Kujichukulia Jina la Yesu Kristo
Kadiri tunavyojitambua na kumkumbuka Yesu Kristo, ndivyo tunavyotaka zaidi kuwa kama Yeye.
Mwaka 2018, Chuo Kikuu cha Utah, kilianzisha uprofesa wa heshima uitwao “Kiti cha Urais cha Dkt. Russell M. Nelson na Dantzel W. Nelson katika Upasuaji wa Moyo na Kifua (Cardiothoracic Surgery)”—cardio, ikimaanisha moyo, na thoracic, ikimaanisha kifua. Hii inaheshimisha kazi muhimu ya Rais Nelson kama daktari wa upasuaji wa moyo na msaada aliopewa na marehemu mke wake, Dantzel. Uprofesa huu ulilipiwa na mfuko ulio sanifiwa ili udumu katika siku zijazo. Mtu aliye chaguliwa kwa aina ya uprofesa huu maarufu anapokea kutambuliwa, msaada wa mshahara na fedha za utafiti.
Daktari wa kwanza wa upasuaji wa moyo aliye chaguliwa kushikilia uprofesa huu alikuwa Dk. Craig H. Selzman, daktari mwenye umahiri wa upasuaji wa moyo ambaye si muumini wa Kanisa letu. Katika sherehe ya kutunza uprofesa huu kwa Dkt. Selzman, wageni wengi muhimu walihudhuria, wakiwemo Rais Nelson na mke wake Dada Wendy W. Nelson. Wakati wa mkutano, Rais Nelson alizungumza kwa kiasi kuhusu taaluma yake ya uanzilishi wa upasuaji wa moyo.
Kisha Dkt. Selzman alishiriki kile kilichomaanisha kwake kuteuliwa katika uprofesa huu. Alieleza kwamba siku nne zilizopita, baada ya siku ndefu kwenye chumba cha upasuaji, aligundua kwamba mmoja wa wagonjwa wake alihitaji kurudi kwenye upasuaji. Dkt. Selzman alikuwa amechoka na mwenye kukata tamaa, akijua kuwa angetumia usiku mwingine pale hospitali.
Jioni hii, Dkt. Selzman alikuwa na maongezi-ya-kubadilisha maisha yeye mwenyewe. Wakati huo, alifikiria, “Siku ya Ijumaa, nitateuliwa kwenye uprofesa unaoitwa kwa jina la Dkt. Nelson. Daima alijulikana kama mtu aliyedhibiti hisia zake, alimtendea kila mtu kwa heshima, na kamwe hakuwa na hasira. Sasa kwamba jina langu litakuwa limeunganishwa na lake, nahitaji kujaribu kuwa zaidi kama yeye.” Dkt. Selzman tayari alikuwa daktari wa upasuaji mahiri. Lakini alitaka kuwa hata bora zaidi.
Hapo awali, timu yake ya upasuaji inawezekana kuwa ilijua kuhusu uchovu wake na kukasirika kwake kwa sababu aliruhusu ionekane kupitia mtindo wake na sauti yake. Lakini katika chumba cha upasuaji usiku huo, Dkt. Selzman alifanya jitihada za kuwa mwangalifu sana ili kuwa mwenye msaada maalum na mwenye kuielewa timu yake. Alihisi kwamba ilileta tofauti na aliazimia kuendelea kujaribu kuwa zaidi kama Dkt. Nelson.
Miaka mitano baadaye, Rais Nelson alichangia nyaraka zake za kitaaluma kwa Chuo Kikuu cha Utah. Watu mashuhuri kutoka Chuoni walikuja kumshukuru rasmi Rais Nelson. Wakati wa tukio hili, Dkt. Selzman alizungumza tena. Akitaja herufi za Rais Nelson, RMN, alisema, “Kuna maadili ya jamii katika ‘RMN’ ambayo sasa yanaenea katika Idara ya Upasuaji wa Moyo na Kifua katika Chuo Kikuu cha Utah.”
Katika hali za kukata tamaa, Dkt. Selzman alieleza, “ninafanya kile tunacho wafundisha wanafunzi wetu kufanya—fokasi, sahau, na fanya vyema kadiri unavyoweza. Maadili haya yanaishi ndani yetu kila siku. Tunawapa pini za kifuani kila mshiriki wa idara na kila mwanafunzi mpya. Chini ya pini kuna herufi hizi‘RMN.’ Maadili ya RMN ni ya msingi kwa mafunzo yetu; tunayafundisha kwa kila mtu. Dkt. Selzman alikuwa kwa makusudi ameboresha mtazamo wake na matarajio yake ya awali kwa sababu jina lake sasa lilikuwa limeunganishwa na lile la Rais Nelson.
Mfululizo huu wa matukio unao mhusisha Dkt. Selzman ulinifanya nijiulize, “Je, mimi nimebadilikaje tangu nimeunganisha jina langu na jina la Yesu Kristo? Je, nimechukua maadlil kama ya Kristo kama matokeo yake? Je, nimejaribu kwa dhati kuwa bora na kuwa zaidi kama Yeye?
Katika uzoefu wa Dkt. Selzman, tunaweza kuona angalau milingano mitano ya mchakato ambao tunajichukulia juu yetu jina la Yesu Kristo. Ingawa mchakato huo unaanza na ubatizo, haukamiliki hadi pale tutakapo kuwa wasafi na watakatifu zaidi na kuwa zaidi kama Yeye.
Mlingano wa Kwanza ni utambulisho. Uteuzi wa Dkt. Selzman kwenye uprofesa wa Nelson uliunganisha jina lake na la Rais Nelson, na Dkt. Selzman aliaanza kujitambulisha pamoja na Rais Nelson. Tunapojichukulia juu yetu wenyewe jina la Yesu Kristo, tunaunganisha jina letu pamoja na Lake. Tunajitambulisha Naye. Tunafurahia kujulikana kama Wakristo. Tunamtambua Mwokozi na bila aibu tunasimama ili kuhesabiwa kama walio Wake.
Jambo linalohusiana kwa karibu na utambulisho ni mlinganisho mwingine—ukumbusho. Wakati Dkt. Selzman anapoingia ofisini kwake, macho yake yanavutwa kwenye medali aliyopokea alipochaguliwa kwenye uprofesa wa Nelson. Medali hii inamkumbusha kila siku kuhusu maadili ya RMN. Kwetu sisi, kushiriki sakramenti kila wiki kunatusaidia kumkumbuka Yesu Kristo kwa wiki nzima. Tunaposhriki sakramenti, tunafanya hivyo katika ukumbusho wa thamani ya gharama ambayo Yeye alilipa ili kutukomboa sisi. Tunafanya agano upya ili kumkumbuka Yeye, kutambua ukuu Wake na kuthamini wema Wake. Tunatambua tena na tena kwamba ni kwa neema Yake pekee tunaokolewa kutokana na kifo cha kimwili na kiroho.
Ukumbusho inamaanisha kwamba tunafuata ushauri uliotolewa na nabii Alma wa Kitabu cha Mormoni. Tunaacha “vitendo [vyetu] vyote viwe kwa Bwana, na po pote [tuendako, tuache] iwe kwa Bwana; … [tuache] mawazo [yetu] yote yaelekezwe kwa Bwana; … [na tuache] mapenzi ya [mioyo yetu] yawe juu ya Bwana milele.” Hata wakati tunapo jihusisha na mambo mengine, bado tunamkumbuka Yeye, kama tunavyo kumbuka majina yetu wenyewe, bila kujali kile kingine tunacho zingatia.
Ukuaji wa kukumbuka kile alichotufanyia Mwokozi ni mlingano wa tatu—kufuata mfano. Dkt. Selzman alianza kumuiga Rais Nelson na maadili ya RMN. Ninaamini kwamba maadili ya Rais Nelson ni dhihirisho tu la uanafunzi wake wa maisha yote kwa Yesu Kristo. Kwetu sisi, kadiri tunavyojitambua na kumkumbuka Yesu Kristo, ndivyo tunavyotaka kuwa zaidi kama Yeye. Kama wanafunzi wake, tunabadilika kuwa bora tunapo fokasi Kwake, zaidi ya tunapojitazama sisi wenyewe. Tunajaribu kuwa kama Yeye na kutafuta kubarikiwa kwa sifa Zake. Tunasali kwa bidii ili tujazwe na hisani, ule upendo msafi wa Kristo.
Kama Rais Nelson alivyofundisha mwezi Aprili: “Kadiri hisani inavyokuwa sehemu ya asili yetu, tutakosa hamu yaa kuwadhalilisha wengine. Tutaacha kuwahukumu wengine. Tutakuwa na hisani kwa wale wanaotoka katika hali zote za maisha. Hisani kwa watu wote … ni muhimu kwa ajili ya maendeleo yetu. Hisani ni msingi wa sifa ya uchamungu” Sambamba na hisani, tunatafuta, “kukuza, … na kupanua” zawadi nyingine za kiroho kutoka kwa Mwokozi, zikiwemo uadilifu, uvumilivu na bidii.
Kumuiga Yesu Kristo kunatuongoza kwenye mlingano wa nne—mfungamano na madhumuni Yake. Tunaungana Naye katika kazi Yake. Kama daktari wa upasuaji, Dkt. Nelson alijulikana kama mwalimu, mponyaji na mtafiti. Pini kwenye mkunjo wa koti kifuani inayotumika katika Kitengo cha Dkt. Selzman inasisitiza kazi hizi, zikionyesha maneno fundisha, ponya, na gundua. Kwetu sisi, sehemu ya kujichukulia juu yetu jina la Yesu Kristo inahusisha kwa hiari, kwa kukusudia, na kwa shauku kufungamanisha malengo yetu na Yake. Tunaungana Naye katika kazi Yake wakati “tunapopenda, tunaposhiriki na tunapoalika.” Tunaungana Naye katika kazi Yake tunapowatumikia wengine, hasa wale walio katika hatari na wale ambao wamejeruhiwa, kuharibiwa au kupondwa na uzoefu wao wa duniani.
Kwa hiyo tunajichukulia juu yetu jina la Yesu Kristo kwa ukamilifu zaidi kupitia utambulisho, ukumbusho, kuiga mfano na mfungamano. Kutenda haya manne yanatuongoza kwenye mlingano wa tano—uwezeshaji. Tunafikia nguvu na baraka za Mungu katika maisha yetu. Uprofesa wa Nelson unampa Dkt. Selzman utambulisho na fedha za msaada ambazo anazitumia kubadilisha utamaduni katika idara yake. Yeye anatumia hii “baraka ya nguvu” ili kuwasaidia watu wengine. Kwa njia hiyo hiyo, tunapojichukulia sisi wenyewe jina la Mwokozi, Baba yetu wa Mbinguni anatubariki kwa nguvu zake ili kutusaidia kutimiza misioni yetu katika maisha ya duniani.
Tunapofanya maagano ya ziada na Mungu, tunajichukulia juu yetu wenyewe kwa ukamilifu zaidi jina la Yesu Kristo. Kama matokeo yake, Mungu anatubariki zaidi kwa nguvu Zake. Kama Rais Nelson alivyofundisha: “Kila mtu anayefanya maagano katika visima vya ubatizo na hekaluni—na kuyashika—ameongeza ufikiaji wa nguvu ya Yesu Kristo. … “Thawabu ya kushika maagano na Mungu ni nguvu ya mbinguni … ambayo inatuimarisha sisi ili kustahimili majaribu, vishawishi na maumivu yetu ya moyo vyema zaidi.”
Tunakuwa wapokeaji zaidi kiroho. Tunakuwa na ujasiri zaidi wa kukabiliana na hali zisizowezekana. Tunaimarishwa zaidi katika azma yetu ya kumfuata Yesu Kristo. Kwa haraka zaidi tunatubu na kurudi Kwake pale tunapovunja sheria. Tunakuwa bora zaidi katika kushiriki injili Yake kwa nguvu Yake na mamlaka. Tunawasaidia wale walio katika shida bila ya kuwahukumu, bila kuwahukumu kabisa. Tunabakisha ondoleo la dhambi zetu. Tunakuwa na amani kubwa, na tunakuwa wenye shangwe zaidi kwa sababu daima tunaweza kushangilia. Utukufu wake utatuzunguka, na malaika Wake watakuwa na dhamana juu yetu.
Mwokozi anatualika, “Njooni kwa Baba katika jina langu, na katika wakati wake mtapokea utimilifu wake.” Ninawasihi kutenda haya. Njooni kwa Baba Yetu wa Mbinguni. Jichukulie juu yako jina la Yesu Kristo. Jitambulishe pamoja Naye. Daima mkumbuke Yeye. Jitahidi kuwa kama Yeye. Jiunge Naye katika kazi Yake. Pokea nguvu na baraka Zake katika maisha yako. Andika jina Lake moyoni mwako, kwa hiari na kwa kusudia. Hii inakupa wewe “hadhi” mbele za Mungu na kukustahilisha kwa ajili ya uombezi wa Mwokozi kwa niaba yako. Utakuwa mrithi aliyetukuka katika ufalme wa Baba yetu Mbinguni, mshirika wa urithi pamoja na Mzaliwa Wake wa Kwanza, Mwokozi wetu mpendwa na Mkombozi.
Yeye yu hai. Hakika ninajua hivyo. Yeye anakupenda. Yeye alitoa uhai Wake kwa ajili yako. Yeye anakusihi uje kwa Baba kupitia Kwake. Katika jina la Yesu Kristo, amina.