Kujigundua Mimi Mwenyewe
Je, bado ninaweza kuwa muumini mzuri wa Kanisa hata kama nilikuwa na maswali?
Hivi karibuni niliwatazama ndugu zangu kila mmoja akichukua njia tofauti na mwingine. Kaka yangu alikuwa akijiandaa kwenda kuhudumu misheni. Kwa upande mwingine, dada yangu alikuwa akijiondoa kutoka Kanisani kabisa. Uamuzi wake ulikuwa wenye kunikanganya, na kwa muda, sikujua jinsi ya kulichakata.
Nilitambua kwamba imani yangu haikuwa kitu nilichochagua—ilikuwa ni kitu ambacho nilikuwa nimekua nacho. Nilihitaji kutambua kile ambacho hakika nilikikiamini mimi mwenyewe. Je, niliamini katika injili kwa sababu ilikuwa kweli, au kwa sababu ndicho pekee nilichowahi kufundishwa? Na bado ningeweza kuwa muumini mzuri wa Kanisa hata kama nilikuwa na maswali?
Niligeukia maandiko kwa azimio jipya. Nilianza kusoma nikiwa na maswali akilini, nikitafuta majibu na uelewa. Nilikuja kutambua kwamba kuuliza maswali kuhusu imani yangu haikumaanisha kuwa nilikuwa napoteza imani. Badala yake, ilimaanisha kwamba ningeweza kujenga msingi wa kina, wa kibinafsi zaidi.
Kujenga ushuhuda siyo tukio la mara moja; ni mchakato wa maisha yote wa kuuliza maswali, kutafuta, na kuthibitisha tena. Nimehisi Roho akinishuhudia kwamba injili ni ya kweli, lakini pia nimepitia nyakati nilipohisi kuwa mbali na Mungu. Imani si kitu kilichosimama; ni kitu ambacho lazima tukilee kila siku kupitia sala, kujifunza maandiko, na huduma.
Kukua katika Kanisa kumenipa msingi, lakini ni juu yangu mimi kujenga juu yake. Tunapoendelea kumgeukia Bwana, Yeye ataimarisha imani yetu na kutusaidia kushindana na mashaka ya maisha.
Mwandishi anaishi Kansas, Marekani.