“Ninawezaje Kulalamika?,” Liahona, Januari 2026.
Picha za Imani
Ninawezaje Kulalamika?
Hatua zetu nne kama familia ya wakimbizi zilithibitisha kuwa mtihani mkubwa. Lakini tunashikilia fimbo ya chuma kwa uhakika kwamba Bwana anatusogeza kuelekea maisha bora ya baadaye.
Katika majira ya majani kupukutika ya mwaka 2019, niliwasili Uhispania pamoja na watoto wangu, Aaron mwenye umri wa miaka 8 na Jorge mwenye umri wa miaka 17, ambaye ana usonji. Kwa ndoto zangu tu zilizojaa kwenye sanduku, nilimshikilia Mungu na kumtumainia yeye kabisa.
Msamaria mwema alitukaribisha nyumbani mwake, ambamo tulikaa kwa wiki mbili. Lakini kumuondoa Jorge kutoka kwenye mazingira yake anayoyajua haikuwa rahisi. Kwa sababu ya hali yake, anafuata utaratibu madhubuti. Usiku wa siku chache za kwanza, angejigonga kwenye kuta, na kwa haraka ningeamka ili kumzuia kuwaamsha wengine. Nilipiga magoti karibu naye na kusali, nikikumbuka Isaya 41:10: “Usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu.”
Wakati wa wikiendi yetu ya pili huko Uhispania, tulifika kanisani wakati mkutano wa sakramenti ulipokuwa unamalizika. Nilimwendea msichana ambaye alikuwa na watoto wa Msingi na kuelezea kwamba nilikuwa muumini wa Kanisa lakini sikumjua mtu ye yote. Alitutambulisha kwa waumini wengine kadhaa.
Siku iliyofuata baraza la mji wa Zaragoza lilitukubali kama wakimbizi na kutupeleka kwenye fleti ya makazi ambayo haikuwa na maji au umeme. Uaskofu, Muungano wa Usaidizi wa Akina Mama, na akidi ya wazee kutoka katika kata tuliyohudhuria walikuja kutusaidia kwa blanketi, chakula ambacho hakihitaji kutiwa joto, nguo za majira ya baridi, na mahitaji mengine muhimu.
Watoto wangu walianza shule, na nilianza kozi ya mafunzo. Muda wa chakula ulikuwa changamoto kwa Jorge, ambaye alikuwa amezoea kula wakati wa mchana. Mwalimu wake binafsi alinijulisha kwamba bila kujali nani alikuwa anafundisha, wakati saa sita adhuhuri inapogonga, angetoa chakula chake na kuanza kula.
“Nami Nitafunga Pia”
Hatua zetu nne zilithibitisha kuwa mtihani mkubwa. Nilisali ili nibaki imara lakini mara nyingi nilijikuta nikilia pekee yangu. Kwa wiki kadhaa, nililala kwa saa mbili au tatu tu usiku. Baada ya siku kadhaa kutafuta kazi, nilibarikiwa kupata kazi ya kumtunza mwanamke kijana mwenye saratani ya ubongo isiyotibika. Baada ya kila zamu ya kazi, nilipita kuwachukua watoto wangu, nikawasaidia kwenye masomo yao, na kisha kufanya kazi yangu ya mafunzo nyumbani.
Nilimtunza huyu mwanamke mzuri kijana kwa mwaka mmoja, hadi alipofariki akiwa na umri wa miaka 48, akiwaacha watoto wawili wadogo. Hali yake ilinisukuma kujiuliza, “Ninawezaje kulalamika?” Kumtunza yeye kulikidhi mahitaji yetu na kujaza nafsi yangu kwa shukrani kwa Baba yangu wa Mbinguni.
Kila siku nyumbani tulisoma maandiko, tulisali, na kuanzisha utaratibu wa kumpa Jorge usalama. Mapema mwaka 2024, tulianza maandalizi ya kwenda Hekalu la Madrid Spain. Ili kuwa karibu na Baba wa Mbinguni, nilihisi kwamba tunapaswa kufunga kama familia. Aaron alikubali, na asubuhi iliyofuata Jorge aliniambia, “Mama, leo nitafunga pia.” Ilikuwa ni wakati wa shangwe isiyoelezeka.
“Ili kuwa karibu na Baba wa Mbinguni tulipoanza maandalizi ya kwenda Hekalu la Madrid Spain, nilihisi kwamba tunapaswa kufunga kama familia,” anasema Yesmin. “Jorge aliniambia, ‘Mama, leo nitafunga pia.’ Ilikuwa ni wakati wa shangwe isiyoelezeka.”
Tangu matembezi yetu hekaluni, Jorge hali yake imeimarika kwa kiasi kikubwa. Anaweza kubadilisha kwa urahisi zaidi katika ratiba yake. Siku za Jumamosi anaandaa nguo zake ili aweze kuwa tayari kupitisha sakramenti siku ya Jumapili. Pia amefanya maendeleo makubwa kielimu.
Leo tunakidhi mahitaji yetu sisi wenyewe, tukisaidiwa na Baba wa Mbinguni mwenye upendo. Yesu Kristo ametuinua kutoka kwenye majivu (ona Isaya 61:3). Kwa kulipa zaka yetu, tumepokea baraka tele. Tunashikilia fimbo ya chuma (ona 1 Nefi 8:24, 30; 11:25; 15:23) kwa uhakika kwamba tunasonga mbele kuelekea maisha bora ya baadaye.