Wanajihukumu Wenyewe
Ikiwa tumetumia imani katika Yesu Kristo, kufanya na kushika maagano na Mungu, na kutubu dhambi zetu, kiti cha hukumu kitakuwa mahali pa kupendeza.
Kitabu cha Mormoni kinatamatisha kwa mawaliko wa kuvutia kutoka kwa Moroni wa “kuja kwa Kristo,” “kukamilishwa ndani Yake,” “na [tujinyime] ubaya wote,” na kumpenda Mungu kwa mioyo [yetu] yote, akili na nguvu.” Cha kustaajabisha, sentensi ya mwisho ya maelekezo yake inatazamia vyote, Ufufuko na Hukumu ya Mwisho.
“Hivi karibuni nitaenda kupumzika katika peponi ya Mungu, mpaka roho yangu na mwili vitakapounganishwa tena, na niinuliwe juu kwa ushindi kupitia angani, kukutana na ninyi mbele ya kiti cha enzi cha kupendeza cha yule Yehova mkuu, Mwamuzi wa Milele wa wanaoishi na waliokufa.”
Ninavutiwa na matumizi ya maneno ya Moroni “kupendeza” kufafanua Hukumu ya Mwisho. Manabii wengine kwenye Kitabu cha Mormoni vilevile wanaielezea hukumu kama “siku ya utukufu” na ambayo tunapaswa “kuitazamia [kwa] macho ya imani.” Lakini mara nyingi tunapotarajia siku ya hukumu, maelezo mengine ya kinabii huja akilini kama “aibu na hatia,” “woga na hofu ya kutisha,” na “taabu isiyo na mwisho.”
Ninaamini utofauti huu unaonyesha kwamba fundisho la Kristo lilimuwezesha Moroni na manabii wengine kuitazamia siku hiyo kuu kwa shauku na matumaini, badala ya woga waliouonya kwa wale ambao hawakujiandaa kiroho. Je, Moroni alielewa nini ambacho wewe na mimi tunahitaji kujifunza?
Ninasali kwa ajili ya usaidizi wa Roho Mtakatifu wakati tunapotafakari mpango wa furaha wa Baba wa Mbinguni na rehema, nafasi ya Mwokozi kwenye mpango wa baba, na jinsi “tutakavyowajibika kwa dhambi [zetu] wenyewe siku ya hukumu .”
Mpango wa Furaha wa Baba
Malengo makuu ya mpango wa Baba ni kutoa kwa watoto Wake wa kiroho fursa ya kupokea miili ya nyama na mifupa, kujifunza, “mazuri na maovu” kupitia uzoefu wa maisha ya duniani, kukua kiroho, na kupiga hatua milele.
Kile ambacho Mafundisho na Maagano hukirejelea kama “haki ya kujiamulia” ni kiini katika mpango wa Mungu wa kuleta kutokufa na uzima wa milele wa wana na mabinti Zake. Kanuni hii muhimu pia inaelezewa kwenye maandiko kama haki ya kujiamulia na uhuru wa kuchagua na kutenda.
Kirai “Haki ya kujiamulia” kina maana kubwa. Maneno yanayofanana na neno “haki” hujumuisha “nzuri,” “aminifu,” na “takatifu.” Maneno yanayofanana na neno “kujiamulia” hujumuisha “tendo,” “shughuli,” na “kazi.” Hivyo, “haki ya kujiamulia” inaweza kueleweka kama uwezo au fursa ya kuchagua na kutenda sisi wenyewe katika njia ambazo ni nzuri, aminifu, safi, na za kweli.
Uumbaji wa Mungu hujumuisha vyote “vitu vya kutenda na vitu vya kutendewa.” Haki ya kujiamulia ni “nguvu takatifu ya matendo huru” ambayo hutuwezesha sisi kama watoto wa Mungu kuwa mawakala wa kutenda na si vitu wa kutendewa.
Dunia iliumbwa kama sehemu ambapo watoto wa Baba wa Mbinguni wangeweza kuthibitisha ikiwa “wangefanya vitu vyote ambavyo Bwana Mungu wao angewaamuru wao kuvifanya.” Lengo la msingi la uumbaji na uwepo wetu duniani ni kutupatia fursa ya kutenda na kuwa vile ambavyo Bwana hutualika kuwa.
Bwana alimfundisha Henoko:
“Tazama ndugu zako hawa; wao ni kazi ya ustadi wa mikono yangu mwenyewe, nami niliwapa maarifa yao, katika siku ile niliyowaumba; na katika Bustani ya Edeni, nikampa mtu haki ya kujiamulia;
“Na kwa ndugu zako Mimi niliwaambia, na pia nikawapa amri, kwamba yawapasa kupendana, na kwamba yawapasa kunichagua Mimi, Baba yao”
Madhumuni makuu ya kutumia haki ya kujiamulia ni kupendana na kumchagua Mungu. Na madhumuni haya mawili hulandana kwa usahihi na amri ya kwanza na ya pili za kumpenda Mungu kwa moyo wetu wote, nafsi zetu zote na akili zetu zote, na kumpenda jirani kama nafsi zetu.
Fikiria kwamba tumeamriwa—si tu kuinua kiroho au kushauri, lakini tumeamriwa—kutumia uhuru wetu wa kuchagua kupendana na kumchagua Mungu. Acha nipendekeze kwamba katika maandiko, neno “maadili” si tu kivumishi lakini labda pia ni mwongozo mtakatifu kuhusu namna haki yetu ya kujiamualia inavyotakiwa kutumika.
Wimbo wa dini unaofahamika umepewa jina “Chagua Jema” kwa sababu maalum. Hatujabarikiwa kwa haki ya kujiamulia ili kufanya lolote tunalotaka vyovyote tunavyotaka. Badala yake, kulingana na mpango wa Baba, tumepokea haki ya kujiamulia ili kutafuta na kutenda kulingana na ukweli wa milele. Kama “mawakala [wetu sisi wenyewe],” tunapaswa kujishughulisha kwa shauku katika kazi njema, “kufanya mambo mengi kwa hiari [yetu] wenyewe, na kutekeleza haki nyingi.”
Ukweli wa milele kuhusu haki ya kujiamulia umeainishwa kwenye matukio ya kimaandiko ya baraza lililofanyika kabla ya sisi kuja duniani. Lusiferi aliasi dhidi ya mpango wa Baba kwa watoto Wake na alitafuta kuharibu nguvu ya matendo huru. Kwa sehemu kubwa, ukaidi wa shetani ulifokasi moja kwa moja kwenye kanuni ya haki ya kujiamulia.
Mungu alifafanua, “Kwa sababu … Shetani aliasi dhidi yangu, na akatafuta kuangamiza haki ya mtu ya kujiamulia, … nikamfanya atupwe chini.”
Mpango wa ubinafsi wa mwovu ulikuwa ni kuondoa uwezo wa watoto wa Mungu wa kuwa “mawakala wao wenyewe” ambapo wangeweza kujitendea kwa utakatifu. Nia yake ilikuwa ni kuwafanya watoto wa Baba wa Mbinguni kutendewa tu.
Kutenda na Kuwa
Rais Dallin H. Oaks amesisitiza kwamba injili ya Yesu Kristo hutualika kujua kitu fulani na kuwa kitu fulani kupitia kutumia kwa usahihi haki ya kujiamulia. Yeye alisema:
“Biblia na mengi ya maandiko ya sasa huzungumza kuhusu hukumu ya mwisho ambapo watu wote watazawadiwa kulingana na matendo yao au kazi zao au nia za mioyo yao. Lakini maandiko mengine yanaelezea zaidi kuhusu hili kwa kurejelea kwa sisi kuhukumiwa kulingana na hali ambazo tumezifikia.
“Nabii Nefi alifafanua Hukumu ya Mwisho katika njia ya namna ambavyo tumekuwa: ‘Na kama matendo yao yalikuwa machafu lazima wao wawe wachafu; na kama wao ni wachafu lazima iwe kwamba hawawezi kuishi katika ufalme wa Mungu’ [1 Nefi 15:33; msisitizo umeongezwa]. Moroni alitamka, ‘Yule ambaye ni mchafu ataendelea kuwa mchafu; na yule ambaye ni mwenye haki ataendelea kuwa mwenye haki’ (Mormoni 9:14; msisitizo umeongezwa).”
Kutokana na mafundisho hayo tunahitimisha kwamba hukumu ya Mwisho si tu tathmini ya majumuisho ya matendo mema na mabaya—yale tuliyoyafanya. Ni utambuzi wa athari ya mwisho ya matendo na mawazo—kile ambacho tumekuwa.”
Upatanisho wa Mwokozi
Matendo yetu na nia zetu pekee hazituokoi na haziwezi kutuokoa. “Baada ya kutenda yote tunayoweza,” tunapatanishwa na Mungu kupitia rehema na neema pekee inayopatikana kupitia dhabihu ya Mwokozi isiyo na mwisho ya kulipia dhambi.
Alma alitamka, “Uanze kuamini katika Mwana wa Mungu, kwamba atakuja kukomboa watu wake, na kwamba atateseka na kufa ili alipie dhambi zao; na kwamba atafufuka tena kutoka kwa wafu, na kutimiza ufufuo, kwamba watu wote watasimama mbele yake, kuhukumiwa katika siku ya mwisho ya hukumu, kulingana na matendo yao.”
“Tunaamini kwamba kwa njia ya Upatanisho wa Kristo, wanadamu wote wanaweza kuokolewa, kwa kutii sheria na ibada za Injili.” Ni shukrani iliyoje tunayopaswa kuwa nayo kwamba dhambi na matendo yetu maovu havitasimama kama ushuhuda dhidi yetu ikiwa kwa dhati “tunazaliwa upya,” kuwa na imani katika Mwokozi, kutubu kwa “moyo wa dhati” na “kusudi la dhati” na “kuvumilia hadi mwisho.”
Hofu ya Kimungu
Wengi wetu tunaweza kutegemea kwamba kusimama kwetu mbele ya kiti cha Hakimu wa Milele kutakuwa sawa na mchakato wa kesi kwenye mahakama ya kidunia. Hakimu atasimamia. Ushahidi utawasilishwa. Hukumu itatolewa. Na tutategemea kuwa na wasiwasi na waoga mpaka tutakapojua matokeo ya mwisho. Lakini ninaamini mfanano kama huo si sahihi.
Ingawa ni tofauti lakini unaoendana na woga tunaopata duniani ambao maandiko huuelezea kama “hofu ya kimungu” au “kumcha Bwana.” Tofauti na woga wa kiulimwengu ambao husababisha hofu na dukuduku, hofu ya kimungu hualika kwenye maisha yetu amani, uhakika, na ujasiri.
Hofu ya kimungu hujumuisha hisia za kina za unyenyekevu na kustaajabisha kuhusu Bwana Yesu Kristo, utiifu wa amri Zake, kutegemea Hukumu ya Mwisho na Haki mikononi Mwake. Hofu ya kimungu huzalishwa na uelewa sahihi wa asili takatifu na kazi ya Mwokozi, utayari wa kuacha mapenzi yetu kuwa sawa na Yake, na uelewa kwamba kila mwanamume na mwanamke atawajibika kulingana na matamanio yake, mawazo na maneno na matendo katika Siku ya Hukumu.
Kumcha Bwana si uwoga ambao huja kuhusu kusimama mbele ya uwepo wake ili kuhukumiwa. Badala yake, ni tazamio la hatimaye kukubali kuhusu jinsi tulivyo na jinsi tutakavyokuwa.
Kila mtu aliyeishi, anayeishi sasa, na atakayeishi duniani “ataletwa kusimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu, kuhukumiwa kulingana na matendo [yake] kama ni mema au kama ni maovu.”
Ikiwa matamanio yetu yamekuwa kwa ajili ya utakatifu na matendo yetu ni mema—ikimaanisha tumetumia imani katika Yesu Kristo, kufanya na kushika maagano na Mungu, na kutubu dhambi zetu—basi kiti cha hukumu kitakuwa mahali pa kupendeza. Enoshi alitamka, “tutasimama mbele ya [Mkombozi]; kisha [tutaona] uso wake kwa furaha.” Na katika siku ya mwisho “tutazawadiwa kwa haki”
Hata hivyo, kama tumetamani maovu na matendo yetu ni maovu, basi kiti cha hukumu kitatutia woga. Tutakuwa na “ufahamu kamili,” “tukijua kama tujuavyo sasa” na “uelewa wa hatia [zetu] wenyewe.” “Hatutaweza kumwangalia Mungu wetu katika hali hii mbaya; na tutakuwa na furaha kama tungeweza kuamuru miamba na milima ituangukie ili itufiche kutoka kwenye uwepo wake” Na katika siku ya mwisho tutapata zawadi [yetu] ya uovu”
Hatimaye, kisha, sisi tutajihukumu wenyewe. Hakuna yoyote atakayehitajika kutuambia wapi pa kwenda. Katika uwepo wa Bwana, tutakiri kile ambacho tumechagua kuwa katika maisha ya duniani na kujua sisi wenyewe wapi tunapaswa kuwepo milele yote.
Ahadi na Ushuhuda
Kuelewa kwamba Hukumu ya Mwisho inaweza kuwa ya kufurahisha si baraka iliyowekwa kwa ajili ya Moroni pekee.
Alma alielezea baraka zilizoahidiwa zinazopatikana kwa kila mfuasi aliyejitolea wa Mwokozi. Yeye alisema:
“Maana ya neno kurudisha ni kurejesha tena uovu kwa uovu, au mwili kwa mwili, au uibilisi kwa uibilisi—uzuri kwa lile ambalo ni zuri; haki kwa kile ambacho ni haki; adilifu kwa kile ambacho ni adilifu; rehema kwa lile ambalo lina rehema.
“… tenda yaliyo mazuri, toa hukumu kwa haki, na ufanye mema kila mara; na ikiwa utafanya vitu hivi vyote ndipo utakapopokea zawadi yako; ndiyo, utapata rehema irudishwe kwako tena; utapata haki kurudishwa kwako tena; utapata hukumu ya haki kurudishwa kwako tena; na utapata zawadi nzuri kutolewa kwako tena.”
Kwa furaha ninashuhudia kwamba Yesu Kristo ni Mwokozi wetu aliye hai. Ahadi ya Alma ni ya kweli na inatumika kwako na kwangu—leo, kesho, na hata milele. Ninashuhudia hivyo katika jina takatifu la Bwana Yesu Kristo, amina.