Sauti za Vijana
Kuuheshimu Mwili Wangu
Kielelezo na Katelyn Budge
Ninaenda shule ambako wasichana wengi huvaa mavazi yenye kuonyesha maungo, wanakunywa kahawa, na kufanya chaguzi ambazo haziendani na maadili yangu.
Mwongozo wa Kwa Ajili ya Nguvu kwa Vijana umenisaidia kubaki mkweli katika amri na imani zangu. Kwa mfano, ninafuata Neno la Hekima, hivyo wakati marafiki zangu wanaponialika kupata kahawa, kwa upole nakataa. Wanapopendekeza aina fulani ya nguo, ninachagua mavazi ambayo ninajihisi vizuri na ya staha. Ninaamini staha ni muhimu kwa sababu miili yetu ni mahekalu. Ninapochagua kuvaa kwa staha, ninaonyesha heshima yangu kwa mwili wangu na shukrani zangu kwa Mungu.
Ninajaribu kutumia mafundisho ya injili katika maisha yangu ya kila siku, na ninapokabiliana na changamoto, ninageukia kujifunza maandiko kwa ajili ya mwongozo na ufunuo. Ninajua kwamba Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo wanatupenda. Baba wa Mbinguni daima atatuongoza na kutulinda tunapomtafuta Yeye. Hata katika njia ndogo, Yeye hutubariki kila siku.
Mamello M., umri miaka 16, Jimbo la Gauteng, Afrika Kusini
Anapenda kucheza chess, kuoka, kupiga ala za muziki, kujifunza lugha tofauti, kujifunza astronomia, kucheza hoki uwanjani, na kuunda sanaa.