“Kumsikia Roho Mtakatifu,” Rafiki, Machi 2025, 40.
Kumsikia Roho Mtakatifu
“Bahatisha kile nilichojifunza katika Darasa la Watoto,” Chim alisema.
Hadithi ya kweli kutoka Ufilipino.
Chim alifungua macho yake yenye usingizi. Hatimaye ilikuwa mwishoni mwa wiki!
“Muda wa kuamka, au tutachelewa,” Mama aliita.
Chim alitamani angeweza kulala kwa muda mrefu zaidi, lakini leo ilikuwa siku ya soko. Alihitaji kumsaidia Mama kununua chakula kwa ajili ya wiki. Kwa hiyo aliamka na kwa haraka akala kifungua kinywa chake.
Mama alifanya mengi kwa ajili ya Chim na kaka zake wawili. Alikuwa na shughuli nyingi sana, na hakuwa na muda mwingi wa kuwa nyumbani. Chim na kaka zake walifanya kazi pamoja kufanya kazi nyingi za nyumbani. Chim alikuwa na furaha kusaidia.
Wakati Chim na Mama waliporudi kutoka sokoni, Mama alilazimika kuondoka kwenda kazini. Alipokuwa ameondoka, Chim na kaka zake walijiandaa kwa ajili ya Jumapili. Chim aliweka viatu, suruali na shati ambavyo angevaa kanisani kesho yake. Kaka yake mkubwa, Robin, alimsaidia kupiga pasi shati lake. Kisha wakatengeneza chakula cha jioni.
Chim alikuwa akisafisha jikoni wakati Mama aliporudi nyumbani. Mama alionekana amechoka kweli.
“Chukua, Mama.” Chim alimkabidhi bakuli la chakula cha moto ili ale.
Mama alitabasamu. “Asante kwa msaada wako leo. Hiki kinaonekana kitamu!”
Asubuhi iliyofuata, Chim aliamka mapema na kujiandaa kwa ajili ya kwenda kanisani. Alikuwa na shauku ya kuwaona rafiki zake katika Darasa la Watoto na kujifunza kuhusu Yesu Kristo.
“Mama?” aliita kimya kimya, akigonga mlango wake. “Je, unaenda pamoja nasi kanisani leo?”
“Siwezi,” Mama alisema. “Inabidi nifanye kazi mchana huu.”
“SAWA.” Chim alihisi huzuni kidogo. Ilikuwa karibu mwaka mmoja tangu Mama alipoenda kanisani pamoja nao. “Uwe na safari pamoja na siku nzuri,” chim alimwambia mama.
“Tayari kuondoka?” kaka yake mdogo, Mattew, aliuliza.
“Ndiyo!” Chim alivaa viatu vyake na kukimbia nje ya mlango na kaka zake kuwahi basi.
Chim alihisi furaha alipoingia katika jengo la kanisa. Alijaribu kufikiria juu ya Yesu Kristo wakati wa sakramenti. Na katika Darasa la Watoto, alijaribu sana kusikiliza somo la Dada Ortega.
“Leo tunajifunza kuhusu Roho Mtakatifu,” alisema Dada Ortega. “Roho Mtakatifu anatuletea jumbe kutoka kwa Baba wa Mbinguni. Kama vile redio.”
Chim alitazama picha ya redio ambayo Dada Ortega aliyokuwa ameinyanyua juu.
“Redio inafanya kazi kwa kupokea ishara na kuigeuza kuwa mawimbi ya sauti tunayoweza kusikia,” alieleza. “Lazima uiweke kwenye idhaa sahihi ili kuisikia. Ili kumsikia Roho Mtakatifu, tunahitaji kuweka mioyo na akili zetu kwenye njia sahihi pia. Je, tunawezaje kufanya hilo?”
Kila mmoja alikuwa anafikiria. Kisha Chim akasema, “Kwa kumfuata Yesu Kristo na kushika amri.”
Dada Ortega alitabasamu. “Hiyo ni sawa.”
Baada ya kanisani, Chim alisaidia kutengeneza chakula cha jioni tena. Alihisi vizuri ndani alipokuwa akisaidia. Alijua kwamba kwa kuihudumia familia yake, alikuwa akiweka moyo wake kwenye njia sahihi ya kumhisi Roho Mtakatifu.
Wakati Mama alipofika nyumbani, Chim alimpa kumbatio kubwa. Kisha wakasali juu ya chakula na wakaanza kula.
“Bahatisha kile nilichojifunza kanisani leo,” Chim alisema. Alipenda kumwambia Mama kuhusu Darasa la Watoto.
“Nini?” Mama aliuliza.
“Tulijifunza kuhusu Roho Mtakatifu,” alisema Chim. “Ni kama redio. Tunapotii amri, tunaweza kuigeuza mioyo yetu iwe kwenye njia sahihi ya kumsikiliza Yeye.”
Mama alikubali kwa kichwa. “Hiyo ni vizuri sana. Kwa hiyo ni mfano ulioje wa kutii amri?”
Chim alitabasamu. “Msaidie mama yako!” Chim alicheka. “Nakupenda, Mama.”
Vielelezo na Uran Duo