2025
Hadithi Yangu ya Uongofu
Januari 2025


Kurasa za Karibu

Hadithi Yangu ya Uongofu

Jina langu ni Annie B. Biwole na ninaishi Douala, Cameroon.

Nimekuwa muumini wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho tangu Mei 8, 2010. Nilikulia katika familia iliyopenda Ukatoliki.

Kadiri ninavyoweza kukumbuka, wazazi wangu wangetuamsha kila mapambazuko ya asubuhi kwa ajili ya sala ya familia, kisha tungefanya tena jambo hilohilo wakati wa jioni kabla ya kwenda kulala. Kila jumapili tulikwenda kwenye misa.

Lakini mara tu nilipofikia umri wa utu uzima, sikwenda kanisani tena kwa sababu sikuelewa chochote.

Miongo kadhaa baadaye, nilipokuwa kwenye miaka ya hamsini, nikiwa naishi nje ya nchi yangu nilianza kuhisi ukosefu mkubwa wa mambo ya kiroho ndani yangu, lakini sikujua kipi cha kufanya au wapi pa kutazama.

Kwa kuwa nilikuwa Mkatoliki na nilikuwa nikiishi kwenye nchi yenye Ukatoliki mwingi (Ufaransa), niliamua kuchagua kanisa ambapo ningeenda kila Jumamosi ili kuabudu.

Kanisa la kupendeza nililolipata mara nyingi lilikuwa tupu, likiwa na wanawake wachache wazee wakiwa wamepiga magoti katika sala, na kila baada ya muda wakinyanyuka ili kuwasha moja ya mishumaa iliyowekwa juu ya meza upande wa nyuma wa chumba.

Na niliwaiga kwa sababu sikujua kingine chochote cha kufanya.

Nilifanya hivi kwa takribani miezi saba mpaka dada yangu, ambaye pia alikuwa akitafuta ukweli, alibadilisha makanisa na kunishawishi niwe Mpentekoste kama yeye.

Kutoka wakati huo na kuendelea nilianza kusoma Biblia, bila kuelewa mengi kuhusu Biblia.

Lakini faida ilikuwa ni kwamba nilianza kutii amri na kufanyia kazi mafundisho niliyoyapokea.

Bado, nilihisi kana kwamba kuna kitu kilikosekana.

Usiku mmoja nilipata ndoto ambapo mtu katika ndoto aliniambia: “BARAKA KWA AJILI YAKO NA FAMILIA YAKO ZINAWEZA KUPATIKANA KATIKA NCHI YAKO ULIPOZALIWA.”

Sikuelewa hili lilimaanisha nini, lakini kwa sababu ya matatizo ya kiafya ya mwanangu, ilinibidi niondoke nchi ya kigeni nilimokuwa nikiishi ili kurejea nyumbani Cameroon kumsaidia mwanangu mgonjwa.

Nilipowasili Cameroon mnamo Septemba 2009 baada ya miaka 30 ya kutokuwepo kwangu, nilienda kutoka kanisa la Pentekoste hadi lingine, lakini bado nilikuwa na hisia zilezile ndani yangu kwamba kuna kitu kilikosekana.

Mara nyingi niliwaona vijana wakipita, wakiwa wamevalia shati jeupe na tai, wawili wawili. Nilidhani walikuwa Mashahidi ya Yehova.

Na, kwa kuwa nilikuwa nikitafuta ukweli na sikujua wapi pa kuupata, kwa nini nisiwajaribu wao? Nilijiambia mwenyewe.

Wakati nikiwauliza maswali, walijitambulisha kama wamisionari wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho.

Baada ya masomo mawili, walinialika nihudhurie mkutano wa sakramenti, na kimuujiza, hatimaye nilihisi amani ya nafsi. Hatimaye nilihisi niko nyumbani kwa sababu nilikuwa nimeupata ukweli niliokuwa nikiutafuta.

Miaka saba baadaye, nilipoenda hekaluni, hatimaye nilielewa maana ya ndoto niliyopata, kwa sababu nilifanya ibada kwa ajili ya watu wengi katika familia yangu.

Ninashuhudia kwamba Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho ndilo Kanisa la kweli pekee lililorejeshwa juu ya uso wa dunia.

Ninashuhudia juu ya hili katika jina la Yesu Kristo. Amina.