Unyofu na Usafi kwa Kristo
Kutumia mafundisho halisi ya Kristo katika njia iliyorahisishwa na yenye fokasi kutatusaidia sisi kupata shangwe katika maisha yetu ya kila siku.
1. Utangulizi
Miaka thelathini na mitatu iliyopita nilipokea wito wangu wa kuhudumu kama mmisionari katika Misheni ya Ogden Utah. Hakika, kwa sababu nilikuja kutoka Ulaya, baadhi ya desturi za Utah kama vile “jeli ya kijani na karoti” au “viazi vya matangani” vilikuwa vitu vya kipekee sana!
Hata hivyo, nilifurahishwa sana na moyo wa ibada na uanafunzi wa wengi wa watakatifu, idadi tu iliyokuwa ikihudhuria mikutano ya Kanisa, na kiwango cha ufanyaji kazi kikamilifu cha programu za Kanisa. Wakati misheni yangu ilipofika tamati, nilitaka kuhakikisha kwamba shangwe niliyojisikia na nguvu ya kiroho na ukomavu niliouona vingepatikana pia kwa ajili ya familia yangu ya siku zijazo. Nilikuwa nimeazimia kurudi upesi kuishi maisha yangu katika “vivuli vya vilima vya milele.”
Hata hivyo, Bwana alikuwa na mipango tofauti. Jumapili yangu ya kwanza nyumbani, askofu wangu mwenye hekima aliniita nihudumu kama rais wa Wavulana katika kata yetu. Kuhudumia kundi hili la wavulana wazuri, nilijifunza upesi kwamba shangwe ambayo huja kutokana na kuwa mwanafunzi wa Kristo kwa vyo vyote vile haihusiani na ukubwa wa mikutano ya Kanisa au viwango vya programu.
Kwa hiyo nilipomuoa mke wangu mrembo Margret, kwa shangwe tuliamua kuishi Ulaya na kulea familia yetu katika nchi yetu ya nyumbani ya Ujerumani. Kwa pamoja tulishuhudia kile Rais Russell M. Nelson alichofundisha miaka mingi iliyopita “Shangwe tunayojisikia haichangiwi na hali ya maisha yetu na kitu cho chote kinachohusiana na fokasi ya maisha yetu.” Fokasi ya maisha yetu inapokuwa katika Kristo na ujumbe wa injili Yake, tunaweza kupata baraka kamili za uanafunzi mahali po pote tunapoishi.
Unyofu na Usafi Ambao Uko katika Kristo
Hata hivyo, katika ulimwengu ambao unaongezeka kuwa wa kiulimwengu, changamani, na wenye kukanganya, ukiwa na jumbe na matakwa tofauti na mara nyingi kinzani, ni kwa jinsi gani tunaweza kuepukana na macho yetu kupofushwa na mioyo yetu kufanywa iwe migumu na kubaki tumefokasi kwenye “vitu vilivyo wazi na vyenye thamani” vya injili ya Yesu Kristo? Wakati wa mkanganyiko, Mtume Paulo alitoa ushauri mkuu kwa Watakatifu wa Korintho kwa kuwakumbusha wao kufokasi kwenye “unyofu na usafi kwa Kristo.”
Mafundisho ya Kristo na sheria ya injili ni rahisi sana kiasi kwamba hata watoto wadogo wanaweza kuelewa. Tunaweza kupata nguvu za Yesu Kristo za ukombozi na kupokea baraka zote za kiroho Baba wa Mbinguni yetu ameziandaa kwa ajili yetu kwa kufanya imani katika Yesu Kristo, kutubu, kubatizwa, na kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu, na kuvumilia hadi mwisho. Rais Nelson alielezea safari hii vizuri sana kama “njia ya agano” ” na mchakato wa kuwa “mwanafunzi wa Yesu Kristo mwenye kumchamungu.”
Kama ujumbe huu ni rahisi hivyo, kwa nini mara nyingi ionekane kama changamoto kuishi sheria ya Kristo na kuufuata mfano Wake? Inaweza kuwa tunafafanua kimakosa unyofu na usafi kama kitu ambacho ni rahisi kukipata bila juhudi au bidii. Kumfuata Kristo kunahitaji juhudi za kila mara na mabadiliko endelevu. Tunahitaji “[kumvua] mtu wa asili na … [kuwa kama mtoto] mdogo.” Hii hujumuisha kuweka “tumaini letu kwa Bwana” na kuacha uchangamani kuondoka, kama vile tu watoto wadogo wanavyofanya. Kutumia mafundisho ya Kristo katika njia iliyorahisishwa na yenye fokasi kutatusaidia sisi kupata shangwe katika maisha yetu ya kila siku, kutupa mwongozo katika miito yetu, kujibu baadhi ya maswali changamani sana ya maisha, na kutoa nguvu za kukabiliana na changamoto zetu kubwa sana.
Lakini ni kwa jinsi gani sisi kiutendaji tunatelekeza hili kwa urahisi katika safari yetu ya maisha yote kama wanafunzi wa Kristo? Rais Nelson alitukumbusha tufokasi kwenye “ukweli halisi, mafundisho safi, na ufunuo halisi” tunapotafuta kumfuata Mwokozi. Mara kwa mara tukiuliza, “Ni nini Bwana Yesu Kristo angetaka nifanye? kunafunua mwelekeo muhimu. Kufuata mfano Wake kunatoa njia salama kupitia kutokuwa na uhakika na mkono wenye upendo, wenye kuongoza ili tuushikilie siku hadi siku. Yeye ni Mfalme wa Amani na Mchungaji Mwema. Yeye ni Mfariji na Mkombozi Wetu. Yeye ni Mwamba na Kimbilio Letu. Yeye ni Rafiki—rafiki yako na rafiki yangu! Yeye anatualika sisi sote kumpenda Mungu, kushika amri Zake, na kumpenda jirani yetu.
Tunapochagua kufuata mfano Wake na kusonga mbele kwa imani katika Kristo, kukumbatia nguvu ya Upatanisho Wake na kukumbuka maagano yetu, upendo hujaza mioyo yetu, tumaini na uponyaji vinainua roho zetu, na machungu na huzuni vinabadilishwa na shukrani na subira ya kusubiria baraka zilizoahidiwa. Wakati mwingine, tunaweza kuhitaji kujitenga mbali wenyewe kutoka kwenye hali zisizo nzuri na kutafuta msaada wa kitaalamu. Lakini katika kila hali, kutumia kanuni rahisi za injili kutatusaidia kupita changamoto za maisha katika njia ya Bwana.
Wakati mwingine tunapuuza nguvu tunayopokea kutokana na vitendo rahisi kama sala, kufunga, kujifunza maandiko, toba ya kila siku, kupokea sakramenti kila wiki, na kuabudu kila mara katika nyumba ya Bwana. Lakini tunapotambua kwamba hatuhitaji “kufanya vitu vikubwa” na kujikita wenyewe kwenye kutumia mafundisho halisi na rahisi, tunaanza kuona jinsi injili “inavyofanya kazi ya kushangaza” kwa ajili yetu, hata katika mazingira yenye changamoto sana. Tutapata nguvu na “kujiamini mbele za Mungu,” hata wakati tunapatwa na machungu. Mzee M. Russell Ballard alitukumbusha sisi mara nyingi, “Ni katika urahisi huo ambapo [sisi] tutapata … amani, shangwe, na furaha.”
Kutumia unyofu na usafi ambao upo katika Kristo hutufanya sisi kuweka kipaumbele kwa watu badala ya michakato na uhusiano wa milele badala ya tabia za muda mfupi. Tunafokasi kwenye “vitu ambavyo vina maana zaidi” katika kazi ya Mungu ya Wokovu na kuinuliwa badala ya kutekwa katika kusimamia utumishi wetu. Tunajiweka wenyewe huru ili kuvipa vipaumbele vitu ambavyo sisi tunaweza kufanya badala kulemewa na vitu tusivyoweza kufanya. Bwana alitukumbusha: “Kwa hiyo, msichoke kutenda mema, kwa kuwa mnaijenga misingi ya kazi kubwa. Na kutokana na mambo madogo huja yale yaliyo makuu.” Ni himizo lililoje la kutenda katika urahisi na unyenyekevu, bila kujali hali zetu.
3. Oma Cziesla
Bibi yangu Maria Cziesla alikuwa mfano wa kupendeza wa kufanya “mambo madogo na rahisi” ili kuwezesha mambo makuu. Kwa upendo sisi tulimwita Oma Cziesla. Oma alikumbatia injili katika kijiji kidogo cha Selbongen katika East Prussia pamoja na bibi wa mama yangu mnamo Mei 30, 1926.
Marta Cziesla (kulia) katika siku ya ubatizo wake.
Alimpenda Bwana na injili Yake na alikuwa ameazimia kuyashika maagano aliyokuwa amefanya. Katika mwaka wa 1930 aliolewa na babu yangu, ambaye hakuwa muumini wa Kanisa. Wakati fulani ilikuwa vigumu kwa Oma kuhudhuria mikutano ya Kanisa kwa sababu shamba la babu yangu lilikuwa mbali sana kutoka kwenye mkusanyiko uliokuwa karibu zaidi. Lakini yeye alifokasi juu ya kile ambacho angeweza kufanya. Oma aliendelea kusali, kusoma maandiko, na kuimba nyimbo za Sayuni.
Baadhi ya watu wangefikiria yeye hakuwa hai katika imani yake, lakini hilo lilikuwa mbali sana na ukweli. Wakati shangazi yangu na baba yangu walipozaliwa, kukiwa hakuna ukuhani katika nyumba ile na hakuna mikutano ya Kanisa au ufikiaji wa ibada karibu, yeye tena alifanya kile ambacho angeweza kufanya na kufokasi kwenye kuwafundisha watoto wake “kusali, na kutembea wima mbele za Bwana.” Aliwasomea kutoka kwenye maandiko, akaimba pamoja nao nyimbo za Sayuni, na hakika alisali pamoja nao—kila siku. Asilimia 100 ya uzoefu wa nyumba iliyo kitovu cha Kanisa.
Mwaka 1945 babu yangu alikuwa akihudumu katika vita mbali sana na nyumbani. Wakati maadui walipokaribia shamba lao, Oma aliwatwaa watoto wake wawili wadogo na kuliacha shamba walilolipenda na kwenda kutafuta kimbilio katika sehemu salama. Baada ya safari ngumu na ya kutishia maisha, mwishowe walipata kimbilio katika mwezi Mei 1945 huko kaskazini mwa Ujerumani. Hawakuwa na cho chote kilichobaki isipokuwa nguo kwenye miili yao. Lakini Oma aliendelea na kile alichoweza kufanya; alisali pamoja na watoto wake. Aliimba pamoja nao nyimbo za Sayuni alizokuwa amezikariri moyoni—kila siku.
Maisha yalikuwa magumu sana na kwa miaka mingi alifokasi tu katika kuhakikisha kulikuwa na chakula mezani. Lakini mwaka 1955 baba yangu, wakati huo akiwa na umri wa miaka 17, alikuwa anahudhuria shule ya ufundi katika mji wa Rendsburg. Akitembea karibu na jengo aliona ubao mdogo nje ambao umeandikwa “Kirche Jesu Christi der Heiligen der Letzten Tage”—“Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho.” Alifikiria, “Hiyo inapendeza; hili ni Kanisa la mama.” Kwa hiyo alipofika nyumbani, alimwambia Oma kwamba alikuwa amelipata kanisa lake.
Unaweza kufikira jinsi yeye alivyojisikia baada ya karibu miaka 25 ya kutokuwa na mawasiliano na Kanisa. Aliamua kuhudhuria Jumapili iliyofuata na kumshawishi baba yangu kuandamana naye. Rendsburg ilikuwa zaidi ya maili 20 (kilomita 32) kutoka kwenye kijiji kidogo pale walipoishi. Lakini hili halingemzua Oma kuhudhuria Kanisa. Jumapili iliyofuata, alipanda baiskeli yake pamoja na baba yangu na wakaenda kanisani.
Wakati mkutano wa sakramenti ulipoanza, baba yangu alikaa chini katika safu ya mwisho, akitumainia ingeisha punde. Hili lilikuwa kanisa la Oma na si lake. Kile alichokiona hakikupendeza sana: wanawake wakubwa wachache wakihudhuria na wamisionari vijana wawili ambao kwa ufanisi waliendesha kila kitu katika mkutano ule. Lakini kisha walianza kuimba, na waliimba nyimbo za Sayuni ambazo baba yangu alikuwa amezisikia tangu akiwa mvulana mdogo: “Njooni, Enyi, Watakatifu,” “Baba Yangu,” “Sifa kwa Aliyenena na Bwana.” Kulisikia hili kundi dogo likiimba nyimbo za Sayuni alizozijua tangu utotoni kulichoma moyo wake, na yeye alijua mara moja na bila shaka kwamba Kanisa lilikuwa la kweli.
Mkutano wa kwanza wa sakramenti ambao bibi yangu alihudhuria baada ya miaka 25 ulikuwa ndio mkutano ambao baba yangu alipokea uthibitisho binafsi juu ya ukweli wa urejesho wa injili ya Yesu Kristo. Alibatizwa wiki tatu baadaye, mnamo Septemba 25, 1955, pamoja na babu yangu na shangazi yangu.
Imekuwa miaka zaidi ya 70 tangu huo mkutano wa sakramenti mdogo huko Rendsburg. Mara kwa mara ninafikiria kuhusu Oma, jinsi yeye alivyojisikia katika usiku wa upweke wa siku zile, akifanya vitu vidogo na rahisi alivyoweza kufanya, kama kusali, kusoma na kuimba. Ninaposimama hapa leo katika mkutano mkuu na kuzungumza kuhusu Oma wangu, maamuzi yake ya kushika maagano yake na kumwamini Bwana licha ya mapambano yanaujaza moyo wangu kwa unyenyekevu na shukrani—si tu kwa ajili yake pekee bali kwa wengi wa Watakatifu wa kupendeza kote ulimwenguni ambao wanafokasi kwenye unyofu na usafi kwa Kristo katika hali zao zenye changamoto, pengine kuona mabadiliko kidogo sasa lakini kutumainia kwamba mambo makubwa yatatokea siku nyingine katika siku zijazo.
4. Vitu Vidogo na Rahisi
Nimejifunza kupitia uzoefu wangu mwenyewe kwamba vitu vidogo na rahisi vya injili na kufokasi kwa uaminifu katika Kristo hutuongoza kwenye shangwe ya kweli, vikileta miujiza mikubwa, na hutupatia kujiamini kwamba baraka zote zilizoahidiwa zitakuja. Hii ni kweli kwa ajili yako kama ilivyo kweli kwangu. Katika maneno ya Mzee Jeffrey R. Holland, “Baraka zingine huja haraka, zingine huchelewa, na zingine haziji hadi tufikapo mbinguni; lakini kwa wale wanaokumbatia injili ya Yesu Kristo, zinakuja.” Juu ya hili pia ninashuhudia katika jina la Yesu Kristo, amina.