2025
Hakujua Niliuhitaji
Kwa Ajili ya Nguvu kwa Vijana, Septemba 2025


Hakujua Niliuhitaji

Wakati nilipokuwa nahangaika, rafiki katika seminari alifuata msukumo.

msichana

Picha na Melanie Miza

Nilikuwa nikishughulikia baadhi ya maswala binafsi. Siku moja sikuwa najisikia vizuri, na kweli sikutaka kwenda seminari. Lakini niliwaza, “Ni mwaka wangu wa mwisho, na ninapaswa kupata faida yake.”

Hivyo nilienda, na tukazungumza kuhusu jinsi Yesu Kristo anavyomjua kila mmoja wetu kwa jina. Daima nimependa Mafundisho na Maagano 18:10: “Thamani ya nafsi ni kuu machoni pa Bwana.” Nilianza kupata hisia nilipokuwa nikiangazia mstari huu. Ninapopata hisia, ninalia sana, hivyo sikutaka kuusoma tena darasani.

Baadaye mwalimu aliuliza, “Nini kilikuvutia sana, na kwa nini?” Sikutaka kuzungumza, lakini rafiki yangu alitaja andiko hilo. Alitoa ushuhuda wake kwamba Mungu hatatuacha peke yetu, kwamba wakati mwingine tutasahau, lakini Yeye anatujua na Yeye atakuwa pale kwa ajili yetu.

Niliposikia hayo, ilihisi kama alikuwa Baba wa Mbinguni akizungumza nami kupitia rafiki yangu. Ilikuwa kama vile Yeye alikuwa anasema, “Usigeuke mbali nami—Nipo hapa.”

Baadaye nilienda kukausha uso wangu, na rafiki yangu akaja kwangu. Alisema, “Sikutaka kushiriki, lakini nilihisi nilihitaji kushiriki kwa sababu ingemsaidia mtu fulani. Sikujua kwamba mtu huyo fulani alikuwa wewe.” Hiyo ilinithibitishia hata zaidi kwamba Baba wa Mbinguni ananijali.

Baada ya seminari, nilienda nyumbani na kusali. Kwa kawaida, ninatoa shukrani na kuomba vitu. Lakini sala hiyo—nadhani ilikuwa sala ya shukrani zaidi ambayo nimewahi kuisema. Nilimhisi Roho katika chumba changu, na nilihisi kwamba Baba wa Mbinguni alikuwa pale pamoja nami.

Mwandishi anaishi huko Sacatepéquez, Guatemala.