wa Baba yetu wa Mbinguni kwa kweli ni mpango wa rehema.
Mwaliko wa Nabii
Aprili iliyopita, mara baada ya habari njema kwamba Kanisa limepata Hekalu la Kirtland, Rais Russell M. Nelson alitualika kusoma sala ya kuwekwa wakfu kwa Hekalu la Kirtland, iliyoandikwa katika sehemu ya 109 ya Mafundisho na Maagano. Sala ya uwekaji wakfu, alisema Rais Nelson, “ni mafunzo kuhusu jinsi gani hekalu katika hali ya kiroho hututia nguvu wewe na mimi ili kukabiliana na changamoto za maisha kwenye siku hizi za mwisho.”
Nina uhakika kujifunza kwenu sehemu ya 109 kulitoa ufahamu uliowabariki. Jioni hii, ninashiriki mambo kadhaa niliyojifunza nilipofuata mwaliko wa nabii wetu. Njia ya kutoa amani ambayo kwayo utafiti wangu uliniongoza ilinikumbusha kwamba Bwana ni mwenye rehema na kwamba mpango wa wokovu wa Baba yetu wa Mbinguni kwa kweli ni mpango wa rehema.
Wamisionari Wapya Walioitwa Kuhudumu Hekaluni
Kama unavyoweza kufahamu, “wamisionari wapya walioitwa wanahimizwa kupokea endaumenti ya hekaluni haraka iwezekanavyo na kuhudhuria hekaluni mara nyingi kadiri hali zinavyoruhusu.” Mara baada ya kupatiwa endaumenti, wao pia “wanaweza kuhudumu kama wafanyakazi … wa hekaluni kabla hawajaanza huduma ya umisionari.”
Muda katika hekalu kabla ya kuingia katika chuo cha mafunzo ya wamisionari (MTC) unaweza kuwa baraka ya ajabu kwa mmisionari mpya kujifunza zaidi kuhusu maagano ya hekaluni kabla ya kushiriki baraka za maagano hayo na ulimwengu.
Lakini katika kusoma sehemu ya 109, nilijifunza kwamba hekaluni, Mungu anawawezesha wamisionari wapya—ndiyo, sisi sote—katika njia ya ziada, njia takatifu. Katika sala hiyo ya uwekaji wakfu, iliyotolewa kwa ufunuo, Nabii Joseph Smith aliomba kwamba “wakati watumishi wako watakapo waendea kutoka nyumbani kwako … kutoa ushuhuda wa jina lako,” “mioyo” ya “watu wote” ingeweza “kulainishwa”—wote “wakubwa wa dunia” na “maskini wote, wahitaji, na [wale] wanaoteseka.” Aliomba kwamba “chuki zao zipate kutoa njia mbele ya ukweli, na watu wako wapate kukubalika machoni pa wote; ili miisho yote ya dunia ipate kujua kwamba sisi, watumishi wako, tumeisikia sauti yako, na kwamba wewe umetutuma sisi.”
Hii ni ahadi nzuri kwa mmisionari mpya aliyeitwa—kuwa chuki “zipate kutoa njia mbele ya ukweli,” “kupata kukubalika machoni pa wote,” na kuifanya dunia ijue kuwa wametumwa na Bwana. Kila mmoja wetu anahitaji baraka sawa na hizo. Ni baraka iliyoje kuwa na mioyo iliyolainishwa tunapozungumza na majirani na wafanyakazi wenzetu. Sala ya kuweka wakfu haielezei hasa jinsi gani muda wetu hekaluni utakavyolainisha mioyo ya wengine, lakini ninashawishika kuwa inaungana na jinsi gani muda katika nyumba ya Bwana unavyolainisha mioyo yetu wenyewe kwa kutuweka sisi kwenye kiini cha Yesu Kristo na rehema Yake.
Bwana Anajibu Ombi la Joseph Smith kwa Rehema
Nilipokuwa nikisoma sala ya kuweka wakfu ya Kirtland, nilishangazwa pia kwamba Joseph tena na tena aliomba rehema—kwa ajili ya waumimi wa Kanisa, kwa maadui wa Kanisa, kwa viongozi wa nchi, kwa ajili ya mataifa ya dunia. Na, binafsi sana, alimsihi Bwana amkumbuke na kumhurumia mpendwa wake Emma na watoto wao.
Ni jinsi gani Joseph alipata kuhisi wakati, wiki moja baadaye, siku ya Pasaka, Aprili 3, 1836, katika Hekalu la Kirtland, Mwokozi alipomtokea yeye na Oliver Cowdery na, kama ilivyoandikwa katika sehemu ya 110 ya Mafundisho na Maagano, alisema, “Nimekubali nyumba hii, na jina langu litakuwa hapa; nami nitajidhihirisha kwa watu wangu kwa rehema katika nyumba hii.” Ahadi hii ya rehema lazima ilikuwa na maana maalumu kwa Joseph. Na kama Rais Nelson alivyofundisha Aprili iliyopita, ahadi hii pia inatumika kwa kila hekalu lililowekwa wakfu leo.”
Kupata Rehema katika Nyumba ya Bwana
Kuna njia nyingi ambazo kila mmoja wetu anaweza kupata rehema katika nyumba ya Bwana. Hii imekuwa kweli tangu kwa mara ya kwanza Bwana alipoiamuru Israeli kujenga hema na kuweka katikati yake “kiti cha rehema.” Hekaluni, tunapata rehema katika maagano tunayofanya. Maagano hayo, kama nyongeza ya agano la ubatizo, yanatufunga kwa Baba na Mwana na kutupatia ufikiaji wa kile ambacho Rais Nelson amefundisha kuwa ni “aina maalumu ya upendo na rehema … unaoitwa hesed” kwa Kiebrania.
Tunapata rehema katika fursa ya kuunganishwa na familia zetu milele. Katika Hekalu, pia tunakuja kuelewa kwa uwazi zaidi kwamba Uumbaji, Anguko, dhabihu ya Mwokozi ya kulipia dhambi, na uwezo wetu wa kuingia tena katika uwepo wa Baba yetu wa Mbinguni—hakika, kila sehemu ya mpango wa wokovu—ni madhihirisho ya rehema. Inaweza kusemwa kwamba mpango wa wokovu ni mpango wa furaha hasa kwa sababu ni “mpango wa rehema.”
Kutafuta Msamaha Kunafungua Mlango kwa Roho Mtakatifu
Ninashukuru kwa ahadi nzuri katika sehemu ya 110 kwamba Bwana atajidhihirisha Mwenyewe kwa rehema katika mahekalu Yake. Pia nina shukrani kwa kile inachofunua kuhusu jinsi Bwana atakavyojidhihirisha Mwenyewe kwa rehema wakati wowote ambapo sisi, kama vile Joseph, tunapoomba kwa ajili ya rehema.
Ombi la Joseph Smith la rehema katika sehemu ya 109 halikuwa mara ya kwanza kwa maombi yake ya rehema kusababisha ufunuo. Katika Kijisitu Kitakatifu, kijana Joseph aliomba siyo tu kujua ni Kanisa gani lilikuwa la kweli, lakini pia alisema kwamba “alimlilia Bwana kwa rehema, kwa maana hakukuwa na mtu mwingine ambaye ningeweza kumwendea ili kupata rehema.” Kwa namna fulani, kutambua kwake kwamba alihitaji rehema ambayo ni Bwana pekee ndiye angeweza kuitoa kulisaidia kufunguka kwa madirisha ya mbinguni. Miaka mitatu baadaye malaika Moroni alionekana kufuatia kile ambacho Joseph alikuwa amesema kilikuwa “sala na dua yake kwa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya msamaha wa dhambi zangu zote na upumbavu.”
Mpangilio huu wa ufunuo kufuatia ombi la rehema ni wa kawaida katika maandiko. Enoshi alisikia sauti ya Bwana baada tu ya kuomba kwa ajili ya kupata msamaha. Uongofu wa baba wa Mfalme Lamoni, unaanza kwa sala yake, “Nitaacha dhambi zangu zote ili nikujue wewe.” Huenda tusibarikiwe kwa uzoefu huu wa kushangaza, lakini kwa wale ambao wakati mwingine wanahangaika kuhisi majibu ya sala, kutafuta rehema za Bwana ni moja ya njia zenye nguvu zaidi za kuhisi ushahidi wa Roho Mtakatifu.
Kutafakari Rehema za Mungu Kunafungua Mlango wa Ushuhuda wa Kitabu cha Mormoni
Kanuni kama hiyo inafundishwa vizuri katika Moroni 1:3–5. Mara nyingi tunafupisha mistari hii kufundisha kwamba, kupitia sala ya dhati, tunaweza kujua kama Kitabu cha Mormoni ni cha kweli. Lakini ufupisho huu unaweza kupuuza jukumu muhimu la rehema. Sikiliza jinsi Moroni anavyoanza mawaidha yake: “Ningewasihi kwamba wakati mtakaposoma mambo haya, … kwamba mngekumbuka jinsi vile Bwana amekuwa na huruma kwa watoto wa watu, kutokea kuumbwa kwa Adamu hadi chini mpaka wakati ambapo mtapokea vitu hivi, na kuvitafakari katika mioyo yenu.”
Moroni anatuhimiza sio tu kusoma mambo haya—kumbukumbu ambazo alikuwa karibu kuzifunga—lakini pia kutafakari mioyoni mwetu kile ambacho Kitabu cha Mormoni kinafunua kuhusu “jinsi Bwana alivyokuwa na huruma kwa watoto wa watu.” Ni kutafakari juu ya rehema za Bwana ambazo zinatuandaa “kumuuliza Mungu, Baba wa Milele, katika jina la Kristo, ikiwa vitu hivi si vya kweli.”
Tunapotafakari juu ya Kitabu cha Mormoni, tunaweza kuuliza: Je, ni cha kweli, kama Alma alivyofundisha, kwamba mpango wa Mungu wa rehema unahakikisha kwamba kila mtu aliyewahi kuishi hapa duniani atafufuliwa na kwamba “watarejeshwa kwa … sura kamili”? Je, Amuleki yuko sahihi—je, rehema ya Mwokozi inaweza kukidhi mahitaji yote ya kweli ya haki ambayo tungelazimika kulipa na badala yake “[kutuzingira] katika mikono ya usalama”?
Je, ni kweli, kama Alma alivyoshuhudia, kwamba Kristo aliteseka si tu kwa ajili ya dhambi zetu bali kwa ajili ya “maumivu na mateso” ili kwamba aweze “kujua … jinsi ya kuwasasidia watu wake kulingana na unyonge wao”? je, Bwana kweli ni mwenye rehema, kama Mfalme Benyamini alivyofundisha, kwamba kama zawadi ya bure, alitoa dhabihu ya kulipia dhambi “za wale … ambao wamekufa bila kujua mapenzi ya Mungu juu yao, au ambao wametenda dhambi kwa ujinga”?
Je, ni kweli, kama Lehi alivyosema, kwamba “Adamu alianguka ili wanadamu wawe; na wanadamu wapo, ili wapate shangwe”? Na je, ni kweli, kama Abinadi alivyoshuhudia, akimnukuu Isaya, kwamba Yesu Kristo “alijeruhiwa kwa ajili ya makosa yetu, alichubuliwa kwa ajili ya maovu yetu; adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake; na kwa kupigwa kwake sisi tumepona”?
Kwa jumla, je, mpango wa Baba kama ulivyofundishwa katika Kitabu cha Mormoni kweli ni wa rehema? Ninashuhudia kwamba ni wa rehema na kwamba mafundisho ya amani na tumaini la rehema katika Kitabu cha Mormoni ni ya kweli.
Bado, nadhani kwamba inawezekana wengine wanapambana, licha ya kusoma kwa uaminifu na sala zako, kutambua ahadi ya Moroni kwamba Baba wa Mbinguni “atadhihirisha ukweli kwako, kwa nguvu ya Roho Mtakatifu.” Najua mahangaiko haya kwa sababu niliyahisi, miaka mingi iliyopita, wakati usomaji wangu wa kwanza wa Kitabu cha Mormoni haukutoa jibu la haraka na la wazi kwa sala zangu.
Ikiwa unapambana, naomba nikualike ufuate ushauri wa Moroni ili kutafakari juu ya njia nyingi ambazo Kitabu cha Mormoni kinafundisha “jinsi Bwana alivyokuwa na huruma [kwa] watoto wa watu”? Kulingana na uzoefu wangu, natumaini kwamba, unapofanya hivyo, amani ya Roho Mtakatifu inaweza kuingia moyoni mwako na unaweza kujua, kuamini, na kuhisi kwamba Kitabu cha Mormoni na mpango wa rehema unaofundishwa ni vya kweli.
Ninatoa shukrani zangu kwa mpango mkuu wa rehema wa Baba na kwa utayari wa Mwokozi kuutekeleza. Ninajua kwamba atajidhihirisha Mwenyewe kwa rehema katika hekalu Lake takatifu na katika kila sehemu ya maisha yetu ikiwa tutamtafuta. Katika jina la Yesu Kristo, amina.