“Fuata Maneno ya Furaha,” Rafiki, Mei 2025, 44–45.
Kisomaji Rahisi
Fuata Maneno ya Furaha
Hadithi ya kweli kutoka Marekani.
“Je, tunaweza kwenda kuchora kwa chaki?” Quinn alimuuliza Mama.
“Hakika!” Mama alisema. “Twende.”
Quinn na kaka yake mdogo na dada yake walikimbia nje.
“Nataka bluu!” Quinn alisema kwa sauti.
Kade na Chloe walichukua chaki pia. Waliketi chini na kuanza kuchora kwenye njia ya kutembea kwa miguu. Mama aliokota baadhi ya chaki nyekundu na kuanza kuandika.
“Unafanya nini?” Quinn aliuliza.
“Ninaandika maneno ya furaha kwa ajili ya watoto wa shule wanapotembea kwenda nyumbani leo,” Mama alisema.
Quinn aliweza kuiona shule kutoka dirisha lake la mbele. Alipenda kuwapungia mkono watoto walipokuwa wakipita.
“Ni jumbe gani tunaweza kuandika kuwafanya watabasamu?” Mama aliuliza.
Quinn alisoma juu ya bega la Mama. “Wewe ni …”
“Wa kupendeza!” Mama akamaliza.
Quinn alitabasamu na kuendelea kusoma. “Unavutia. Unaweza!”
Kisha Quinn akapata wazo. Alianza kuchora mstari mrefu kwenye mojawapo ya jumbe za Mama. Alichora mstari kwenye ule uliofuata. Kisha akaunga na mwingine.
“Unafanya nini?” Mama aliuliza.
“Ninatengeneza mstari kwa ajili ya watoto kutembelea,” Quinn alisema. Alianza kukimbia juu ya mstari. “Unaona? Ninawaonyesha wapi pa kupata maneno yote ya furaha.”
“Nadhani hiyo ni njia nzuri ya kumfanya kila mtu atabasamu,” Mama alisema. Na hiyo ilimfanya Quinn kutabasamu hata zaidi.
Vielelezo na Asya Aizenstein