“Toba Siyo tu Kuhusu Kushinda Dhambi,” Liahona, Jan. 2026.
Kutoka kwa VW Kila Wiki
Toba Siyo Tu Kuhusu Kushinda Dhambi
Kumgeukia Kristo—kubadilisha mitazamo yetu na kuwianisha mitazamo yetu na Yake—ni aina ya toba pia.
Kielelezo na Nate Wilde
Nilipokuwa misheni, nilikosa harusi ya rafiki yangu wa dhati.
Sikuweza kuacha kufikiria juu yake siku nzima. Tulikutana chuoni kama wakazi wa chumba kimoja, na haraka akawa kama dada kwangu. Nilijua kwamba Baba wa Mbinguni alikuwa ameniongoza kukutana naye.
Lakini sasa, sikuweza kuwa pale kusherehekea moja ya nyakati kubwa za maisha yake. Na nilighadhibika.
Majaribu Yasiyotarajiwa
Kabla ya misheni yangu, maisha yangu hayakuwa makamilifu, lakini yalikuwa mazuri. Nilipenda chuo na nilikuwa nimeunda urafiki bora niliowahi kuwa nao. Nilikuwa na furaha sana.
Nilijua kwamba kuhudumu misheni kungekuwa changamoto. Bado, nilikuwa na matarajio haya kwamba kuhudumu misheni kungekuwa miezi 18 bora ya maisha yangu—pamoja na ugumu mdogo.
Lakini miezi sita baadaye, harusi ya rafiki yangu ikawa kiingilio kipya zaidi katika orodha ya mambo magumu ambayo sikutarajia. Kuhamia nchi ya kigeni na kujifunza lugha mpya kulinifanya niwe mpweke na mwenye wasiwasi. Kukataliwa kukiwa sehemu ya maisha ya umisionari kulichosha kiakili. Kwa kweli, nilitaka tu kurudi nyumbani.
Nilikuwa nimechoka na kukata tamaa, na sikuhisi kama Mungu alikuwa ananipa tumaini na furaha ambayo nilihitaji sana. Ni baada tu ya kuchunguza sana kila chaguo lingine niligeukia ahadi kutoka katika baraka yangu ya kipatriaki: kwamba ningehisi upendo wa Baba wa Mbinguni kupitia maandiko.
Mtazamo Mpya
Nilipopekua maandiko, nilijikuta nikijihusisha kwa kina na hadithi ya Hawa. Alitupwa nje ya paradiso na kwenda kwenye nyika yenye giza na yenye kuchosha, ambayo ilikuwa aina ya jinsi nilivyojisikia. Sawa na uzoefu wangu, mabadiliko ya Hawa yalikuwa yamekuja kwa sababu ya uchaguzi mahususi. Nilijiuliza kama aliwahi kujutia uchaguzi wake, kama vile nilivokuwa naanza kujutia uchaguzi wangu wa kuhudumu.
Lakini Hawa alikuwa na mtazamo wenye hekima zaidi kuliko mimi. Ingawa kimsingi alikuwa amepoteza kila kitu, alipogundua kwamba alikuwa na Mwokozi, alikuwa na “furaha, akisema: Kama siyo kwa ajili ya uvunjaji wetu wa sheria … kamwe singeweza kujua mema na maovu, na shangwe ya ukombozi wetu” (Musa 5:11).
Hakujutia uchaguzi wake. Alikuwa na shukrani kwa hilo! Ingawa yeye na Adamu walikuwa wametupwa nje ya paradiso, shangwe ya kukombolewa ilikuwa tamu kuliko maumivu ya hasara yake. Kwa kweli, ilionekana kama ukombozi ulimletea shangwe zaidi kuliko kama hangehitaji kukombolewa kabisa.
Hii ingewezekanaje?
Utamu wa Toba
Tunaweza kufikiria kwamba toba ni kwa ajili tu ya kuondoa dhambi na tabia mbaya kutoka katika maisha yetu. Mchakato huo wa kuondoa unaweza kuwa mgumu na mara kwa mara wenye maumivu, na kuifanya iwe rahisi kuambatanisha dhana hasi kwenye neno hili.
Lakini toba siyo tu kuhusu kuwa mwenye dhambi kidogo. Pia ni kuhusu kuwa zaidi kama Kristo.
Kumgeukia Yeye—kubadilisha mitazamo yetu na kuwianisha mtazamo wetu na Wake—ni aina ya toba pia.
Nilitambua kwamba katika hasira yangu na upweke, mtazamo wangu ulikuwa finyu. Nimekuwa nimefokasi sana kwenye kile nilichokosa kwamba nilishindwa kuona kile nilichopata: uhusiano wa karibu na Mwokozi wangu.
Nilitambua nilihitaji kutubu kwa ajili ya mtazamo wangu duni. Ilichukua muda, lakini nilipoomba msaada wa Mkombozi wangu, nilihakikishiwa kwamba “katika maisha haya nitakuwa na shangwe” (Musa 5:10).
Nilikuwa bado na huzuni kwamba nilikosa harusi ya rafiki yangu, lakini baada ya muda, Bwana alijibu sala zangu. Nilikuwa na furaha sana kwa ajili ya rafiki yangu, na nilipata furaha kubwa katika ushuhuda wangu kwamba Baba wa Mbinguni hakika anaona na kumpenda kila mmoja wa watoto Wake. Nilipata mengi zaidi sana kuliko nilivyokosa.
Dada Kristin M. Yee, Mshauri wa Pili katika Urais Mkuu wa Muungano wa Usaidizi, alifundisha, “Kutubu kunaturuhusu kuhisi upendo wa Mungu na kumjua na kumpenda Yeye katika njia ambazo kamwe hatungeweza kujua.”
Kwa sababu ya toba, sasa najua kwamba ninaposogea karibu na Kristo, “ataifanya nyika [yangu] kuwa kama Edeni, na jangwa [langu] kama bustani ya Bwana; furaha na kicheko zitaonekana ndani yake” (Isaya 51:3).
Niliporudi nyumbani kutoka katika misheni yangu, sikurudi paradiso. Maisha baada ya misheni ni nyika mpya kwangu kuilima. Si rahisi, na wakati mwingine bado ninakosa maisha yangu ya kabla ya misheni yangu.
Lakini najua kwamba kwa sababu ya Kristo, shangwe yangu itafanywa kuwa ya kina katika ufahamu wa ukombozi wangu.