Kitabu cha Mormoni—Hazina Isiyopimika Katika Safari Yetu
Tunaposherehekea maneno ya Kristo yanayopatikana katika Kitabu cha Mormoni, Roho atatusaidia kuelewa kweli za milele.
Je, unaweza kushiriki wakati mtu alikupatia zawadi ambayo ilibadilisha maisha yako? Oktoba hii inatimia miaka 40 tangu nilipopokea moja ya zawadi kuu maishani mwangu. Nilipokuwa katika shule ya upili, nilitambua kwamba mwanafunzi mwenzetu alikuwa na nuru ambayo ilikuwa tofauti na vijana wengine wengi. Nilifurahia kuwa karibu naye. Siku moja aliniambia mimi alikuwa ni muumini wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho. Kisha akanipa zawadi ya nakala ya Kitabu cha Mormoni. Na alinialika nisome kurasa chache kisha nikutane na marafiki wawili ambao wangeweza kujibu maswali. Marafiki hao walikuwa wamisionari.
Nilipokutana na wamisionari, walinifundisha mafundisho ya Kristo na kunialika kufuata mwaliko wa nabii Moroni: “Na mtakapopokea vitu hivi, ningewashauri kwamba mngemwuliza Mungu, Baba wa Milele, katika jina la Kristo, ikiwa vitu hivi si vya kweli; na ikiwa mtauliza na moyo wa kweli, na kusudi halisi, mkiwa na imani katika Kristo, atawaonyesha ukweli wake kwenu kwa uwezo wa Roho Mtakatifu.” (Moroni 10:4).
Nilisoma kurasa kadhaa za Kitabu cha Mormoni na nikasali. Ingawa bado sikuwa na ufahamu wa kina wa mambo yote ambayo wamisionari walikuwa wakinifundisha, nilihisi moyoni mwangu kwamba nilichokuwa nikisoma kilikuwa kizuri na kilitoka kwa Mungu. Nilipokea uthibitisho wa ahadi ya Moroni: “Na kwa uwezo wa Roho Mtakatifu mpate kujua ukweli wa vitu vyote” (Moroni 10:5).
Baada ya mimi kubatizwa katika Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho, baadhi ya marafiki kutoka shuleni walijaribu kunishawishi kwamba nilikuwa nimefanya uamuzi mbaya. Kila wakati nilipokabiliwa na mashaka au upinzani kama huo, nilipokea uthibitisho mpya kupitia kujifunza maandiko na kusali ili kubaki mwaminifu kwa maagano ambayo nilikuwa nimeingia na Mungu. Tangu wakati huo, Kitabu cha Mormoni kimekuwa mwenza wangu na kimekuwa hazina isiyopimika katika safari yangu hapa duniani.
Kitabu cha Mormoni ni zaidi ya kitabu tu. Ni ushuhuda mwingine wa Yesu Kristo, ulioandikwa na manabii wengi wa kale kupitia roho ya unabii na ufunuo.
Tukio muhimu zaidi lililorekodiwa katika Kitabu cha Mormoni ni huduma binafsi ya Bwana Yesu Kristo miongoni mwa Wanefi muda mfupi baada ya Ufufuko Wake. Kitabu cha Mormoni “Kinaeleza mafundisho ya injili, kinafafanua juu ya mpango wa wokovu, na kuwaambia binadamu mambo wanayolazimika kuyafanya ili wapate amani katika maisha haya na wokovu wa milele katika maisha yanayokuja” (utangulizi wa Kitabu cha Mormoni).
Toleo la kwanza la Kitabu cha Mormoni: Ushuhuda Mwingine wa Yesu Kristo lilichapishwa katika mji mdogo katika jimbo la New York mnamo Machi 1830. Nabii Joseph Smith alikuwa na umri wa miaka 23 alipomaliza kutafsiri kitabu hiki mwaka 1829. Alitafsiri karibu kitabu kizima kwa muda usiozidi siku 75, na mchakato wa kukichapisha ulichukua takribani miezi saba.
Leo, takribani wamisionari 80,000 katika zaidi ya nchi 150 wanahudumu kama watu wa kujitolea, wakijitolea maisha yao kwa kutoa ushuhuda kwamba Kitabu cha Mormoni ni cha kweli na kwamba kinashuhudia juu ya Yesu Kristo.
Katika semina ya hivi majuzi ya viongozi wapya wa misheni mwezi Juni mwaka huu, nabii wetu mpendwa, Rais Russell M. Nelson, alishiriki ushuhuda wake wenye nguvu juu ya Kitabu cha Mormoni: “Kitabu cha Mormoni ni … neno la Mungu. Kinafundisha mafundisho ya Kristo na kuelezea zaidi kuhusu Upatanisho wa Mwokozi kuliko kitabu kingine chochote.”
Ningependa kutoa mapendekezo matatu ambayo yanaweza kusaidia kuimarisha uongofu wetu kwa Yesu Kristo kupitia kujifunza Kitabu cha Mormoni:
1. Kuwa na Bidii na Thabiti katika Kujifunza Kwako Kila Siku.
Kama Alma na wana wa Mosia, ni lazima “[tuyapekue] maandiko kwa bidii, ili [sisi] tujue neno la Mungu” na kuimarishwa katika ukweli.(Alma 17:2).
Tulipokuwa tukihudumu kama viongozi katika Misioni ya Georgia Atlanta, tulimhimiza kila mmisionari kujifunza Kitabu cha Mormoni angalau dakika 30 kila siku. Dhamira hiyo iliongeza imani yetu na kutusaidia sisi kutarajia miujiza.
Inawezekana kwamba baada ya misioni tunaweza kukosa muda wa kujifunza maandiko kila siku, lakini ninaahidi kwamba ikiwa utatanguliza kwa dhati kusoma Kitabu cha Mormoni kwa maombi kila siku, utapata nguvu kubwa zaidi za kiroho na imani katika Bwana na ahadi Zake.
2. Fanya Kujifunza Kwako kuwa na Maana Zaidi kwa Kusherehekea Maneno ya Kristo.
Nefi alitualika: “Shiriki maneno ya Kristo; kwani tazama maneno ya Kristo yatawaelezea vitu vyote mnavyostahili kutenda” (2 Nefi 32:3).
Kusherehekea humaanisha zaidi ya kusoma—humaanisha kufurahia ladha, kutafakari, na kutumia. Unapojifunza Kitabu cha Mormoni, fikiria njia za kufanya kujifunza kwako maandiko kuwa na maana zaidi. Kwa mfano:
-
Kutumia misaada ya kujifunza inayopatikana kwenye aplikesheni ya Gospel Library.
-
Bainisha kweli za milele ambazo hutusaidia kuelewa mpango wa Mungu na kutuongoza kufanya na kushika maagano na Baba yetu wa Mbinguni.
-
Angazia misemo muhimu na andika maoni yako ili kuhifadhi yale ambayo umejifunza wakati wa kujifunza kwako.
Kitabu cha Mormoni kina uwezo wa kujibu maswali ya nafsi. Kama Nefi alivyosema, tunapaswa “kulinganisha maandiko yote na sisi, ili yaweze kuwa kwa ajili ya manufaa yetu na kujifunza” (1 Nefi 19:23).
Tunaposherehekea maneno ya Kristo, yatakufungulia mlango wa ufunuo na kutuonyesha kile tunachohitaji kufanya katika hali mbalimbali za maisha yetu ili kumkaribia Yeye zaidi.
3. Toa Ushuhuda Wako juu ya Ukweli wa Kitabu cha Mormoni.
Kama vile Lehi alivyotamani kushiriki tunda la mti wa uzima na familia yake (ona 1 Nefi 8:12), tunapopata ushuhuda juu ya Kitabu cha Mormoni, tunakuza hamu ya kushiriki furaha inayotokana na kujua injili ya Yesu Kristo.
Mmoja wa wamisionari wetu wanne, Dada Benson, alishiriki nami hamu yake ya kumsaidia kaka yake. Wakati huo, kaka yake alikuwa akijiandaa kuhudhuria chuo kikuu, na hakuwa na uhakika wa kutumikia misheni. Nilihisi kuvutiwa kumwalika Dada Benson kusoma Kitabu cha Mormoni katika muda wa miezi minne ya kwanza ya misioni yake, akiweka alama kwenye vifungu anavyopenda zaidi, na kisha kutuma nakala hiyo kwa kaka yake.
Dada Benson alituma nakala hiyo iliyotiwa alama ya Kitabu cha Mormoni na akamwalika kaka yake kukisoma kila usiku. Baadaye alishiriki nami: “Kabla ya misioni yangu, kaka yangu hakuwa na uhakika kama alitaka kuhudumu misheni. Polepole, baada ya muda, kadiri alivyokuwa akisoma Kitabu cha Mormoni, aligundua shangwe inayoongezeka katika maisha yake na akaanza kufikiria kuhudumu misioni.”
Wiki mbili kabla ya Dada Benson kumaliza misioni yake kaka yake alipokea wito wake wa kuhudumu kama mmisionari. Sasa anahudumu katika Misioni ya Mexico Tuxtla Gutiérrez. Kupitia Kitabu cha Mormoni, Mzee Benson alikuja kuona maisha yake katika uwazi wa kiroho, kitu kilichomwongoza kufanya uamuzi wa kumtumikia Bwana na kuamini kwamba mambo yangefanyika vyema. Uamuzi huu ulikuwa muujiza—ulioshawishiwa na nguvu ya maneno ya Kristo.
Akina kaka na akina dada zangu wapendwa, ninamhimiza kila mmoja wenu kuzidisha kina cha kujifunza Kitabu cha Mormoni. Ninajua tunaposherehekea maneno ya Kristo yanayopatikana katika Kitabu cha Mormoni, Roho atatusaidia kuelewa kweli za milele na kushiriki shuhuda zetu kwa usadikisho kwa wale ambao Bwana amewatayarisha kusikia ujumbe Wake. Bwana alisema, “Wateule wangu huisikia sauti yangu na wala hawaishupazi mioyo yao” (Mafundisho na Maagano 29:7). Ninashuhudia kwamba wale wanaomwomba Mungu kwa imani watapata ushuhuda juu ya ukweli na utakatifu wa Kitabu cha Mormoni kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Juu ya haya ninashuhudia katika jina la Yesu Kristo, amina.