“Mazungumzo na Gabby kuhusu Kuhudumu Kanisani,” Rafiki, Septemba 2025, 40–41.
Mazungumzo na Gabby kuhusu Kuhudumu Kanisani
Gabby ni mwenye umri wa miaka 11 kutoka Harare, Zimbabwe. Tulimuuliza baadhi ya maswali kuhusu kuongoza muziki kanisani.
Tuambie kuhusu wewe mwenyewe.
Ninapenda kupika vitinda mlo na vyakula vitamu na kucheza marimba. Ninaimba na kucheza ngoma, na ninajifunza kucheza filimbi, marimba na piano.
Tuambie kuhusu kazi yako mpya.
Askofu aliniomba nisaidie kuongoza muziki katika mkutano wa sakramenti. Sikutarajia hilo na nilifikiri wangemchagua mtu mkubwa. Lakini pia nilihisi kupendwa na kuwa na furaha kwa sababu ninapenda muziki.
Wakati mwingine bado ninaogopa kwamba nitaimba kitu kisicho sahihi na kwamba watu watakisikia. Lakini Roho Mtakatifu hunisaidia kuwa na faraja mbele ya kila mtu. Sasa kwa kuwa ninazoea, kwa kweli ni furaha sana!
Ilikuwaje kuongoza muziki kwa ajili ya mawasilisho ya watoto kwenye mkutano wa sakramenti?
Mara ya kwanza ilikuwa inatisha. Tulipokuwa tukifanya mazoezi, wakati mwingine nilisahau baadhi ya maneno. Hivyo nilifanya mazoezi ya kuimba na mama yangu nyumbani, na hiyo ilisaidia sana. Tulipofanya mazoezi katika Darasa la Watoto, niliimba kwa sauti ili kuwasaidia wale ambao hawawezi kusoma au hawakujua maneno.
Nilihisi furaha wakati siku ya onyesho ilipofika. Kila kitu kilienda vizuri. Nilihisi amani na utulivu, na maneno yalinijia tu.
Je, ulijifunza nini kutokana na uzoefu huu?
Nilijifunza kwamba wakati mwingine mambo hayaendi kikamilifu, lakini ni SAWA na unaweza kujifunza kutoka kwayo. Kuongoza muziki katika Darasa la Watoto pia kuliniandaa kwa kazi yangu mpya!
Ni ushauri gani ungewaambia wengine kuhusu kuhudumu kanisani?
Wakati mwingine inaweza kuwa vigumu kuhudumu mbele ya watu wengi, lakini jambo kuhusu sisi watoto ni kwamba tunaweza kuongoza bila kujali umri wetu au jinsi tulivyo wafupi au warefu. Ningewaambia kwamba hata ingawa wakati mwingine woga wetu unaweza kutushusha chini, Roho Mtakatifu anaweza kutusaidia kujihisi wenye amani. Yeye mara zote atatusaidia tusimame tena.