Liahona
Kumtafuta Kristo na Maagano: Funguo za Nefi za Kusoma Agano la Kale
Januari 2026 Liahona


Kumtafuta Kristo na Maagano: Funguo za Nefi za Kusoma Agano la Kale

Nefi alishiriki baadhi ya utambuzi ambao unaweza kukusaidia katika kujifunza kwako.

kielelezo cha Yesu Kristo

Picha ya Kristo, na Heinrich Hofmann, kwa hisani ya C. Harrison Conroy Co. Inc.

Ninapenda kusoma Agano la Kale Kwa miaka mingi, nimegundua funguo mbili za kutafuta katika Agano la Kale ili kuleta shangwe na kuongeza uelewa: Kristo na maagano.

Hapa ni baadhi ya njia tunazoweza kumpata Kristo na maagano katika kujifunza kwetu Agano la Kale mwaka huu.

Kumtafuta Kristo

Nefi, ambaye alisoma maandiko kutoka kwenye mabamba ya shaba, alisema, “Tazama, nafsi yangu inafurahia kuwathibitishia watu wangu ukweli wa kuja kwa Kristo; kwani, ni kwa lengo hili kwamba sheria ya Musa imetolewa; na vitu vyote vilivyotolewa na Mungu tangu mwanzo wa dunia, kwa mwanadamu, ni kielelezo chake”(2 Nefi 11:4).

Tunaweza kumpata Yesu Kristo katika Agano la Kale katika njia nyingi.

vielelezo vya nyoka wa shaba na Mwokozi juu ya msalaba

Musa na Nyoka wa Shaba, na Judith A. Mehr; Kristo juu ya Msalaba, na Carl Heinrich Bloch

Mungu wa Agano la Kale

Kwa sababu tunajua kupitia ufunuo wa sasa kwamba Yesu Kristo ni Mungu wa Agano la Kale (ona Mafundisho na Maagano 110:3–4), tunaweza kuona nguvu Zake katika Uumbaji na kama Mtoa Sheria juu ya Mlima Sinai akifundisha Israeli jinsi ya kuwa kama Mungu. Tunajifunza kuhusu neema Yake katika ukombozi kutoka utumwani huko Misri, upendo Wake katika kuwajali watu Wake nyikani na kuwaleta hadi nchi ya ahadi, na kuendelea kushughulika Kwake kwa kuwatuma manabii na kutoa msamaha kwa Israeli kadiri walivyo tubu dhambi zao.

Aina za Yesu Kristo

Kuna aina nyingi (au mawakilisho) ya Yesu Kristo katika hadithi za Agano la Kale, nyingi zinaonyesha ishara ya ujio Wake ujao kama ilivyoandikwa katika Agano Jipya na Kitabu cha Mormoni. Hadithi ya Ibrahimu na Isaka inaonyesha ishara za Mungu Baba akimtoa dhabihu Mwanawe, Yesu Kristo. Yusufu aliwaokoa ndugu zake kutokana na njaa ya kimwili, kama vile Yesu Kristo anavyotuokoa kutokana na njaa ya kiroho. Musa aliwaweka huru watu wake kutoka utumwani kama vile Yesu anavyotuweka sisi huru kutokana na dhambi. Bwana aliwafundisha wana wa Israeli nguvu ya imani katika Yeye na Upatanisho Wake katika hadithi ya nyoka wa shaba nyikani. Eliya na Elisha walitoa mfano wa Mwokozi walipowaponya wagonjwa na kuwafufua wafu.

kielelezo cha Ibrahimu na Isaka

Ibrahimu na Isaka, na Harold Copping, © Look and Learn/Bridgeman Images

Utambuzi katika Mwokozi wa Agano Jipya

Yesu Kristo kiishara yuko katika hadithi za Agano la Kale na sheria ya Musa. Hadithi za Pasaka na dhabihu katika sheria ya Musa zinamwonyesha Kristo. Zikionyesha ishara za misheni ya Yesu, manabii katika Agano la Kale waliwaponya wagonjwa na kuwafufua wafu. Kupitia nabii Yeremia, Bwana alituahidi “agano jipya” (Yeremia 31:31; ona pia mstari wa 32).

Katika Agano Jipya, Yesu anakuja kama utimilifu wa sheria na manabii katika Agano la Kale. Yeye alileta agano jipya katika Mahubiri ya Mlimani na kuweka ishara za agano wakati wa mlo wa Pasaka katika Karamu ya Mwisho. Yesu alitufundisha kupendana na kutumikiana wakati alipowaponya wagonjwa na kuwafufua wafu. Yeye alitukomboa kutokana na dhambi na kifo kupitia Upatanisho Wake, na Yeye alianzisha Kanisa Lake duniani. Tunapomtambua Yesu kama Mungu wa Agano la Kale, tunaweza kumwelewa Yeye vyema zaidi katika Agano Jipya.

Kutafuta Maagano

Nefi pia alitufundisha kutafuta maagano katika maandiko: “Na pia moyo wangu hufurahia katika maagano ya Bwana aliyoagana na baba zetu” (2 Nefi 11:5).

Rais Russell M. Nelson pia amesisitiza umuhimu wa maagano. Yeye alisema: “Pongezi kubwa ambayo inaweza kupatikana hapa katika maisha haya ni kujulikana kama mshika maagano. Malipo ya mshika maagano yatapatikana hapa na baada ya maisha haya.

Ni ahadi ya kushangaza jinsi gani! Hata baada ya kubatizwa na kufanya maagano ya hekaluni, tunaweza tusitambue jinsi ahadi hizi zinavyoweza kuathiri maisha yetu ya kila siku kuwa bora. Lakini Agano la Kale linatukumbusha hakika inamaanisha nini hasa kuwa “watu wa agano” na jinsi tunavyoweza kuelewa vyema baraka na majukumu yanayo kuja nayo.

Agano kuu lililotajwa katika Agano la Kale ni agano la Ibrahimu. Tunaweza kupata kweli kuhusu injili ya Yesu Kristo katika agano hili, ambalo linatuongoza kwa Yesu Kristo, ambaye ndani yake tunapata wokovu.

Hapa ni baadhi ya njia ambazo Agano la Kale hutusaidia kuelewa vyema na kushika maagano yetu.

Kuelewa Wajibu Wetu katika Agano la Ibrahimu

Agano la Ibrahimu lilikuwa mfululizo wa ahadi na baraka alizopewa Ibrahimu ambazo zinaendelea hadi leo katika “agano jipya na lisilo na mwisho” lililorejeshwa na Nabii Joseph Smith (ona Mafundisho na Maagano 132:30–31). Rais Nelson alifundisha:

“Bwana alitokea katika siku hizi za mwisho ili kufanya upya agano lile la Ibrahimu. Kwa Nabii Joseph Smith, Bwana alitamka:

“‘Ibrahimu alipokea ahadi juu ya uzao wake, na juu ya tunda la viuno vyake—ambako katika viuno vyake ninyi mmetoka, … mtumishi wangu Joseph. …

“‘Ahadi hii ni yenu pia, kwa sababu ninyi ni wa Ibrahimu’ [Mafundisho na Maagano 132:30–31].”

Kupitia agano hili, Bwana aliunda familia ya haki ambayo angeweza kufundisha injili Yake na kuwaleta watoto Wake kwa Yesu Kristo. Mtume Paulo alitufundisha kwamba kama tutakuja kwa Kristo, tunakuwa sehemu ya familia ya Ibrahimu: “Mkiwa wa Kristo, basi ninyi ni uzao wa Ibrahimu, na warithi kulingana na ahadi” (Wagalatia 3:29; ona pia mstari wa 27). Kupitia agano la Ibrahimu, waumini wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho wanakuwa nyumba ya Israeli na warithi kwa baraka za agano la Ibrahimu.

Tunaweza kujifunza kuhusu jukumu letu katika agano kwa kuchunguza maisha ya wale walio katika Agano la Kale, kwa kujifunza ahadi zilizofanywa na Bwana kwa watoto Wake katika amri, na kwa kuwasikiliza manabii wa kale ambao waliwasihi wana wa Israeli watubu na kutii maagano yao.

Kupata Baraka Zilizoahidiwa Kupitia Maagano Yetu

Tunaposoma Agano la Kale, tunaweza kutafuta dalili za Bwana akithibitisha ahadi zilizofanywa katika agano la Ibrahimu. Baraka tatu maarufu zaidi ni nchi, ambayo inaashiria urithi katika ufalme wa Baba wa Mbinguni; uzao, ambao ni ahadi ya ongezeko la milele; na baraka za injili na ukuhani, “ambazo ni baraka za wokovu, hata za uzima wa milele” (Ibrahimu 2:11).

Ibrahimu aliahidiwa kwamba kupitia uzao wake “familia zote za dunia zitabarikiwa” (Mwanzo 12:3). Hii ilimaanisha kwamba Yesu Kristo angekuja ulimwenguni kupitia ukoo wa Ibrahimu na kubariki mataifa yote ya dunia kupitia Upatanisho na Ufufuko Wake (ona Wagalatia 3:16).

kielelezo cha Mwokozi akisali Gethsemane

Maelezo kutoka Gethsemane, na J. Kirk Richards, isinakiliwe

Ni baraka gani unazoziona katika maisha yako kwa sababu ya agano la Ibrahimu?

Kazi ya Kukusanya Israeli

Pamoja na baraka, kuwa sehemu ya agano la Ibrahimu inajumuisha majukumu fulani. Kupitia kujifunza Agano la Kale, tunajifunza jinsi ya kuishi kulingana na maagano yetu. Kama familia ya Ibrahimu, waumini wa Kanisa wanaitwa kukusanya Israeli. Tunaposhiriki katika kazi ya umisionari, utumishi, kazi ya hekaluni, miito ya Kanisa, na kufundisha na kulea familia zetu, tunakusanya Israeli kwa kuwaleta wengine karibu zaidi na Kristo.

Rais Nelson alifundisha, “Wakati wo wote unapofanya kitu cho chote kinachomsaidia mtu ye yote—upande wo wote wa pazia—kupiga hatua kuelekea kufanya maagano na Mungu na kupokea ibada zao muhimu za ubatizo na za hekaluni, unasaidia kukusanya Israeli.”

Kujifunza Kupenda Agano la Kale

Mwaka huu unaposoma Agano la Kale kwa ajili ya kujifunza kwetu kwa Njoo, Unifuate, unaweza kujifunza kupenda mafundisho yake kwa kufuata mfano wa Nefi wa kutafuta dhamira hizi mbili: Kristo na maagano. Kwa kufanya hivyo, unaweza kumwelewa vyema Yesu Kristo, Upatanisho Wake, na injili Yake. Unaweza pia kujifunza zaidi kuhusu “agano jipya na lisilo na mwisho” na jukumu lako ndani yake kama mwanafunzi wa Kristo na kama mshiriki wa nyumba ya Israeli.

Hadithi na mafundisho katika Agano la Kale yanaweza kutusaidia kuzamisha kwa kina uhusiano wetu na Mwokozi na uelewa wetu na kujitolea kwetu kwa maagano yetu wenyewe.

Muhtasari

  1. Russell M. Nelson, “Maagano,” Liahona,, Nov. 2011, 88.

  2. Russell M. Nelson, “Maagano,” 87.

  3. Russell M. Nelson, “Hope of Israel” (worldwide youth devotional, June 3, 2018), HopeofIsrael.ChurchofJesusChrist.org; emphasis in original.