“Kuhisi Huzuni,” Rafiki, Machi 2025, 36–37.
Kuhisi Huzuni
Kwa nini siwezi kuwa na furaha kama kila mtu mwingine?
Hadithi ya kweli kutoka Marekani.
Savannah alivuta mablanketi juu ya kichwa chake. Leo ilikuwa siku mbaya kweli.
Wakati wa shule leo, Savannah hakuweza kufokasi kwenye chochote. Alikuwa amehisi kuchoka, kufadhaika, na mwenye huzuni. Kulikuwa na uzito mkubwa tumboni mwake ambao haungetoweka. Kufikia mwisho wa siku, yote aliyotaka kufanya ilikuwa kutambaa chini ya dawati lake na kujificha.
Hivi karibuni, Savannah alihisi huzuni karibu wakati wote. Rafiki zake walikuwa wamejaribu kumchangamsha, lakini wakati mwingine Savannah hakutaka kuwa pamoja nao. Daima walionekana kuwa na furaha sana. Wakati mwingine alifikiri wangekuwa na furaha zaidi bila yeye.
Ni nini kibaya kwangu? Savannah alijiuliza. Kwa nini siwezi kuwa na furaha kama kila mtu mwingine?
Alihisi baridi na upweke kama mawingu ya kijivu nje. Na sasa alitaka tu kulala.
Savannah alisikia mlango wake wa chumba cha kulala ukifunguliwa.
“Savannah,” Mama alisema, akikaa pembeni mwa kitanda, “nini kibaya?”
“Hakuna kitu,” Savannah alisema. “Nimechoka tu.”
“Una hakika? Mama aliuliza. “Nina wasiwasi kukuhusu wewe.”
“Niko SAWA,” Savannah alisema.
“Sawa.” Mama alisimama. “Kumbuka tu kwamba unaweza kuzungumza nami kuhusu chochote. Ninakupenda.”
Savannah alikaa kitandani hadi muda wa chakula cha jioni. Usiku ule, hakuweza kulala. Ubongo wake haungeacha kufikiria kuhusu kila kitu.
Siku iliyofuata bado alihisi kuchoka sana. Ilikuwa siku nyingine ndefu. Savannah alifika nyumbani kutoka shuleni na kukaa mezani jikoni. Alivuta pumzi na kuangalia nje ya dirisha. Theluji ilikuwa inaanguka tena.
“Savannah?”
Savannah aligeuka na kushangaa kumwona Bibi akija chumbani.
“Habari, Bibi,” Savannah alisema. “Ni kitu gani unafanya hapa?”
Bibi aliketi chini. “Mama yako alinitaka nije,” alisema. “Ana wasiwasi juu yako.”
“Nimechoka sana kweli. Mimi niko sawa, tu,” Savannah alisema.
Bibi alitabasamu kwa upole. “Je, niliwahi kukuambia kuhusu majira ya joto mimi na Babu yako tulipohama?”
“Sidhani,” Savannah alisema.
“Nilihuzunika wakati wote,” Bibi alisema. “Nilitaka kuwa na furaha, lakini sikujali kuhusu chochote. Nilihisi kuwa mpweke.”
“Lakini ulikuwa na Babu na mama yangu.” Savannah alitazama chini kwenye viatu vyake. “Kwa nini uhisi mpweke?”
“Sikuweza kujua kilichokuwa kinatendeka,” Bibi alisema. “Kamwe sikuwahi kuhisi hivyo hapo awali. Hatimaye nilienda kwa daktari.”
“Nini kilitokea?”
Bibi alimkumbatia kwa mikono. “Niligundua kuwa nina msongo wa mawazo.”
“Ee, kwa hivyo ulihisi huzuni tu?” Savannah aliuliza.
“Hapana, msongo wa mawazo ni zaidi ya kuhisi huzuni tu,” Bibi alieleza. “Huzuni yangu haikuonekana kuisha. Nilihangaika kufanya mambo yote ambayo kwa kawaida nilifanya. Na nilikuwa na wakati mgumu kuunganika na watu wengine, hata familia yangu mwenyewe. Hakika nilihitaji msaada.
Savannah alitazama juu. “Ni aina gani ya msaada?
“Daktari alielezea tatizo lilikuwa nini, na tulifanya mpango pamoja ili kunisaidia kujihisi vizuri zaidi,” Bibi alisema. “Lakini wakati mwingine bado nilihisi huzuni. Nilitumia muda mwingi nikisali. Nilipokuwa mpweke, nilimfikiria Mwokozi akiwa ameketi kando yangu. Nilihisi vyema kufikiria kumhusu Yeye.”
Savannah aliangalia theluji nje na kutetemeka. “Ninahisi huzuni sana pia. Ninajaribu kuhisi furaha, lakini wakati mwingine siwezi tu, na kisha ninajikasirikia mwenyewe kwa kuhisi hivyo.”
“Ninajua, kipenzi.” Bibi alimpa Savanna kumbatio. “Hivyo ndivyo ninavyohisi wakati mwingine pia. Lakini hauko peke yako. Ninakupenda, wazazi wako wanakupenda, na Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo wanakupenda. Wanaelewa maumivu yako na kamwe hawatakuacha.”
Labda Bibi yuko sahihi, Savannah aliwaza. Mimi siko peke yangu. Uzito katika tumbo la Savannah haukuwa mzito.
“Nadhani ninapaswa kuzungumza na Mama,” Savannah alisema. “Anataka kunisaidia pia.”
“Hilo ni wazo zuri sana.” Bibi aliushika mkono wa Savannah.
Savannah alitabasamu na kuegemea bega la Bibi. Hakuhisi baridi sana wala mpweke tena.
Vielelezo na Marina Pessarrodona