2025
Njia za Mawasiliano Matakatifu
Machi 2025


“Njia za Mawasiliano Matakatifu,” Liahona, Machi 2025.

Njia za MawasilianoMatakatifu

Mungu huzungumza nasi katika njia tofauti. Na kuna mambo tunayoweza kufanya ili kuhakikisha mawasiliano haya yanaendelea kutiririka.

mtu akisali

Vielelezo na David Green

Nilipoanza kuandaa hotuba yangu ya kwanza ya mkutano mkuu, nilitambua kazi kubwa ambayo inaweza kuwa! Wanenaji katika mkutano mkuu hawapangiwi mada, hivyo nilihitaji kugundua mimi mwenyewe kile ambacho Bwana angetaka niseme.

Nilisali na kusubiria maelekezo. Baada ya muda, mke wangu, Isabelle, ambaye ni mwenye hekima na anayenijua vyema, aliniona nikihangaika kuanza.

“Angalia, unapaswa kufanya kitu,” alisema. “Anza na uandike kitu!”

Hicho ndicho nilichofanya. Katika mchakato huo, nilianza hotuba yamkini sita au saba hivi. Nilipotafakari uwezekano tofauti tofauti, nilipata faraja na moja na kuhisi ilikuwa ni hotuba niliyopaswa kutoa. Roho alituliza akili yangu, na hotuba yote ilitiririka.

Katika mkutano mkuu wa Oktoba 2023, nilishiriki kwamba sisi sote ni watoto wa Mungu. Yeye anatupenda, anatujua kwa undani, na yuko katika undani wa maisha yetu. Yeye hutusikia tunaposali na hutamani kuzungumza nasi.

Kujifunza jinsi Mungu anavyozungumza na kila mmoja wetu ni uzoefu binafsi. Lakini hapa kuna baadhi ya njia za kuwezesha mawasiliano ambayo Baba wa Mbinguni anataka kutupatia ili kubariki maisha yetu.

Tenda kwa Imani na Amini

Kutambua wakati Mungu anapoongea kunahitaji imani na tumaini. Imani daima imetia nanga katika Yesu Kristo. Pia tunahitaji kumwamini Yeye. Yeye amesema:

“Tazama, nitakujulisha wewe akilini mwako na katika moyo wako, kwa njia ya Roho Mtakatifu, ambaye atakujia na ambaye atakaa moyoni mwako.

“Sasa, Tazama hii ndiyo roho ya ufunuo (Mafundisho na Maagano 8:2–3).

Lakini ufunuo na maelekezo ya kiungu hayaji kutokana na kusubiri tu madhihirisho ya kiroho. Ni lazima tutende. Kama vile mke wangu alivyoniambia nifanye kwa hotuba yangu ya mkutano mkuu, wakati mwingine tunahitaji tu “kuanza.”

Wakati mimi na Isabelle tulipohudumu kama viongozi wa misheni katika Misheni ya Ufaransa Lyon, nilihitaji kuamua wapi kila mmisionari anapaswa kwenda ndani ya misheni na wakati gani wa kufanya kazi hiyo. Niligundua kwamba Roho angeniongoza kama ningesali kwa ajili ya msaada na kisha kutumia uamuzi wangu ulio bora. Uthibitisho kisha utakuja mara moja kila kitu kilikuwapo mahali pake.

Katika wito wangu wa sasa, ninatumwa kwenye vigingi kote katika Kanisa ili kupanga upya urais wa vigingi. Kama mwenza wangu na mimi tunapowahoji watu, tunakuwa na mawazo, hisia, na misukumo kuja kwetu. Kisha tunashauriana na kusali pamoja. Hatimaye, ufunuo huja, na Bwana hututhibitishia sisi ambao Yeye amemuita kumhudumia.

Ni mchakato wa kutambua wakati Mungu anapozungumza na kugundua mapenzi Yake. Tunahitaji kuonyesha kwamba tuko tayari kutenda kwa imani na tumaini.

Mfuate Nabii

Njia mojawapo muhimu ambayo Mungu huzungumza na watoto Wake ni kupitia manabii. Kuwa na nabii duniani leo ni habari njema! Anapokea ufunuo kutoka kwa Mungu ili kuelekeza na kuongoza Kanisa (ona Amosi 3:7). Tunaweza pia kupokea mwongozo na ulinzi kwa kufuata mafundisho yake. Hii siyo mara zote rahisi, lakini Bwana ametuelekeza kumfuata nabii “katika subira na imani yote” (Mafundisho na Maagano 21:5).

“Familia: Tangazo kwa Ulimwengu,” kwa mfano, limethibitika kuwa la kinabii tangu lilipotambulishwa miaka 30 iliyopita. Linazungumzia wasiwasi mwingi ambao hatukujua tungekuwa nao na kutoa mwongozo ambao si lazima tujue tungehitaji—lakini tunafanya hivyo sasa. Mwongozo wa nabii huenda usiwe kile tunachotaka kusikia. Huenda usifungamane na maadili ya sasa ya jamii. Bila kujali, tutaongozwa na kulindwa tunapomfuata nabii.

mwanamke akisoma maandiko

Uliza Maswali na Tafuta Majibu

Katika siku za mwanzo za Urejesho, Mungu mara nyingi alizungumza katika kujibu maswali ya dhati nabii Joseph Smith na wengine walikuwa nayo. Wakati Joseph na Oliver Cowdery wakifanyia kazi kutafsiri Kitabu cha Mormoni, walikuja kwenye mafundisho ya Mwokozi juu ya mafundisho ya ubatizo (ona 3 Nefi 11:23–33). Walitamani kujifunza zaidi na kwenda msituni kusali. Punde, Yohana Mbatizaji alitokea na kurejesha mamlaka ya kubatiza kwa kuzamishwa kwa ajili ya ondoleo la dhambi.

Wakati mwingine, mke wa Joseph, Emma, alielezea wasiwasi kuhusu uchafu ulioachwa na wanaume waliovuta kiko na kutafuna tumbaku wakati wa mikutano. Joseph alichukua jambo hilo kwa Bwana na kupokea ufunuo—“Neno la Hekima” (Mafundisho na Maagano 89:1)—juu ya desturi nzuri kwa manufaa ya kimwili na kiroho ya watoto wa Mungu.

Matukio haya—na mengine mengi—yanatukumbusha kwamba ni SAWA kuwa na maswali ilimradi tunatafuta majibu katika mwelekeo sahihi. Kama tutapeleka maswali yetu kwa Bwana, tutapata majibu. Wakati mwingine majibu yatakuja mara moja. Mara nyingi, hata hivyo, majibu huja “mstari juu ya mstari, kanuni juu ya kanuni, hapa kidogo na pale kidogo” (2 Nefi 28:30). Tunaweza kusubiri majibu ya kutusaidia kujifunza na kukua, lakini Mungu atatujibu kulingana na mapenzi Yake, njia, na wakati Wake.

Kumbuka Uzoefu Uliopita

Inapokuwa lazima tumsubiri Mungu azungumzie nasi, ni muhimu kwamba tung’ang’anie kile tunachojua na uzoefu tuliokuwa nao. Tunaweza kupoteza vinginevyo. Hatutakiwi kuwa na shaka juu ya uzoefu uliopita wa Roho kwa sababu tu yawezekana tunahangaika sasa. Katika nyakati hizo, tunapaswa kurudi katika akili zetu na kukumbuka jinsi tulivyojisikia wakati tulipohisi kuwa karibu na Mungu.

Alma wakati mmoja aliuliza maswali haya ya kujichunguza kwa watu wa Zarahemla:

“Mmezaliwa kiroho katika Mungu? Mmepokea mfano wake katika nyuso zenu? Mmeshuhudia mabadiliko haya makuu katika mioyo yenu? …

“Na sasa tazama, ninawambia, … ikiwa mmepata mabadiliko ya moyo, na ikiwa mmesikia kuimba wimbo wa upendo wa ukombozi, ningeuliza, mnaweza kuhisi hivyo sasa? Alma 5:14, 26.

Tunapaswa kuhakikisha tunakumbuka uzoefu wa kiroho na kutousukuma kando. Tunapaswa kujiuliza mara kwa mara, “ Naweza kuhisi hivyo sasa?” Hii inatuimarisha katika nyakati ambazo Mungu anaonekana kuwa kimya. Pia tunakuwa na uwezo bora wa kutambua nyakati anapozungumza nasi.

Baki Umeunganishwa

Mawasiliano na Baba yetu wa Mbinguni ni kitu hai. Tunafanya sehemu yetu ili kuiweka hai kwa kutafuta na kutengeneza fursa za mawasiliano matakatifu. Tunaweza mara kwa mara na kwa dhati kuomba kwa Mungu kwa ajili ya amani, faraja, na mwongozo. Tunaweza kujifunza neno Lake katika maandiko na kuhisi ushawishi wa Roho. Tunaweza pia kufuata mwongozo wa kinabii.

Tunapobaki tumeunganika na Baba yetu wa Mbinguni mwenye upendo, tunaweza kuwa vyombo katika mikono Yake ili kumsaidia yeye katika kazi Yake ya ajabu. Kwa kutii umaizi na ushawishi tunaopokea, tunaweza kuwasaidia wengine kuhisi kwamba Mungu anawajua na anawapenda na anatamani kuzungumza nao.

Hakikisho kwamba Mungu husikia na kuzungumza na watoto Wake ni baraka kubwa sana. Mawasiliano ya kiungu ya mara kwa mara na Yeye hutoa mwelekeo tunaohitaji ili kuongoza safari ya maisha.