“Kama Mungu Angekuwa na Kanisa Duniani,” Liahona, Sept. 2025.
Picha za Imani
Kama Mungu Angekuwa na Kanisa Duniani
Niliwaambia wamisionari wasipoteze muda wao, kwamba nilikuwa na imani yangu mwenyewe. Lakini kisha nilikuja kujua kwamba mafundisho yao yalifanana na imani yangu kuhusu familia, Baba wa Mbinguni mwenye upendo, na Kanisa la Mwokozi.
Nilipokuwa mdogo, wazazi wangu walinichukua kwenye makanisa tofauti. Baadaye, kama kijana, nilianza kumgeukia Mungu na kuanza kusoma Biblia. Nilihisi vizuri.
Nilipofikiria kuhusu Mungu na madhumuni ya maisha, nilitambua kwamba ilikuwa muhimu kuwa na familia. Niliamini kwamba viongozi wa kanisa wanapaswa kufundisha kwa mfano, lakini katika kanisa nililohudhuria, makuhani hawakuoa. Hiyo haikuleta maana kwangu. Niliamini ilikuwa vizuri kuoa au kuolewa na kuwa na familia.
Nilikuwa na umri wa miaka 16 wakati huo. Nilikuwa na mpenzi niliyempenda sana, lakini aliniacha. Hilo lilikuwa jambo gumu kwangu. Niliteseka sana kwa karibu mwaka mmoja. Kwa sababu ya uzoefu huo, nilitaka kuelewa wapi nilitoka, kwa nini nilikuwa duniani, madhumuni ya maisha ni nini na kile kinachotokea baada ya kifo. Nilitaka kupata jibu la maswali haya mimi mwenyewe. Lakini baada ya kufikiria maswali haya kwa muda mrefu, nilimgeukia Mungu tena na kujisemea mwenyewe, “Muumbaji wa maisha anajua maisha vyema zaidi kuliko ninavyoyajua mimi. Ninapaswa kupata majibu kutoka Kwake.”
Kusoma Biblia, nilijifunza kwamba Yesu aliwaita Mitume Kumi na Wawili. ”Kama Mungu alikuwa na kanisa leo,” nilifikiri, ”lingepaswa kuwa na Mitume.” Nilivutiwa zaidi na zaidi na dini, na nilitaka kubatizwa.
Nilipozungumza kuhusu Mungu na baba yangu, aliniambia kwamba Mungu ni mwenye haki. Alisema aidha ubatizwe ili uokolewe, au umelaaniwa jehanamu milele. Sikutaka kuamini kwamba Baba wa Mbinguni mwenye upendo angefurahia kuwatuma watoto Wake kuzimu milele kwa sababu tu hawakuwa wamebatizwa. Vipi kuhusu wale ambao hawakuwa na nafasi ya kubatizwa?
Nchini Ufaransa, kuna waumini wachache. Nilikuwa na marafiki ambao walikuwa wazuri, lakini hawakubatizwa. Nilihitimisha kwamba haikuwa sawa kufikiri wote wangeenda jehanamu.
Kwa hiyo, niliamua kuunda imani yangu mwenyewe. Niliamini katika Mungu ambaye upendo wake ni mkamilifu na ambaye angefanya kila kitu kwa uwezo Wake ili kuwaokoa watoto Wake. Kama watoto Wake hawataki kupokea utukufu Wake, hiyo itakuwa juu yao. Lakini Yeye angewapa nafasi.
Mchepuko hadi Uongofu
Siku moja wamisionari wawili ambao walikuwa wakifanya kazi kijijini kwangu walihisi kuchukua njia ya mchepuko hadi kwenda nyumbani. Wakiwa njiani kwenda nyumbani, walikutana na mama yangu. Aliwasimamisha na kufanya miadi kwa ajili yangu ili nikutane nao. Sikuwa na furaha kuhusu hilo. Sikutaka kuongea nao. Nilidhani wangesema, “Lazima utusikilize sisi. Lazima uamini kile tutakachokuambia.”
Wakati wamisionari walipowasili kwa ajili ya mkutano wetu, niliwaambia, “Msipoteze muda wenu. Nina imani yangu mwenyewe. Kile mnachokifanya ni kizuri, lakini naamini kwamba familia ni muhimu sana. Ninaamini kwamba viongozi wa kanisa wanapaswa kufunga ndoa. Ninaamini kwamba kanisa linapaswa kuwa na Mitume kumi na wawili. Ninaamini kwamba Mungu atawaokoa watoto Wake wengi kadiri awezavyo. Na siamini katika uvutaji sigara na unywaji wa vileo.”
Nilishangaa kujifunza kwamba mafundisho yao yalilingana na imani yangu. Walinipa Kitabu cha Mormoni na wakaniomba kusali juu ya hicho kitabu. Nilimhisi Roho wakati niliposoma kitabu, na nilimhisi Roho nilipokuwa pamoja na wamisionari. Lakini nilifikiria, “Labda ninabuni tu hisia hizi chanya.”
Nilisali na kupata jibu katika ndoto. Katika ndoto yangu, nilifungua Biblia. Ndani ya Biblia kulikuwa na vichupo vingi vya vitabu tofauti vya Biblia. Kichupo cha mwisho kimesema “Mormoni.” Ujumbe huu ulinisaidia kuelewa kwamba Biblia na Kitabu cha Mormoni vilikuwa na injili ileile (ona Ezekieli 37:15–19).
Ushuhuda wangu uliimarishwa zaidi kupitia uzoefu mwingine wa kusoma na kujifunza Kitabu cha Mormoni. Wakati wamisionari waliponialika kubatizwa, nilikubali kwa shangwe. Nilibatizwa mwaka mmoja kamili baada ya mpenzi wangu kuniacha. Ubatizo wangu uliweka alama ya mabadiliko makubwa katika maisha yangu. Nilipoteza baadhi ya marafiki wakati nilipojiunga na Kanisa, lakini nilipata marafiki wapya katika tawi nililohudhuria.
“Injili iliniletea mwanga mwingi na furaha,” anasema Nicolas. “Mungu alinibariki. Nilikutana na mwanamke mwema, na tuna mabinti watatu wazuri.”
Injili iliniletea mwanga mwingi na furaha. Nilijawa na Roho na shangwe. Nilifikiria, “Yote ambayo nimeteseka kabla yamenileta hapa.”
Mungu alinibariki. Nilikutana na mwanamke mwema, na tuna mabinti watatu wazuri. Wawili kati yao wametumikia misheni, wakiwasaidia wengine kuelewa kile nilichokuja kuelewa miaka iliyopita: “Familia ni kitovu cha mpango wa Muumba kwa ajili ya hatima ya milele ya watoto Wake,“ “wafu wanaotubu watakombolewa, kupitia utiifu kwa ibada za nyumba ya Mungu (Mafundisho na Maagano 138:58), na Bwana huwaita mitume na manabii katika siku zetu ili kuliongoza Kanisa Lake (ona Waefeso 2:20).