“Nitakwenda Utakako,” Liahona, Jan. 2026.
Watakatifu katika Kila Nchi
Nitakwenda Utakako
Aliondoka nyumbani kwao, akasafiri baharini kuhubiri injili ya urejesho, na akafa akiwa na miaka 26, akiwa mkweli kwenye maagano yake.
Emma Purcell (safu ya kwanza) na wamisionari wengine katika Misheni ya Samoa, Oktoba 1902
Mnamo Mei 5, 1901, Emma Purcell mwenye umri wa miaka 17 alikubali wito wa misheni katika Samoa. “Ninawahakikishia, kila juhudi yangu itakuwa kuendeleza kazi ya Bwana,” aliandika katika barua kwa Rais Lorenzo Snow. Aliahidi zaidi, “Daima nitafurahia katika kutetea kanuni za Injili, wakati, na po pote fursa inapojitokeza yenyewe.”
Alipokuwa akijiandaa kuhudumu, Emma hakuweza kujua nini cha kutarajia. Alikuwa wa kipekee miongoni mwa wamisionari wenzake. Kanisa lilikuwa limeanza tu kuwaita wanawake waseja kama wamisionari wa kudumu miaka mitatu iliyopita. Na hadi sasa, yeye alikuwa mwenye umri mdogo zaidi aliyewahi kuitwa.
Pia angekuwa mwanamke wa kwanza Msamoa kuhudumu misheni. Ingawa aliishi Jijini Salt Lake, alikuwa amezaliwa Malaela, kijiji katika ncha ya mashariki ya kisiwa cha Samoa cha Upolu. Akiwa na umri wa miaka 12, alikuwa ameondoka nyumbani kwao na familia yake kuhudhuria shule huko Utah, maili 5,000 (kilometa 8,047)
Wazo la kurudi Samoa baada ya miaka mitano lazima lilikuwa la kusisimua na wasiwasi kwa Emma. Ili kujiandaa kiroho, alipokea endaumenti yake katika Hekalu la Salt Lake. Kama wamisionari leo, alifanya maagano matakatifu na Mungu na aliahidiwa baraka kupitia uaminifu wake.
Na, kama hadithi yake inavyoonesha, alifanya kila awezalo kuyashika maagano hayo alipokuwa akimtumikia Bwana.
Kutoka Upolu hadi Utah—na Kurudi
Emma alizaliwa Juni 26, 1883, mtoto wa saba wa Viliamu na Matafua Purcell. Familia yake ilikuwa moja ya familia kadhaa za Kizungu (sehemu Mzungu, sehemu Mpolinesia) ndani na kote kijijini Malaela. Mama yake alikuwa kutoka kisiwa cha Savai‘i, kaskazini na magharibi tu ya Upolu. Baba yake alikuwa mwana wa Mwiingereza ambaye alikuwa amekuja Samoa karibia mwaka 1834, alimuoa mwanamke wa Kisamoa, na aliishi Malaela.
Emma labda kwanza alijifunza kuhusu injili ya urejesho wakati akiishi na John na Nanave Rosenquist, wanandoa watakatifu wa Siku za Mwisho ambao walimchukulia kama binti waliyemuasili. Alibatizwa akiwa na umri wa miaka 12 mnamo Novemba 3, 1895. Mmisionari aliyehudhuria ibada hiyo alishuhudia juu ya roho mwenye nguvu aliyemhisi wakati wa ubatizo.
Miezi michache baadaye, John W. Beck, rais wa Misheni ya Samoa, alipokea idhini kutoka kwa Urais wa Kwanza kumtuma Emma na watoto wengine wa Samoa kwenda Utah kwa ajili ya kusoma shuleni. Aliondoka kutoka Apia, bandari kuu ya Upolu, pamoja na Rais Beck na wamisionari wengine mnamo Aprili 23, 1896. Ingawa wazazi wake wa kibaiolojia walikubali kuondoka kwake, walikuwa wakilia machozi walipokuwa wakisema kwaheri.
Ilimchukua Emma karibu wiki tatu kusafiri kwa meli ya mvuke na reli kwenda Jijini Salt Lake. Jiji lililikuwa kubwa zaidi kuliko kijiji chake kwenye kisiwa cha Upolu, na lazima alihisi kuzidiwa na mitaa yake yenye shughuli nyingi na sauti asizo zijua. Wakati huo, Utah ilikuwa na wakazi wachache wa Kipolinesia. Siku nyingi, asingemwona mtu ye yote aliye fanana naye.
Huko Utah, Emma aliishi katika Jiji la Salt Lake Kata ya Kumi na Tatu, alipata elimu nzuri katika shule zinazomilikiwa na Kanisa, na aliendelea kuwasiliana na wamisionari walio rejea kutoka Misheni ya Samoa. Mapema, askofu wake alitambua uwezekano wake na kumshauri ajiandae kuhudumu misheni katika nchi yake ya nyumbani.
Emma aliyachukua maneno yake moyoni, na wakati wito ulipokuja mapema mwaka 1901, alikuwa tayari.
Kuhudumu katika Malaela
Emma alirudi Upolu mnamo Julai 25, 1901, akiwa na furaha kumpata baba yake akimsubiri bandarini. Wakati alipoondoka, Emma alikuwa amepoteza uwezo fulani wa kuongea Kisamoa. Lakini alipoalikwa kusema sala ya kufunga kwenye mkutano, Roho alimpatia mwongozo wa kiungu, na akaitoa kwa lugha yake ya asili.
Emma alipangiwa kuhudumu huko Malaela, mji wake wa nyumbani, ambapo Kanisa lilikuwa limeendesha shule tangu mwaka 1896. Alipatiwa jukumu la kuwafundisha wanafunzi wa kike. Pia aliongoza Chama cha Uboreshaji wa Wanawake cha Tawi la Malaela. Siku za Jumapili na wiki nzima, angehubiri na kufundisha sambamba na wamisionari wengine.
Mwanzoni, baadhi ya watu wa familia ya Emma kisiwani humo walipinga kazi yake na kumsihi aache Kanisa. Kulingana na rais wa misheni William G. Sears, ingawa, “alitetea mwelekeo wake” na aliamua kushika maagano yake, licha ya upinzani.
Pia alijiunganisha mwenyewe na wamisionari wengine. Mara moja, kama mzaha, wazee wawili walibadilisha maji ya asili ya nazi yake na maji ya kawaida wakati wa kifungua kinywa. Utani “ulimkatisha tamaa” Emma, lakini aliwalipiza wazee wale kwa kuwahudumia nazi iliyofunikwa na chumvi badala ya sukari.
Mbali na utani kama huo, wamisionari hao walikuwa na heshima kubwa kwa “Dada Purcell.” Mmisionari mmoja alisema kwamba alikuwa “amejaa roho wa ofisi yake na wito wake.” Mzee mwingine aliandika kwa shukrani kuhusu ukarimu wake. Wakati mmoja, Emma aliacha ndizi kando ya njia ili yeye na mwenzake wapate kitu cha kula wakati wakisafiri.
Kumbukumbu zinaonyesha kwamba alihubiri juu ya mamlaka ya ukuhani, Kitabu cha Mormoni, na mada zingine za injili. Baada ya kumsikia Emma akihubiri juu ya maisha na misheni ya Joseph Smith, mmisionari mmoja aliandika, “Nilifurahia maneno yake sana; na alihuzunika alipoacha kuongea.”
Cha kusikitisha, Emma alipatwa na ugonjwa wa matende mwishoni mwa misheni yake na kupata kupumzishwa mapema. Wakati wanawake na wasichana shuleni walipojua kwamba alikuwa akirejea Utah, walilia. Tawi la Malaela lilifanya mkutano wa kumuaga, na kumpa nafasi moja ya mwisho ya kuhubiri. “Alizungumza kwa dhati kabisa,” kumbukumbu za mkutano zinaonyesha, “na aliwasihi wote kuwa wakweli kwa injili.”
Urithi wa Ibada
Emma mwenyewe alibaki mkweli kwa injili—na maagano yake—kwa maisha yake yote. Huko Utah, aliendelea na elimu yake, alishiriki katika jumuiya ya Wapolinesia ya jimbo, na kutoa ushauri juu kitabu cha kwanza cha nyimbo za dini cha Watakatifu wa Siku za Mwisho katika Kisamoa. Wakati fulani, pia alikutana na Mtakatifu wa Hawaii aliyeitwa Henry Kahalemanu. Walioana katika Hekalu la Salt Lake mnamo tarehe 31, Januari 1907.
Miaka mitatu baadaye, Emma alifariki akiwa na umri wa miaka 26 na kuzikwa huko Iosepa, makazi ya Watakatifu wa Kipolinesia maili 60 (km 97) magharibi mwa Jiji la Salt Lake. Ingawa maisha yake yalikuwa mafupi, kujitolea kwake kwa dhati kwenye injili ya urejesho ya Yesu Kristo bado ni mfano wenye nguvu kwa Watakatifu ulimwenguni kote, hasa wasichana wanaoitikia wito wa kuhudumu leo.