2025
Jua Wewe ni Nani Hasa
Novemba 2025


10:46

Jua Wewe ni Nani Hasa

Bila kujali wapi tulipo kwenye njia ya uanafunzi, maisha yetu kimsingi yatabadilika ikiwa tutaelewa sisi ni kina nani hasa.

Miaka kadhaa iliyopita, binti yetu alikuwa na uzoefu wa kupendeza kwenye misioni yake. Kwa idhini yake, ninashiriki sehemu ya kile alichotuandikia wiki ile:

“Jana, muumini aliyerudi Kanisani baada ya kutohudhuria kwa muda mrefu alituomba tumtembelee haraka iwezekanavyo. Tulipofika, tulimkuta kwenye sakafu, akilia sana. Akiwa analia machozi, tuligundua kuwa alikuwa amepoteza kazi yake, alikuwa akitakiwa kuondolewa kutoka kwenye nyumba yake aliyokuwa akiishi, na kwa mara nyingine tena, atakuwa asiye na makazi.”

Binti yetu aliendelea: “nilianza kwa haraka haraka kupekua maandiko, nikijaribu kupata kitu—chochote kile ili kumsaidia. Wakati nikitafuta mstari maalum, nilifikiria, ‘Ninafanya nini? Hiki sicho ambacho Kristo angefanya. Hili sio tatizo ambalo ninaweza kulitatua, lakini huyu ni binti halisi wa Mungu anayehitaji msaada wangu.’ Hivyo, nilifunga maandiko yangu, nikapiga magoti pembeni yake, na kumkumbatia wakati tukilia kwa pamoja, mpaka alipokuwa tayari kusimama na kukabiliana na jaribu hili.

Baada ya dada huyu kuwa amefarijiwa, binti yetu kisha alitumia maandiko kujaribu na kumsaidia kuelewa uhalisia wa thamani yake takatifu na kumfundisha moja kati ya kweli za msingi za kuwepo kwetu duniani—kwamba sisi ni wana na mabinti wapendwa wa Mungu, Mungu ambaye anahisi huruma kamilifu kwa ajili yetu wakati tunaposumbuka na yuko tayari kutusaidia wakati tunapo simama tena wima.

Ni ya kuleta umaizi kwamba kanuni ya kwanza ya fundisho ambalo wamisionari wetu wanafundisha ni kwamba Mungu ni Baba yetu Mpendwa wa Mbinguni. Kila ukweli wa kimatokeo hujenga kwenye msingi wa uelewa wa sisi ni kina nani hasa.

Susan H. Porter, Rais Mkuu wa Watoto, alifundisha: “Unapojua na kuelewa jinsi gani kwa ukamilifu unapendwa kama mtoto wa Mungu, hilo hubadilisha kila kitu. Linabadilisha namna unavyohisi kuhusu wewe binafsi wakati unapofanya makosa. Linabadilisha jinsi unavyohisi wakati mambo magumu yanapotokea. Linabadilisha mtazamo wako juu ya amri za Mungu. Linabadilisha mtazamo wako juu ya wengine, na juu ya uwezo wako wa kuleta tofauti.”

Badiliko hili lina kielelezo wakati tunaposoma kuhusu uzoefu alioupata Musa wakati akizungumza na Mungu uso kwa uso. Wakati wa mazungumzo hayo, Mungu alirudia kumfundisha Musa kuhusu utakatifu wa urithi wake, akisema, “Musa, … wewe ni mwana wangu.” Mungu alifafanua kwamba Musa alikuwa ni mfano wa Mwanawe wa Pekee. Musa alipata kuelewa dhahiri kuwa yeye alikuwa nani, kwamba alikuwa na kazi ya kufanya, na kwamba alikuwa na Baba mpendwa wa Mbinguni.

Baada ya tukio hili, mjaribu alikuja kumjaribu na mara moja alimuita kwa kusema “Musa, mwana wa mtu.” Hii ni silaha ya mara zote na hatari iliyoko kwenye ghala la adui. Wakati Baba yetu wa Mbinguni mara zote na kwa upendo hutukumbusha kuwa sisi ni watoto Wake, adui daima atajaribu kutupa majina kwa kutumia madhaifu yetu. Lakini Musa tayari alikuwa amejua kwamba yeye alikuwa ni zaidi ya “mwana wa mtu.” Alimtamkia Shetani, “Wewe ni nani? Kwani tazama, mimi ni mwana wa Mungu.” Vivyo hivyo, wakati tunapokabiliwa na changamoto za maisha ya duniani au wakati tunapohisi kama mtu fulani anajaribu kutupatia jina kwa kutumia udhaifu wetu, tunahitaji kusimama imara katika uelewa wa ukweli wa sisi ni nani. Tunapaswa kutafuta uthibitisho kutoka juu, na si kutoka pembeni. Tunapofanya hivyo, nasi pia tunaweza kutamka kwa uthabiti, “mimi ni mtoto wa Mungu.”

Katika ibada ya ulimwenguni kote kwa ajili ya vijana waseja, Rais Russell M. Nelson alifundisha: “Hivyo wewe ni nani? Kwanza na zaidi ya yote, wewe ni mwana wa Mungu, mwana wa agano na mfuasi wa Yesu Kristo. Unapokumbatia kweli hizi, Baba yetu wa Mbinguni atakusaidia kufikia lengo lako kuu la kuishi milele katika uwepo Wake mtakatifu.”

Si kwa bahati kwamba katika maandiko yanayojirudia sana, Mungu hutukumbusha uhusiano wetu na Yeye. Katika majina yote ambayo Angeweza kutambulishwa nayo kwenye sala ya sakramenti, Yeye amechagua kuitwa “Mungu, Baba wa Milele.”

Tunapokuja kujua ukweli sisi ni akina nani, tutaamini zaidi kwamba Baba yetu mpendwa wa Mbinguni ametoa mpango kwa ajili yetu wa kurudi kuishi Naye tena. Mzee Patrick Kearon alifundisha: “Mpango mzuri wa Baba Yetu, hata ‘mpango Wake wa kupendeza’, umesanifiwa ili kukurudisha wewe nyumbani, sio kukuacha wewe nje. … Mungu anaweka juhudi endelevu kukutafuta.” Fikiria kuhusu hilo kwa muda—Baba yetu mpendwa mwenye nguvu zote anaweka “juhudi endelevu kukutafuta wewe.”

Bila kujali wapi tulipo kwenye njia ya uanafunzi, maisha yetu yatabadilika kwa kiasi kikubwa ikiwa tutaelewa sisi ni kina nani hasa. Ninaweza kupendekeza njia mbili ambazo kwazo tunaweza kulielewa hili kwa kina.

Kwanza, Sala

Wakati Mwokozi alipoanza huduma Yake duniani, aliongozwa kwenda nyikani ili “kuwa na Mungu.” Pengine tunapaswa kuondoa mawazo yetu kwenye kusema tu sala zetu na kuyapeleka kwenye kuchukua muda wa kutosha wa kuzungumza kwa dhati na “kuwa na Mungu” kila siku.

Nimegundua kwamba ubora wa sala huongezeka wakati ninapotumia dakika chache kujiandaa kuzungumza na Baba yangu. Maandiko yanatuonyesha kwamba mfumo wa aina hii hufanya kazi. Iwe Joseph Smith; Nefi, wana wa Helamani; au Enoshi, wote wana aina fulani ya mfumo wa kutafakari na kujichunguza kabla ya mawasiliano yao yaliyorekodiwa na Mungu. Enoshi alisema kwamba nafsi yake ilipata njaa wakati maneno ya baba yake yalipozama kwa kina moyoni mwake. Kila moja ya mifano hii hutufundisha hitaji la kujiandaa kiroho kila siku, “kuwa na Mungu.”

Kwa Wanefi, Mwokozi alielekeza, “Lakini wewe unaposali, ingia kwenye chumba chako kidogo, na wakati umefunga mlango wako, sali kwa Baba yako”

Iwe ni kwenye chumba kidogo au chumba cha kulala, kanuni iliyopo ni kupata mahali ambapo unaweza kuwa peke yako ili kusali, kuruhusu nafsi yako kuwa tulivu, na kuhisi misukumo ya “sauti ndogo tulivu.” Tunaweza kujiandaa kwa kutafakari kuhusu vitu ambavyo tuna shukrani navyo na kwa ajili ya dukuduku au maswali ambayo tungependa kupeleka kwa Baba. Tunapaswa kujitahidi kutokuwa na aina ya sala ya kujirudia rudia, lakini tuzungumze na Baba yetu, kwa sauti kama inawezekana.

Ninatambua kwamba changamoto za maisha yetu, wakati tunaposumbuka na watoto wachanga au kuharakisha mikutanoni tunaweza tusiwe na chumba kidogo cha kifahari na maandalizi yafaayo—lakini sala hizo za kimya kimya, za haraka, na dharura zinaweza kuwa za muhimu zaidi wakati tunapokuwa tumeweka juhudi ya “kuwa na Mungu” mapema katika siku.

Kunaweza kuwa na baadhi ambao hawajasali kwa muda mrefu au wengine ambao hawajahisi kwamba sala zao zinasikiwa. Ninawaahidi kwamba Baba yenu wa Mbinguni anawajua, anawapenda, na anataka kusikia kutoka kwenu. Anataka kuwasiliana nanyi. Anataka mkumbuke ninyi ni akina nani hasa.

Rais Jeffrey R. Holland hivi karibuni alifundisha, “bila kujali ni kwa bidii kiasi gani unasali, sali zaidi. Bila kujali unasali kwa bidii kiasi gani, sali kwa bidii zaidi.”

Kama nyongeza kweye ongezeko na utakatifu wa sala zetu, kujifunza Kitabu cha Mormoni kila siku na kuabudu hekaluni kutaandaa mawazo yetu kwa ajili ya ufunuo. Tunapojitahidi kuboresha mawasiliano yetu na Baba yetu wa Mbinguni, Yeye atatubariki tujisikie zaidi kwamba tu watoto Wake.

Pili, Kutambua kuwa Yesu ni Kristo

Dhihirisho kuu la upendo wa Baba yetu wa Mbinguni kwetu kama watoto Wake ni uhalisia kwamba Yeye alimtuma Mwanawe, Mwokozi wetu binafsi, ili kutusaidia kurudi nyumbani. Hivyo, tunapaswa kumjua Yeye.

Miaka kadhaa iliyopita, wakati nikihudumu kama rais wa kigingi, niliwasilisha pendekezo kwa ajili ya kaka kuhudumu kama mhudumu wa ibada za hekaluni. Baada ya kufafanua uzuri wa namna ambavyo mhudumu huyu wa ibada za hekaluni angekuwa, pasipo kukusudia nilibonyeza “Usimpitishe” na pendekezo langu liliwasilishwa. Baada ya kujaribu bila mafanikio kurudisha pendekezo lile, nilimpigia simu rais wa hekalu na kusema “nimefanya kosa kubwa.” Pasipo kusita, Rais huyu mwema wa hekalu alisema “Rais Eyre, hakuna ambacho umefanya kisichoweza kusamehewa na hatimaye kusahihishwa.” “Ni ukweli mkuu ulioje. Hakika, Yesu Kristo ana “uwezo wa kuokoa.”

Mwaka 2019, kulikuwa na mabadiliko makubwa kwenye maswali ya kibali cha kuingia hekaluni. Kabla ya hapo, moja ya swali liliuliza ikiwa ulikuwa na ushuhuda kuhusu jukumu la Yesu Kristo kama Mwokozi na Mkombozi. Sasa linauliza ikiwa una ushuhuda kuhusu jukumu lake kama Mwokozi na Mkombozi wako . Upatanisho wa Yesu Kristo si tu unafanya kazi kwa wengine; unafanya kazi pia kwako na kwangu. Yeye ni Mwokozi wangu. Yeye ni Mwokozi wako. Kila mmoja binafsi. Ni kupitia Yeye pekee wewe na mimi tunaweza kurudi kuishi na Baba yetu.

Hivyo, akina kaka na akina dada, acheni tumtafute Yeye. Acheni tujifunze uhusiano Wake mtakatikfu na Baba na kwa kila mmoja wetu. Acheni tupate uzoefu wa wimbo wa upendo wa ukombozi ambao huja binafsi kwa kila mmoja wetu kupitia Mkombozi wetu wakati tunapotubu. Wakati tunapokuja kumjua “yeye anayeweza kuokoa,” tutakuja kuelewa kwamba sisi, kama watoto wa Mungu ni shangwe Yake, fokasi Yake kuu zaidi, na hakika kila mmoja ni mwenye kustahili kuokolewa.

Ninashuhudia kwamba tunaye Baba mpendwa wa Mbinguni. Tupatapo kujua ukweli huu wa milele kupitia sala ya dhati, ufunuo binafsi, na kumuendea Yesu Kristo, tunaweza sasa na daima kwa ujasiri kutamka “mimi ni mtoto wa Mungu.” Katika jina la Yesu Kristo, amina.