Njia3 za Kumkataa Shetani na Kumchagua Yesu Kristo
Kuelewa kilichotokea katika maisha kabla ya kuja duniani kunaweza kukusaidia kufanya chaguzi nzuri sasa.
Vielelezo na Dean MacAdam
Wakati Baba wa Mbinguni alipowasilisha mpango Wake kwa ajili ya furaha na maendeleo yetu ya milele, Aliahidi kumtuma Mwokozi ili kutusaidia. Pale Baba alipouliza, “Nimtume nani?” (Ibrahimu 3:27), Yesu Kristo, “[Mwana wa Baba] Mpendwa na Aliyeteuliwa tangu mwanzo” (Musa 4:2), alisema, “Niko hapa, nitume mimi” (Ibrahimu 3:27). Yeye hakuomba chochote, Yeye alitaka tu kufanya mapenzi ya Baba yetu (ona Musa 4:2).
Kisha Lusiferi akaja. Yeye pia alisema, “nitume mimi” (ona Musa 4:1). Lakini Lusiferi alikuwa mchoyo, bila kuwa tayari kutoa dhabihu kwa ajili yetu. Alitaka heshima, nguvu na utukufu wa Mungu uwe wake yeye mwenyewe (ona Musa 4:1). Lusiferi alitaka kuangamiza haki yetu ya kujiamulia. Jinsi alivyofikiria kufanya hili haijulikani. Lakini tunajua kwamba bila haki ya kujiamulia, kamwe hatungeweza kuendelea na kuwa kama Baba yetu wa Mbinguni. Hivyo, kimsingi, Lusiferi aliasi dhidi ya Baba wa Mbinguni na kukataa mpango Wake.
Uasi wa Lusiferi ulisababisha vita mbinguni, ambapo “alitupwa chini;” naye “akawa Shetani” (Musa 4:3–4). Theluthi moja ya majeshi ya mbinguni yalimfuata (ona Mafundisho na Maagano 29:36). Lakini tulitumia haki yetu ya kujiamulia na kumfuata Yesu Kristo.
Vita ambavyo vilianza mbinguni bado vinaendelea hadi leo. Shetani na wafuasi wake daima wanatafuta kutupinga. Hapa kuna njia tatu za kutambua mbinu na mikakati ya Shetani, kuepuka mitego yake, na kumchagua Yesu Kristo katika maisha yetu yote.
1. Usiache Uchungu Ushinde
Miaka mingi iliyopita, wakati mmoja nilijaribu kuwashawishi marafiki zangu shuleni wasifanye kazi zao za nyumbani kwa sababu sikuwa nimefanya yangu. Nilikuwa katika kosa, lakini nilifikiri kwamba kama sote tungepata shida, kwa namna fulani ningehisi vizuri kuhusu mimi mwenyewe. Tabia yangu mbaya inanikumbusha mtazamo wa Shetani kwetu. Kwa sababu ana huzuni, anataka kuharibu uwezekano wetu wa uzima wa milele.
Shetani anasumbuliwa na uchungu wake mwenyewe kwamba yeye—hata akijua mwishowe atashindwa—kwa shauku anajaribu “kueneza kazi za giza” (Helamani 6:28), kuwadhuru wengi wetu kadiri awezavyo.
Uchungu wa Shetani sio mpango tulio uchagua. Tunaweza kutumia haki yetu ya kujiamulia kuendelea kumfuata Yesu Kristo na kuendelea kukataa ushawishi mchungu wa Shetani, rahisi, na wenye kujizuia wenyewe. Mwokozi alitoa uhai Wake ili tuweze kuwa kile Anachojua tunaweza kuwa na kuonja utamu wa uzima wa milele.
2. Usikubali kuingia kwenye Hofu
Wakati mwingine mimi hushangaa kwa nini sehemu ya tatu ya watoto wa kiroho wa Mungu wangechagua kukataa mpango Wake. Shetani anajua kwamba hofu na shaka vyote ni njia bora za kupunguza imani. Anaweza kutujaribu kutilia shaka thamani yetu au kutushawishi sisi kwamba kwa kweli hatuwezi kuwa wasafi kupitia Upatanisho wa Yesu Kristo. Au anaweza kujaribu kutufanya tuwe na hofu kuhusu kutubu au kufuata mpango wa Mungu.
Tunapokabiliana na majaribu na taabu, tunaweza kuchagua kuamini katika mpango wa Mungu na katika Yesu Kristo. Amevumilia vitu vyote ili Yeye aweze kuwa nguvu yetu wakati tunapokabiliana na hofu, na kupitia Kwake, hatimaye tunaweza kushinda.
3. Kumbatia Yote Ambayo Mwokozi Anakupa
Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo wote wako kwa ajili ya kutuwezesha. Nani mwingine anayesema wanataka kutusaidia kuwa bora kabisa na kutupatia kila kitu walicho nacho bila kushikilia? Kila kitu Baba alicho nacho kinaweza kuwa chetu! Hii imetolewa kwetu kupitia Yesu Kristo pekee.
Ninapofikiria kuhusu kukosa ubinafsi na nguvu za ukombozi za Mwokozi, ninataka kumfuata Yeye. Yesu Kristo ni bingwa mkamilifu wa mpango kamili. Tunapomchagua Yeye, Yeye hutusaidia kumshinda adui, kufuata mpango wa Baba wa Mbinguni, na kufikia hatima yetu ya kiungu.