Nimethibitishwa na Kuimarishwa katika Kristo
Nyakati za kuthibitisha si uhalisia kwamba Bwana amekuacha. Badala yake, ni ushahidi kwamba anakupenda kiasi cha kutosha kukusafisha na kukuimarisha.
Wapendwa kaka zangu na dada zangu, ninahisi upendo wa Bwana tunapokutana pamoja. Ninanyenyekea kuzungumza nanyi. Ninamwomba Roho aingize mioyoni mwenu kile ambacho Bwana angetaka ninyi msikie, zaidi ya maneno ambayo mimi nitayasema.
Miaka mingi iliyopita, nilitafuta kujifunza fizikia na hisabati katika miaka yangu ya chuo kikuu. Nilihisi kuzidiwa. Nilianza kuhisi kwamba nilikuwa najaribu kujifunza kitu kilichokuwa nje ya uwezo wangu. Kadiri nilivyojisikia kuzidiwa, ndivyo nilivyokosa nguvu ya kuendelea kujaribu. Kuvunjika kwangu moyo kuliongoza kufikiri kwamba jitihada zangu hazikuzaa matunda. Nilianza kufikiria kuacha, na kufanya kitu kilicho rahisi zaidi.
Nilihisi kuwa dhaifu. Niliposali, nilihisi hakikisho tulivu la Bwana. Nilimhisi Yeye akiiambia akili yangu, “ninakuthibitisha wewe, lakini pia niko pamoja nawe.”
Sikujua wakati huo maneno yale yote yalimaanisha nini. Lakini nilijua nini cha kufanya—nilienda kazini.
Kwa kutafakari na kufanya kazi katika miaka iliyofuata, nilikuja kuelewa ujumbe huu wenye kutia moyo katika maandiko matakatifu: “Nayaweza mambo yote katika Kristo anitiaye nguvu.”
Nilikuja kujua kwamba mapambano yangu katika fizikia kwa kweli yalikuwa ni zawadi kutoka kwa Bwana. Alikuwa akinifundisha kwamba kwa msaada Wake ningeweza kufanya mambo ambayo yalionekana kuwa hayawezekani ikiwa nitakuwa na imani kwamba Yeye angekuwa hapo ili kunisaidia. Kupitia zawadi hii, Bwana alikuwa akifanya kazi ili kunithibitisha na kuniimarisha.
Neno thibitisha lina maana nyingi. Kuthibitisha kitu fulani sio tu kukijaribu. Ni kuongeza nguvu yake. Ili kukithibitisha kipande cha chuma ni kukiweka chini ya mkazo. Joto, uzito, na shinikizo vinaongezwa, hadi hali yake ya asili inapoboreshwa na kufunuliwa. Chuma hakifanywi kuwa dhaifu kwa sababu ya kuthibitishwa. Kwa kweli, kinakuja kuwa kitu fulani ambacho kinaweza kuaminiwa, kitu chenye nguvu vya kutosha kuhimili mzigo mkuu zaidi.
Bwana anatuthibitisha sisi katika njia hiyo hiyo ili kutuimarisha. Uthibitishaji huo hauji katika nyakati za furaha au faraja. Huja katika nyakati tunapohisi tumenyumbulishwa kupita kile tulichofikiri tungeweza kuvumilia. Bwana anafundisha kwamba tunapaswa kuendelea kukua na kamwe tusichoke katika jitihada zetu, kwamba hatukati tamaa, kwamba tunaendelea kujaribu.
Tunapoendelea kuwa na imani katika Yesu Kristo—hata wakati mambo yanapoonekana hayawezekani kwetu kwa wakati huo—tunakuwa imara zaidi kiroho. Kumbukumbu za maandiko matakatifu zinatilia mkazo ukweli huu.
Nabii Moroni, kwa mfano, alithibitishwa na kuimarishwa katika njia kama hii. Yeye aliishi miaka yake ya mwisho peke yake. Aliandika kwamba hakuwa na marafiki, kwamba baba yake alikuwa ameuawa, kwamba watu wake wameangamizwa. Alikuwa anawindwa na wale watu waliotafuta uhai wake.
Lakini bado Moroni hakukata tamaa. Badala yake, alichonga ushuhuda wake wa Yesu Kristo juu ya mabamba kwa ajili ya watu ambao hangeishi kuwaona, ikijumuisha uzao wa wale watu waliotamani kumuua yeye. Aliandika kwa ajili yetu sisi. Yeye alijua baadhi ya watu wangekebehi maneno yake. Alijua kwamba baadhi ya watu wangeyakataa. Lakini yeye aliendelea kuandika.
Katika kuthibitishwa kwake imani ya Moroni ilinolewa na kuimarishwa. Ikawa safi zaidi. Maneno yake yanabeba nguvu ya mtu ambaye alivumilia kwa uaminifu hadi mwisho. Tunaweza kuhisi nguvu hiyo tunaposoma ushuhuda wake:
“Sasa mimi, Moroni, naandika machache ambayo naona ni ya kufaa; na ninaandika kwa ndugu zangu, Walamani; na ningependa kwamba wajue kwamba zaidi ya miaka mia nne na ishirini imepita tangu ishara ilipotolewa ya kuja kwa Kristo.
“Na ninaweka muhuri maandishi haya, baada ya kuzungumza maneno machache kwa njia ya ushauri kwenu.
“Tazama, ningewashauri kwamba mtakaposoma vitu hivi, ikiwa itakuwa hekima katika Mungu kwamba myasome, kwamba mngekumbuka jinsi vile Bwana amekuwa na huruma kwa watoto wa watu, kutokea kuumbwa kwa Adamu hadi chini mpaka wakati ambapo mtapokea vitu hivi, na kuvitafakari katika mioyo yenu.
“Na mtakapopokea vitu hivi, ningewashauri kwamba mngemwuliza Mungu, Baba wa Milele, katika jina la Kristo, ikiwa vitu hivi si vya kweli; na ikiwa mtauliza na moyo wa kweli, na kusudi halisi, mkiwa na imani katika Kristo, atawaonyesha ukweli wake kwenu, kwa uwezo wa Roho Mtakatifu.
“Na kwa uwezo wa Roho Mtakatifu mtajua ukweli wa vitu vyote.”
Ushuhuda wa Moroni ulisafishwa katika upweke, lakini unang’ara kwa nuru ili kuongoza vizazi vyote kumtafuta Baba wa Mbinguni na Mwokozi Yesu Kristo.
Nabii mwingine wa Kitabu cha Mormoni, Yakobo, alithibitishwa na kuimarishwa kama mtoto aliyepitia mateso na huzuni nyingi. Lakini Lehi, baba yake, alimfundisha kuwa Mungu angembariki kupitia majaribu yake.
“Na tazama, katika utoto wako umeteseka kwa masumbuko na huzuni nyingi, kwa sababu ya ujeuri wa ndugu zako.
“Walakini, Yakobo, mzaliwa wangu wa kwanza nyikani, wewe unajua ukuu wa Mungu; na ataweka wakfu masumbuko yako kwa faida yako.
“Kwa hivyo, nafsi yako itabarikiwa, na wewe utaishi salama na kaka yako, Nefi; na utamtumikia Mungu wako maishani mwako. Kwa hiyo, najua kwamba wewe umekombolewa, kwa sababu ya haki ya Mkombozi wako; kwani wewe umeona kwamba katika wakati mtimilifu yeye atakuja kuwaletea wanadamu wokovu.”
Joseph Smith alipitia aina hii ya kuthibitishwa na kuimarishwa alipokuwa katika jela ya Liberty. Katika kina cha maumivu yake, Nabii Joseph alilia:
“Ee Mungu, uko wapi? …
“Ni kwa muda gani mkono wako utazuiliwa?”
Bwana aliona katika mateso ya Joseph matokeo ya kutakaswa yaliyotokana na kuvumilia kwake vyema wakati Yeye alipojibu:
“Mwanangu, amani iwe katika nafsi yako; taabu yako na mateso yako yatakuwa kwa muda mfupi;
“Na halafu, kama utastahimili vyema, Mungu atakuinua juu; nawe utawashinda maadui zako wote.”
Mfano mkubwa zaidi wa kuthibitishwa na kuimarishwa ulitokea kupitia Upatanisho wa Mwokozi. Alijichukulia juu Yake dhambi za ulimwengu. Ameyachukua maumivu na huzuni zetu. Alikunywa kikombe kichungu. Alithibitisha uaminifu katika kila wakati.
Kwa sababu ya Upatanisho Wake Mtukufu, Yesu Kristo anaweza kutuimarisha sisi katika nyakati zetu za majaribu. Yeye anajua jinsi ya kutusaidia kwa sababu Yeye amezijua changamoto zote ambazo sisi tutazijua katika maisha ya duniani. “Yeye atabeba maumivu na magonjwa ya watu wake … ili ajue kulingana na mwili jinsi ya kuwasaidia watu wake kulingana na unyonge wao.”
Tunajifunza kwamba wakati akiwa katika Bustani ya Gethsemane, Mwokozi alimwomba Baba ikiwa majaribu yale yangemwepuka—lakini Yeye pia alisema kama ni mapenzi ya Baba, basi Mwokozi angeyafanya. Katika maneno mengine, Mwokozi hata alitilia shaka na kutokuwa na uhakika, lakini alikuwa na imani kwa Baba Yake wa Mbinguni.
Akina kaka na akina dada kuthibitishwa na kuimarishwa kwenu yawezekana kusionekane kama vile kwa Moroni na Yakobo au kwa Nabii Joseph. Lakini kunakuja. Kunawezekana kukaja kimya kimya, kupitia majaribu ya maisha ya familia. Kunaweza kuja kupitia ugonjwa au kukatishwa tamaa, huzuni au upweke.
Ninatoa ushuhuda kwamba nyakati hizi sio ushahidi kwamba Bwana amekutelekeza. Badala yake, ni ushahidi kwamba anakupenda kiasi cha kutosha kukusafisha na kukuimarisha. Anakufanya wewe uwe imara vya kutosha kuweza kubeba uzito wa uzima wa milele.
Kama tunabaki waaminifu katika huduma yetu, Bwana atatutakasa. Yeye atatuimarisha. Na siku moja, tutatazama nyuma na kuona kwamba majaribu yale yale yalikuwa ushahidi wa upendo Wake. Tutaona kwamba alikuwa akitutengenezea umbo ili tuweze kusimama pamoja Naye katika utukufu. Kama Mtume wa Bwana Paulo alivyosema mwishoni mwa maisha yake mwenyewe, “Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda.”
Ninashuhudia kwamba Bwana anakujua wewe. Anajua majaribu unayokabiliana nayo. Yeye yu pamoja nawe. Yeye hatakuacha. Ninashuhudia kwamba Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu. Yeye ni nguvu yetu, ni Mkombozi wetu, ni tumaini letu. Kama tunamwamini, Atafanya nguvu yetu ya kiroho iwe sawa kwa kila jaribu tuliloitwa kulibeba. Ninashuhudia hivi katika jina takatifu la Yesu Kristo, amina.