Karama ya Milele ya Ushuhuda
Kila mwana au binti wa Mungu anaweza kujipatia maarifa ya ndani zaidi, thabiti na ya uhakika.
Wapendwa akina kaka na dada zangu, hivi majuzi nimekuwa nikitafakari juu ya kweli tatu zenye nguvu kutoka kwenye Urejesho. Kweli hizi zimebariki sana maisha yangu. Leo, ningependa kushiriki nanyi jinsi ambavyo kweli hizi zimeniongoza katika safari yangu kuelekea ushuhuda wa hakika wa injili ya Yesu Kristo.
1. Mungu ni Baba Yetu wa Mbinguni Mwenye Upendo
Yeye ni mjuzi wa yote na muweza wa yote. Kupitia Nuru ya Kristo na huduma ya Roho Mtakatifu, ushawishi Wake uko kila mahali. Ni asili yake kutubariki.
Yeye anauona wakati wetu uliopita, wa sasa, na hatma ya milele. Hakuna kinachoweza kufichwa kwake.
Mwaliko wa Rais Russell M. Nelson wa “fikiria selestia” unatuhimiza tuige ono na asili ya Baba yetu wa Mbinguni.
Kwa sababu ya sifa Zake takatifu, Baba yetu wa Mbinguni hutupatia kila zawadi nzuri, kila mmoja akiwa na mtazamo Wake wa milele na ono akilini.
2. Haki ya kujiamulia ni zawadi ya kuamua na kutenda wenyewe
Pia ni jukumu la kuchagua vyema.
Yesu Kristo alilipa gharama ya fursa hiyo kwa damu Yake yenye thamani.
Wakati mwingine tunaweza kuamini kuwa haki ya kujiamulia inamaanisha kufanya chochote tunachotaka. Lakini ukweli kwamba gharama ililipwa inamaanisha kuwa haki ya kujiamulia ni zawadi takatifu.
Sisi ni mawakala, na mawakala wanawajibika kwa jambo fulani. Katika hali hii, tunawajibika kwa uchaguzi tunaofanya kulingana na ujuzi tulionao na karama tunazopewa. Hatuwezi kufanya uchaguzi bila kuwajibika kwa matokeo.
Kwa nini tuna haki ya kujiamulia?
Kuchagua mema.
Kumchagua Kristo.
3. Ushuhuda Wetu Huja Kupitia Nguvu ya Roho Mtakatifu
Ushahidi kutoka kwa Roho Mtakatifu ni mkuu kuliko kuona. Yeye ndiye shahidi mkuu wa Baba na Mwana. Rais Nelson alifunza, “Katika siku zijazo, haitawezekana kunusurika kiroho bila uzoefu wa kuongoza, kuelekeza, kufariji na ushawishi wa daima wa Roho Mtakatifu.”
Akina kaka na akina dada, hii ndiyo sababu kila mmoja wetu anahitaji nguvu ya Roho Mtakatifu leo.
Ushuhuda kupitia Roho Mtakatifu unaweza kuja kwa njia nyingi. Kama balbu ya mwanga katika chumba chenye giza, unaweza kuwaka kwa kasi na ghafla. Unaweza kuja kama jua hatua kwa hatua na baada ya muda. Unaweza kuja kama miale ya mwanga, mfiduo wa mara kwa mara kwenye akili safi. Vyovyote vile, huja kupitia kwa Roho Mtakatifu.
Kupata Ushuhuda huko Jamaica
Nilikulia katika Jamaika nzuri; ilikuwa ya kufurahisha na ya kupendeza. Hata hivyo, nilipoanza shule ya upili, baadhi ya wanafunzi wenzangu na marafiki hawakuelewa uamuzi wangu wa kuwa mshiriki wa Kanisa la Yesu Kristo. “Ungewezaje kujiunga na kanisa hilo?,” wangeuliza. “Ungewezaje kuamini hadithi hiyo?”—wakirejelea Ono la Kwanza. “Ungewezaje kusoma kitabu hicho?”—wakirejelea Kitabu cha Mormoni. “Je, kweli unaamini hayo yote?” Na “Kwa nini unapoteza maisha yako?”
Ilikuwa inaumiza, hasa ilipotoka kwa watu niliowajali.
Lakini jambo ambalo hawakujua lilikuwa hili: Nilipata uzoefu kwa Roho Mtakatifu. Ushuhuda huo ulipojaa moyoni mwangu, ulipunguza uchungu wa siku, na “kwa muda mfupi, mtazamo wa mbinguni [ulionekana] mbele ya macho yangu.”
Labda umeulizwa baadhi ya maswali haya. Labda, hata sasa unashambuliwa kama ilivyokuwa kwangu.
Karama na ushuhuda wa Roho Mtakatifu vinapatikana kwa kila mtu.
Jamaika kwangu ni kama Palmyra ilivyokuwa kwa Joseph Smith. Ni Kijisitu changu Kitakatifu. Sijui mahali hasa ambapo Joseph alipiga magoti kusali katika Kijisitu Kitakatifu, lakini ninajua hasa mahali nilipokuwa wakati Kijisitu changu Kitakatifu kilipokuja kuwa halisi. Ilitokea katika Barabara ya Four Grove, Mandeville, Jamaika, bafuni kwangu, saa 12:00 asubuhi siku ya Jumatano miaka mitatu baada ya ubatizo wangu. Uzoefu huu mtakatifu ulitokea kwa sababu wiki mbili mapema dada mmisionari aliyetiwa moyo alinialika kusoma Kitabu cha Mormoni. Dada Audrey Krauss anahudhuria mkutano huu leo pamoja na familia yake, na ninampenda milele.
Uzoefu huo ulinibadilisha.
Akina kaka na akina dada, ushuhuda hautolewi kwa matumizi ya muda. Zawadi hii kutoka kwa Baba yetu wa Mbinguni mwenye upendo imekusudiwa kuwa ya milele kwa sababu mtoaji ni wa milele. Ushuhuda haupaswi kuwa na tarehe ya mwisho wa matumizi. Haupaswi kudhoofika au kupungua kwa sababu kitu fulani katika maisha yangu kimebadilika au kitu kimebadilika ulimwenguni. Unapaswa kuwa na nguvu zaidi kwa sababu, kama vile talanta ya mtumishi katika mfano wa talanta, ushuhuda wangu binafsi ni zawadi ya kuzidishwa—si kuzikwa.
Nikitazama nyuma hizo siku ngumu za majaribio na mateso ambazo nilizipitia kama mtoto zilinisaidia kupata nafasi pale sasa ninapojua mwenyewe. Siamini tu, au kutumaini, ingawa hizi ni chembe muhimu za imani kwenye njia ya ushuhuda wa kweli. Ninakupongeza kwa kutengeneza njia yako mwenyewe kwa kuuliza maswali, kusoma, kuomba, kufunga na kutafakari. Tafadhali usisimame. Inafaa kila juhudi kufuata njia hii ya ushuhuda. Ni nani utamruhusu au nini utakiruhusu kuuchukua? Ni ushahidi gani mkubwa zaidi unaoweza kupata kuliko ule kutoka kwa Mungu?”
Kila mwana au binti wa Mungu anaweza kujipatia maarifa ya ndani zaidi, thabiti na ya uhakika. Kama Joseph Smith, ambaye alithibitisha ushuhuda wake licha ya upinzani, tunaweza kusema kwa ujasiri, “Nilijua, na nilijua kwamba Mungu alijua, na nisingeweza kukataa, wala kuthubutu kufanya hivyo.”
Akina kaka na dada zangu wapendwa, acha mche mdogo wa ushuhuda ufanye kazi ndani yenu hadi kuchipua kufikia maarifa yenye utukufu wa uhakika.
Kama wewe umebatizwa na kuthibitishwa kuwa muumini wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho lakini bado unahangaika na, “Sina hakika kama najua,” tafadhali kumbuka ahadi hii katika sala ya sakramenti: “Ili Roho wake apate kuwa pamoja nao daima.” Kwa sababu ya ahadi hii, kila mmoja wetu anaweza kufuata njia ya ushuhuda na maarifa ya uhakika.
Simamia Ushuhuda Wako
Sasa hapa kuna ukweli mkuu: Kwa njia yoyote ile ushuhuda unatolewa—iwe ni mwangavu kama mawio ya jua au unakuja katika ono tukufu—bado inahitajika uchaguzi kupokea zawadi hii ya thamani.
Kusema “Ninachagua kuamini” hurahisisha kupokea ushuhuda kutoka kwa Mungu. Ikiwa tunaona ushuhuda wetu unadhoofika, kumbuka kwamba ni chaguzi tunazofanya ambazo zinapunguza nguvu ya ushuhuda. Lakini ushuhuda haujaenda popote. Tunahitaji tu kuchagua kuungana nao tena.
Kuchagua kuamini ni njia ya busara na yenye nguvu ya kutumia haki yako ya kujiamulia.
Siwezi kuona njia bora ya kutumia haki yangu ya kujiamulia kuliko kutetea ushuhuda wangu.
Rais Nelson alifundisha: “Ninakusihi wewe kuchukua udhibiti wa ushuhuda wako. Ufanyie kazi. Umiliki. Utunze. Ulee ili kwamba uweze kukua. Ulishe ukweli.”
Kwangu, maneno simamia, fanya kazi, jali, miliki, lea na lisha yanasikika kama wakala aliyepewa usimamizi kwa kitu cha thamani na muhimu.
Katika Kanisa la awali, Parley P. Pratt alihisi kutoridhika na Nabii Joseph Smith na alichagua kumkosoa yeye na Kanisa. Wakati John Taylor ambaye Parley alimfundisha injili alipokuja mjini, Parley alimchukua kando na kumwonya kutomfuata Joseph. John Taylor akamwambia Parley:
“Kabla hujaondoka Kanada, ulitoa ushuhuda wenye nguvu wa Joseph Smith kuwa nabii wa Mungu, … na ulisema ulijua mambo haya kwa ufunuo na kipawa cha Roho Mtakatifu.
“… Sasa ninao ushuhuda uleule ambao wewe uliufurahia wakati ule. Kama kazi ilikuwa kweli miezi sita iliyopita, ni kweli leo. Kama Joseph Smith alikuwa nabii hapo mwanzo, basi hata sasa yeye ni nabii.”
Mimi nashuhudia kwamba Joseph Smith alikuwa nabii wa Mungu na kwamba vazi la kinabii alilopokea linaendelea leo. Yesu Kristo anaongoza kazi hii.
Ninawaalika kufikiria kuhusu njia yako ya ushuhuda wa uhakika wa Yesu Kristo na injili Yake. Simamia ushuhuda wako; tumia haki yako ya kujiamulia kwa busara na mtambue mtoaji na sifa Zake zote tukufu. Ninashuhudia kwamba nguvu iko ndani yako. Hakuna mtu anayeweza kukuchagulia. Hakuna mtu anayeweza kuchukua zawadi hii. Unaweza kuchagua kuamini.
Ninaahidi kwamba ukifanya hivi, ushuhuda wako utakuwa “maji ya kisima cha uzima, yakichipuka hata uzima wa milele.” Utakuwa ngao na ushawishi, na pia utakusaidia wewe pindi upitiapo magumu. Utakuwezesha katika kukuza karama za kiroho. Utakusaidia katika kuhudumu na huduma yako binafsi. Utakuwa silaha dhidi ya shetani na ushawishi wake. Ushuhuda wako utakuwa furaha unapouona ukisambaa kwa watoto wako, wajukuu, na vitukuu na kwa wale unaowapenda na kuwahudumia. Utakuwa wenye nguvu unapoushiriki na kuutumia kushuhudia.
Kama unajua, unajua. Ninajua kwamba ninajua. Tunahitaji mashahidi wa kweli wa Yesu Kristo na injili yake. Fika huko! Utafute! Ni jambo la dharura! Hiki ni kipindi cha mwisho—kipindi cha utimilifu wa nyakati.
Yesu Kristo alisema ukweli huu:“Mbingu na dunia zitapita; maneno yangu hayatapita.”
Akina kaka na akina dada, ushuhuda wa Yesu Kristo haukukusudiwa kamwe kuwa zawadi ya muda. Hakuna chochote kuhusu ushuhuda huo kilicho cha muda—si mtoaji, si zawadi yenyewe, si mfikishaji wa zawadi, si yule ambaye zawadi inamuhusu. Ushuhuda wako na uelezewe kwa njia sawa na hii. Ingawa “mbingu na dunia zitapita,” ushuhuda wako na ushahidi wa injili ya Yesu Kristo havitapita. Sasa ni muda wa kutwaa zawadi hii ya thamani. Katika jina la Yesu Kristo, amina.