Mkutano Mkuu
Upendo wa Mungu
Mkutano mkuu wa Aprili 2025


10:34

Upendo wa Mungu

Kwa shangwe ninashuhudia kwamba Mwokozi Yesu Kristo ni upendo wa Mungu. Upendo Wake kwetu ni mkamilifu, binafsi na endelevu.

Wakati mmoja wa majira ya kiangazi tukisafiri eneo la nje ya mji, familia yetu ilitumia jioni moja kulala nje chini ya anga safi lisilo na mawingu. Kilichoonekana wazi kabisa juu yetu ulikuwa Mfumo wa Anga, uliojaa nyota zisizo na idadi na kimondo adimu. Wakati tulipostaajabia ukuu wa uumbaji wa Mungu, tulihisi muunganiko wa unyenyekevu Kwake. Watoto wetu wadogo, waliokuwa wamekulia Hong Kong, hawakuwahi kupata uzoefu huu hapo kabla. Bila hatia waliuliza ikiwa tuliishi chini ya anga sawa na lile huko nyumbani kwetu. Nilijaribu kuwafafanulia kwamba ni anga lilelile, lakini uchafuzi wa hewa na mwanga kule tulikoishi ulituzuia kuona nyota hizi japokuwa zilikuwepo.

Maandiko yanatufundisha kwamba “Imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana.” Wakati vivuruga mawazo na matamanio ya kiterestria vinapoweka wingu kwenye uoni wetu wa kiroho, tunapotumia imani kwa Mungu na Mwana Wake Yesu Kristo, tunapata hakikisho la wazi la uhalisia wao na kujali kwao juu yetu.

Katika Kitabu cha Mormoni, nabii Lehi aliona “mti, ambao matunda yake yalitamanika kumfurahisha mwanadamu” na yalikuwa “matamu zaidi ya yote.” Alipolionja tunda, nafsi yake ilijawa shangwe, na alitaka familia yake walionje pia. Tunajifunza kwamba mti huu unawakilisha “upendo wa Mungu,” na kama vile Lehi, sisi pia tunaweza kupokea ushahidi wenye shangwe juu ya Mungu wakati tunapomwalika Yeye ndani ya maisha yetu.

Yesu Kristo ni dhihirisho la upendo wa Baba wa Mbinguni kwetu. Kupitia dhabihu Yake ya kulipia dhambi, alijichukulia juu Yake dhambi zetu na alijeruhiwa kwa makosa yetu. Yeye binafsi amechukua huzuni zetu, amejitwika simanzi zetu, na kujichukulia juu Yake maumivu na magonjwa yetu. Yeye anamtuma Roho Mtakatifu kutufariji, na matunda ya Roho hujumuisha shangwe, amani na imani, ambavyo hutujaza na tumaini na upendo.

Wakati upendo wa Mungu unapatikana kwa wote, wengi wanautafuta bila kuchoka, wakati wengine wanatamani kuhisi upendo wa Mungu lakini hawaamini kwamba wanaustahili. Wengine baadhi wanajaribu kwa juhudi zote kuendelea kuuhisi. Maandiko na nabii wa Bwana hutufundisha kwamba tunaweza daima kuhisi upendo wa Mungu wakati, kupitia neema ya Yesu Kristo, tunapotubu mara kwa mara, tunasamehe kwa dhati, tunajitahidi kutii amri Zake na kuwatumikia wengine pasipo ubinafsi. Tunauhisi upendo wa Mungu pale tunapofanya mambo ambayo yanatusogeza karibu Naye zaidi, kama vile kuzungumza Naye kila siku kupitia sala na usomaji wa maandiko na kuacha kufanya mambo yanayotuweka mbali Naye, kama vile kuwa na kiburi, kubishana na kuasi.

Rais Russell M. Nelson ametualika “tuondoe, kwa msaada wa Mwokozi, uchafu wote wa zamani katika maisha yetu” na “tuweke kando hasira.” Ametuhimiza “tuimarishe misingi yetu ya kiroho” kupitia “kuweka msingi wa maisha yetu juu ya [Mwokozi] na juu ya ibada na maagano ya hekalu Lake.” Ameahidi kwamba “Tunapotii maagano ya hekaluni, tunapata ufikiaji mkubwa wa nguvu ya Bwana ya kuimarisha. … Tunapata uzoefu wa upendo msafi wa Yesu Kristo na Baba yetu wa Mbinguni kwa wingi!”

Ninaye rafiki ambaye alibarikiwa kwa kuwa na familia nzuri na kazi nzuri. Hili lilibadilika wakati ugonjwa ulipomwacha bila uwezo wa kufanya kazi, jambo lililofuatiwa na talaka. Miaka iliyoendelea imekuwa migumu sana, lakini upendo wake kwa watoto wake na maagano aliyoyafanya na Mungu yameendelea kumuimarisha. Siku moja aligundua kwamba mwenza wake wa zamani ameolewa tena na alikuwa ameomba ubatilishaji wa kuunganishwa kwao hekaluni. Alifadhaika na kukanganyikiwa. Alitafuta amani na uelewa katika nyumba ya Bwana. Siku moja baada ya kuzuru huko, nilipokea ujumbe ufuatao kutoka kwake:

“Nilipata uzoefu wa kustaajabisha hekaluni jana usiku. “Nahisi ilikuwa kawaida kwamba bado nilikuwa na chembe ya uchungu. … Nilijua kwamba lazima nibadilike na nimekuwa nikisali wiki nzima ili nibadilike. … Jana usiku ndani ya hekalu nilihisi waziwazi Roho akiondoa uchungu kutoka moyoni mwangu. … Ilikuwa nafuu kubwa iliyoje kuwekwa huru dhidi ya uchungu. … Mzigo wa kutisha wa kimwili ulionilemea umeondolewa.”

Akiwa bado na changamoto zake, rafiki yangu anathamini uzoefu huo ndani ya nyumba ya Bwana ambapo nguvu ya kuweka huru ya upendo wa Mungu imemsaidia kuhisi yu karibu zaidi na Mungu, kuwa zaidi na tumaini kuhusu maisha na kutohofia sana kuhusu siku zake za baadaye.

Tunapopata uzoefu wa upendo wa Mungu, tunaweza kuibeba mizigo yetu kwa urahisi na kunyenyekea kwa furaha na subira kwa mapenzi Yake. Tuna ujasiri kwamba Mungu atakumbuka maagano Yake na sisi, atatutembelea katika mateso yetu na kutukomboa kutoka utumwani. Sisi pia tutatamani kushiriki shangwe tunayoihisi na familia zetu na wapendwa wetu. Kama ilivyokuwa kwa familia ya Lehi, kila mtu ana haki ya kujiamulia kuchagua kula tunda ama la, lakini fursa yetu ni kupenda, kushiriki na kualika katika njia ambayo wale tunaowapenda wanaweza kuhisi upendo wa Mungu.

Ili kuwasaidia wengine kuhisi upendo wa Mungu, tunapaswa kukuza ndani yetu sifa kama za Kristo kama vile unyenyekevu, hisani, huruma na uvumilivu na kusaidia kuwageuza wengine kuelekea kwa Mwokozi kupitia kufuata amri mbili kuu za kumpenda Mungu na kuwapenda wanadamu wenzetu.

Mmoja wa wana wetu alihangaika kujumuika na kuhisi hana thamani wakati wa miaka yake ya ujana. Mimi na mke wangu tulisali kujua jinsi ya kumsaidia na tulikuwa radhi kufanya chochote ambacho Bwana angetutaka tufanye. Siku moja nilihisi msukumo kumuuliza rais wangu wa akidi ya wazee ikiwa alimfahamu mtu yeyote mwenye uhitaji ambaye ningeweza kumtembelea nikiwa na mwanangu. Baada ya mawazo kadhaa, alituomba tumtembelee mwanamke mwenye changamoto za kiafya na kwa ruhusa kutoka kwa rais wa tawi, kumpelekea sakramenti kila wiki. Nilifurahi lakini pia nilikuwa na wasiwasi jinsi ambavyo mwanangu angeitikia ahadi hii ya kila wiki.

Katika matembezi yetu ya kwanza, mioyo yetu iliumia kwa ajili ya mwanamke huyu, kwani alikuwa kwenye maumivu yasiyoisha. Alikuwa na shukrani kwa ajili ya sakramenti, na tulifurahia kumtembelea yeye pamoja na mume wake. Baada ya matembezi kadhaa, Jumapili moja nilikuwa mbali na sikuweza kumsindikiza mwanangu lakini nilimkumbusha juu ya jukumu letu. Nilipofika nyumbani, nilitamani sana kusikia matembezi yalikuwaje. Mwanangu alijibu kwamba hakufikiria kama wana darasa wenzake walipaswa kufanya jambo zuri kama hili. Na alifafanua kwa kusema kwamba alimleta kaka yake asaidiane naye na kwamba sakramenti ilienda vizuri, lakini dada huyu mpendwa alikuwa na huzuni katikati ya wiki kwa sababu aliwaalika marafiki nyumbani kwake kuangalia sinema, lakini kifaa cha kuonesha picha hakikufanya kazi. Mwanangu alisema alitafuta mtandaoni, akapata tatizo na akamsaidia kukitengeneza pale pale. Alihisi kuhitajika, mwenye furaha na kuaminiwa kufanya jambo ambalo lilimfurahisha mwanamke yule. Alihisi upendo wa Mungu kwake.

Ikiwa licha ya juhudi zako, maisha bado ni magumu, ikiwa unahisi kwamba sala zako hazisikiki au ikiwa huwezi kuhisi upendo wa Mungu, tafadhali fahamu kwamba kila juhudi yako ina thamani na, kwa uhakika kama vile nyota angani juu yetu, Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo wanakujua, wanakusikia na wanakupenda.

Katika tukio moja wakati wanafunzi Wake walipokuwa ndani ya mashua “wakisukwasukwa [huku na huko] na mawimbi,” Mwokozi aliwaendea juu ya maji na kuwahakikishia, akisema “Jipeni moyo; ni mimi; msiogope.” Wakati Petro alipotaka kumfuata Mwokozi juu ya maji, Yesu alimwita, akisema, “Njoo.” Na wakati Petro alipopoteza fokasi yake na kuanza kuzama, Mwokozi kwa haraka alinyosha mkono Wake kumshika na kumwongoza kwenye usalama wakati akisema, “Ewe mwenye imani haba, mbona uliona shaka?”

Wakati pepo ziko dhidi yetu katika maisha yetu, je, tuko radhi kuwa wenye furaha na ujasiri? Tunawezaje kukumbuka kwamba Mwokozi hajatutelekeza na kwamba Yeye yu karibu nasi pengine katika njia ambazo hatujazitambua bado? Je, tuko radhi kwenda Kwake katika imani, hususani wakati njia mbele yetu inapoonekana kutowezekana? Na ni kwa njia zipi Yeye anatupeleka kwenye usalama wakati tunapopata misukosuko? Tunawezaje kumtegemea kwa uaminifu katika kila wazo, bila kutia shaka au kuogopa?

Ikiwa ungependa kuhisi upendo wa Mungu kwa wingi zaidi katika maisha yako, ninakualika uzingatie yafuatayo:

  • Kwanza, tulia mara kwa mara ili kukumbuka kwamba wewe ni mtoto wa Mungu na fikiria mambo ambayo una shukrani kwayo.

  • Pili, sali kila siku, ukimwomba Baba wa Mbinguni akusaidie ujue ni nani kando yako anahitaji kuhisi upendo Wake.

  • Tatu, uliza kwa nia ya dhati kile unachoweza kufanya ili kumsaidia mtu huyo ahisi upendo wa Mungu.

  • Na nne, tenda haraka juu ya mwongozo wa kiungu unaoupokea.

Ikiwa daima tunasali na kuuliza kwa niaba ya wengine, Mungu atatuonesha watu tunaoweza kuwasaidia. Na ikiwa tunatenda haraka, tunaweza kuwa njia ambayo kupitia hiyo Yeye anajibu sala zao. Kwa kufanya hivyo, baada ya muda, tutapokea majibu ya sala zetu wenyewe, na tutahisi upendo wa Mungu katika maisha yetu wenyewe.

Mwonekano nje ya dirisha la ndege

Miezi michache iliyopita wakati nikisafiri huko Vietnam, mimi na mke wangu tulikuwa ndani ya ndege iliyopaa katika dhoruba kali. Msukosuko ulikuwa mkali, na mawingu meusi, mvua kubwa na mwanga wa radi ungeweza kuonekana kupitia dirisha letu. Baada ya kupaa muda mrefu kwenye hali tete, ndege yetu hatimaye iliinuka juu ya mawingu ya dhoruba na kutokea kwenye mwonekano huu mtukufu. Tulikumbushwa kwa mara nyingine tena juu ya Baba yetu wa Mbinguni na Yesu Kristo na tulihisi upendo Wao mkuu kwetu.

Marafiki wapendwa, kama mtu ambaye nimepata uzoefu wa upendo wa Mungu, ninashuhudia kwa shangwe kwamba Mwokozi Yesu Kristo ni upendo wa Mungu. Upendo Wake kwetu ni mkamilifu, binafsi na endelevu. Tunapomfuata kwa uaminifu, hebu tujazwe na upendo Wake na tuwe nuru ambayo inawaongoza wengine kwenye upendo Wake. Katika jina la Yesu Kristo, amina.