“Bwana Ataniongoza,” Liahona, Januari 2026.
Sauti za Watakatifu wa Siku za Mwisho
Bwana Ataniongoza
Kupitia imani, utiifu, subira, na sala, nimejifunza kwamba sihitaji kuhofu kwa ajili ya siku zijazo.
Kielelezo na Allen Garns
Nimekua nikiwa ninaimba na kuzungukwa na muziki. Ndoto yangu kama mtoto ilikuwa kuwa mwimbaji wa kulipwa. Hata nilishinda mashindano kadhaa ya kuimba. Lakini wakati fulani maishani mwangu, nilihisi utupu nilipofikiria kuhusu lengo ambalo Mungu alikuwa nalo kwangu zaidi ya kutambuliwa na sifa kutoka kwa wengine.
Kuwa na injili ya Yesu Kristo ikiongezeka katika maisha yangu kumenisaidia kuwa na imani katika nyakati za mashaka. Pia imenisaidia kuelewa kwamba Baba wa Mbinguni ananitaka nitumie talanta aliyonipa ili nimkaribie na kumtukuza Yeye.
Ingawa niliacha ndoto yangu, nilihisi kwamba nilipaswa kuendelea kuimba na kujifunza muziki.
Katika umri wa miaka 25, nilikuwa nimemaliza kujifunza usanifu wa majengo na pia nilikuwa nimesoma kupitia BYU–Pathway Worldwide na Brigham Young University–Idaho, ambayo ilinisaidia kuboresha uwezo wangu wa kuzungumza Kiingereza.
Kisha kitu cha kimuujiza kilitokea.
Nilipokea mwaliko wa kuwa mmisionari wa muziki kama sehemu ya Programu ya Mshiriki wa Tabenakulo ulimwenguni kote. Sikujua hilo, lakini kila kitu nilichokuwa nikifanya kwa miaka kadhaa kilisaidia kuniandaa kwa ajili ya wakati huu. Mwaliko ulikuwa ni jibu la sala na hamu zangu. Baba wa Mbinguni anajua mwisho kutoka mwanzo na kuniruhusu kuimba na Kwaya ya Tabernacle katika Temple Square wakati wa mkutano mkuu wa Oktoba 2024.
Kupitia uzoefu huu, ninaweza kushuhudia juu ya nguvu ya kuongozwa na Roho Mtakatifu, kuwa na subira, na kuamini kwamba Mungu ana kusudi, ingawa hatuwezi kuelewa kusudi hilo. Kama vile tulivyoahidiwa, “Njia ya haraka siku zote inaweza isiwe wazi, lakini tunaweza kumfuata Mwokozi kwa imani kwamba safari yetu itakwisha vizuri na kwa ushindi kwa sababu Yeye atatuongoza kwa usalama hadi kule tunakohitaji kuwa.”
Kwa wale wanaotafuta njia zao kwenda mbele, jua kwamba Bwana ameandaa kitu kwa ajili yako zaidi ya unavyoweza kufikiria. Tukimfuata Yeye, tutapokea kile ambacho Yeye ameandaa kwa ajili yetu. Njia inaweza isiwe wazi, na maisha yanaweza kuwa magumu, lakini Bwana bado anatenda miujiza kwa ajili ya watoto Wake.
Nimejifunza kwamba kupitia imani, utiifu, subira, na sala, Bwana ataniongoza.