“Ninataka Kuwa Kama Wewe,” Liahona, Sept. 2025.
Sauti za Watakatifu wa Siku za Mwisho
Nataka Kuwa Kama Wewe
Nilihisi wasiwasi mwingi ambao ulitokana na hofu ya mapungufu—hadi niliposali.
Kielelezo na David Malan
Baada ya siku ndefu, ngumu iliyojawa na masumbuko ambayo yanakuja kutokana na kuwatunza watoto watatu wadogo, yote niliyotaka kufanya ilikuwa ni kuoga na kwenda kulala.
Nilivuta pumzi kwa nguvu kisha nikaenda chumbani kwangu kupumzika. Hapo ndipo binti yetu wa miaka mitano alipoingia na kunikumbusha ilikuwa zamu yake kwa ajili ya mahojiano binafsi ya kila mwezi ambayo mimi pamoja na mume wangu tulianza kuyafanya pamoja na yeye na mtoto wetu wa kiume wa miaka mitatu. Tungewauliza maswali kuhusu vitu wanavyovipenda na vile walivyopenda kuhusu shule za awali au kanisani. Kisha tungewakumbusha kwamba wao walikuwa watoto wa Mungu na kwamba tuliwapenda.
Nilifurahia hotuba hizi, lakini sikuhisi kuwa vizuri kimwili au kiakili kuhusiana nazo. Nilianza kumwambia binti yangu tungekuwa na hotuba yetu kesho usiku, lakini niligundua jinsi hotuba zetu zilivyokuwa muhimu kwake.
“Sawa,” nilisema kwa uchovu, “hebu tumuipate Baba.”
Sisi watatu tulikaa kitandani na kuanza mazungumzo yetu. Baada ya mume wangu kuondoka chumbani kwa muda, nilimuuliza binti yetu, “Unataka kuwa nini unapokua?”
Sikuwa nimejiandaa kwa ajili ya jibu lake: “Kama wewe.”
Machozi yalitiririka machoni mwangu, na moyo wangu ukajawa na hisia. Niliguswa na jinsi binti yangu alivyoniona, lakini nilihisi wasiwasi mwingi ambao ulitokana na hofu ya kutokutosha. Nilifikiria juu ya sababu zote ambazo sikufanya mfano bora wa kuigwa kwa watoto wangu, na nilikuwa na ufahamu makini wa mapungufu yangu.
Baadaye usiku huo nilipokuwa nikisali, kwa dhati nilimwomba Baba wa Mbinguni anisaidie kuwa mfano bora kwa binti yangu na mwenye kustahili kupendezwa naye. Ghafla, wimbi kubwa la faraja, tumaini na upendo viliniosha. Nilitambua shukrani ambayo Baba yangu wa Mbinguni na Mwokozi walikuwa nayo kwangu mimi kwa kuwa mama ambaye alikuwa anajaribu kuwa bora zaidi. Walitambua juhudi zangu na walikuwa pale kunisaidia kuwa mama na binti Yao wanayemwona ndani yangu.
Ninajua kwa moyo wangu wote kwamba Mungu anatujua na anatupenda na kwamba kupitia “nguvu ya kuwezesha ya Upatanisho wa Mwokozi,” tunaweza kuwa wale tunaotumaini kuwa.