Mkutano Mkuu
Maandalizi Binafsi Kukutana na Mwokozi
Mkutano mkuu wa Aprili 2025


14:10

Maandalizi Binafsi Kukutana na Mwokozi

Fuata mafundisho ya Mwokozi. Maelekezo Yake wala si ya ajabu au changamano. Tunapoyafuata, hatuhitaji kuogopa au kuwa na wasiwasi.

Wapendwa akina kaka na akina dada, Oktoba iliyopita, Rais Russell M. Nelson alifundisha, “Sasa ni wakati wako na mimi wa kujiandaa kwa ajili ya Ujio wa Pili wa Bwana na Mwokozi wetu, Yesu Kristo.” Wakati Rais Nelson anapozungumza kuhusu Ujio wa Pili, daima ni kwa matumani mema ya shangwe. Hata hivyo, msichana wa Darasa la Watoto hivi karibuni aliniambia kwamba yeye anakuwa na wasiwasi wakati wowote Ujio wa Pili unapotajwa. Alisema, “Ninakuwa na woga kwa sababu vitu vibaya vinatokea kabla Yesu hajaja tena.”

Sio tu watoto ambao wanahisi hivyo. Ushauri bora kwake, kwako na kwangu ni kufuata mafundisho ya Mwokozi. Maelekezo Yake wala si ya ajabu au magumu. Tunapoyafuata, hatuhitaji kuogopa au kuwa na wasiwasi.

Kuelekea mwisho wa huduma Yake ya duniani, Yesu Kristo aliulizwa ni lini Yeye angerudi tena. Katika kujibu, Yeye alifundisha mafumbo matatu, yaliyorekodiwa katika Mathayo 25, kuhusu jinsi ya kujiaanda kukutana Naye—Iwe ni katika Ujio Wake wa Pili au wakati wowote tunapoondoka ulimwenguni humu. Mafundisho haya ni muhimu kwa sababu maandalizi binafsi ya kukutana na Yeye ndiyo kiini cha dhumuni la maisha.

Mwokozi kwanza alisema fumbo la wanawali kumi. Katika fumbo hili, wanawali kumi walienda kwenye karamu ya harusi. Watano kwa busara walileta mafuta ya kujaza taa zao, na watano wapumbavu hawakufanya hivyo. Wakati kuwasili kwa bwana harusi kulipotangazwa, wanawali wapumbavu waliondoka kwenda kununua mafuta. Waliporejea, walikuwa wamechelewa; mlango wa kuingia kwenye karamu ulikuwa umefungwa.

Yesu Kristo alitambulisha vipengele vitatu vya fumbo hili kutusaidia sisi. Yeye alieleza:

“Na siku ile, wakati nitakapokuja katika utukufu wangu, ndipo mfano utakapotimia ambao nilisema kuhusu wanawali kumi.

“Kwani wale walio na hekima na kupokea ukweli, na wamemchukua Roho Mtakatifu kuwa kiongozi wao, na hawajadanganyika—amini ninawaambia … watastahimili siku ile.”

Kwa maneno mengine, hawahitaji kuogopa au kuwa na wasiwasi kwa sababu watanusurika na kustawi. Watashinda.

Ikiwa sisi tuna hekima, tutapokea ukweli kwa kukubali injili ya Yesu Kristo kupitia ibada za ukuhani na maagano. Kisha, tunajitahidi kubaki wenye kustahili kuwa na Roho Mtakatifu daima pamoja nasi. Uwezo huu sharti upatikane kwa kila mtu binafsi, tone kwa tone. Vitendo thabiti, binafsi, vya kiibada humwalika Roho Mtakatifu kutuongoza.

Kipengele cha tatu ambacho Yesu aliangazia ni kuepuka udanganyifu. Mwokozi alionya:

“Angalieni kwamba hakuna mtu atakaye wadanganya.

“Kwa sababu wengi watakuja katika jina langu, wakisema, Mimi ni Kristo—nao watawadanganya wengi.”

Mwokozi alijua wenye kujifanya wangejaribu kuwadanyanya hasa wateule na kwamba wafuasi wengi wangedanganywa. Hatupaswi kuwaamini wale ambao kwa uongo wanadai kibali cha uungu au kutembelea majangwa ya kiistiari au vyumba vya siri ili kufundishwa na vitu bandia.

Kitabu cha Mormoni kinatufundisha jinsi tunavyoweza kutofautisha wadanganyifu na wanafunzi. Wanafunzi daima hukuza kuamini katika Mungu, kumtumikia Yeye na kufanya mema. Hatutadanganywa wakati tunapotafuta na kupata ushauri kutoka kwa watu wanaoamimika ambao wao wenyewe ni wanafunzi waaminifu wa Mwokozi.

Tunaweza pia kuepuka udanganyifu kwa kuabudu kila mara katika hekalu. Hii hutusaidia kudumisha mtazamo wa milele na kutulinda kutokana na ushawishi ambao ungeweza kutuvuruga au kutuchepusha kutoka kwenye njia ya agano.

Somo muhimu la fumbo hili la wanawali kumi ni kwamba tunakuwa na hekima tunapokubali injili, kutafuta kuwa na Roho Mtakatifu kuwa pamoja nasi na kuepuka udanganyifu. Wale wanawali watano wenye hekima hawangeweza kuwasaidia wale ambao hawakuwa na mafuta; hakuna mtu anayeweza kukubali injili, kuwa na Roho Mtakatifu kama kiongozi na kuepuka udanganyifu kwa niaba yetu. Tunapaswa kufanya hivi kwa ajili yetu wenyewe.

Mwokozi kisha alisema fumbo la talanta. Katika fumbo hili, mtu alitoa viwango tofauti vya fedha, vilitajwa kama talanta, kwa watumishi watatu. Kwa mtumishi mmoja alitoa talanta tano, kwa mwingine alitoa talanta mbili, na kwa wa tatu alitoa talanta moja. Baada ya muda, watumishi wawili wa kwanza walizalisha maradufu ya kile walichopokea. Lakini mtumishi wa tatu alizika chini ile talanta yake moja. Kwa watumishi wote wawili ambao walizalisha maradufu talanta zao, yule mtu alisema: “Vema, mtumwa mwema na mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako.”

Yule mtu kisha alimkaripia mtumishi ambaye alikuwa amezika talanta yake kwa kuwa “mtumwa mbaya na mlegevu.” Talanta ya mtumishi huyu ilitwaliwa, na akafukuzwa. Bado, kama mtumishi huyu angelirudufu talanta yake, angepokea sifa na tuzo kama wale watumishi wengine.

Ujumbe mmoja wa fumbo ni kwamba Mungu anatutarajia sisi kutanua uwezo tuliopewa, lakini Yeye hataki sisi tulinganishe uwezo wetu na ule wa wengine. Fikiria umaizi uliotolewa na msomi wa Hasidic karne ya 18, Zusya wa Anipoli. Zusya alikuwa mwalimu maarufu ambaye, alianza kuogopa alipokaribia kifo. Wanafunzi wake waliuliza, “Bwana, mbona unatetemeka? Umeishi maisha mazuri; hakika Mungu atakupa tuzo kubwa.”

Zusya alisema: “Kama Mungu akisema kwangu, ‘Zusya, kwa nini wewe haukuwa Musa mwingine? Nitasema, “Kwa sababu wewe haukunipa ukuu wa nafasi ambayo ulimpa Musa.’ Na kama nikisimama mbele za Mungu na Yeye anasema, ‘Zusya, kwa nini wewe haukuwa Sulemani mwingine? Nitasema, ‘Kwa sababu wewe haukunipa hekima ya Sulemani.’ Lakini, ole, kama nikisimama mbele za Muumba wangu na Yeye aseme, ‘Zusya, kwa nini wewe haukuwa Zusya? Kwa nini wewe haukuwa mtu ambaye nilikupa uwezo wa kuwa? Aa, hii ndiyo sababu ninatetemeka.”

Kwa kweli, Mungu atasikitika kama hatutategemea fadhili, rehema na neema ya Mwokozi ili kutanua uwezo uliotolewa na Mungu tuliopokea. Kwa usaidizi Wake wenye upendo, Yeye anatutarajia kuwa toleo bora la sisi wenyewe. Kwamba tunaweza kuanza kwa uwezo unaotofautiana si kitu Kwake. Na inabidi iwe hivyo kwetu.

Mwishowe, Mwokozi alisema fumbo la kondoo na mbuzi. Wakati Yeye atakaporudi katika utukufu Wake, “na mataifa yote watakusanyika mbele zake; naye atawabagua kama vile mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi; atawaweka kondoo mkono wake wa kuume, na mbuzi mkono wake wa kushoto.”

Wale walio upande Wake wa kulia wakawa warithi katika ufalme Wake, na wale walio upande Wake wa kushoto hawatapokea urithi. Sifa bainifu ilikuwa ni kama wao walimlisha Yeye wakati Yeye alipokuwa na njaa, walimpa Yeye kinywaji wakati Yeye alipokuwa na kiu, walimpa Yeye makazi wakati Yeye alipokuwa mgeni, walimvisha Yeye wakati Yeye alipokuwa uchi na walimtembelea Yeye wakati Yeye alipokuwa mgonjwa au kifungoni.

Kila mtu alikanganywa, wote wale walio mkono wa kulia na wale walio mkono wa kushoto. Waliuliza ni lini walimpa au hawakumpa Yeye chakula, kinywaji, mavazi, au kumsaidia Yeye wakati alipokuwa na uhitaji. Kwa kujibu Mwokozi alisema “Amin, nawaambia kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi.”

Ujumbe wa fumbo ni wazi: tunapowatumikia wengine, tunamtumikia Mungu; tusipofanya hivyo, tunavunja moyo. Yeye anatutarajia sisi kutumia vipawa vyetu, talanta na uwezo kubariki maisha ya watoto wa Baba yetu wa Mbinguni. Msukumo wa kiungu wa kuwatumikia wengine ulionyeshwa katika shairi lilioandikwa katika karne ya 19 na mshairi Mfini Johan Ludvig Runeberg. Mimi pamoja na ndugu zangu tulisikia shairi hili likirudiwa rudiwa “Mkulima Paavo” kote katika utoto wetu. Katika shairi, Paavo alikuwa mkulima masikini ambaye aliishi pamoja na mke wake na watoto katika ukanda wa ziwa katikati ya Finland. Kwa miaka kadhaa mfulululizo, mengi ya mazao yake yaliharibiwa, iwe ni kutokana na uyeyukaji wa theluji ya majira ya kuchipua, dhoruba za majira ya joto, au baridi ya mapema ya majira ya kupukutika majani. Kila wakati mavuno haba yalipopatikana, mke wa mkulima aliomboleza, “Paavo, Paavo, wewe mtu mzee mwenye bahati mbaya, Mungu ametutelekeza.” Paavo, akijibu, kwa ukakamavu alisema, “Changanya maganda na unga wa shayiri utengeneze mkate ili watoto wasiwe na njaa. Nitafanya bidii kukausha maji maji kwenye shamba. Mungu anatujaribu, lakini Yeye atatupatia.”

Kila wakati mimea ilipoharibiwa, Paavo alimwelekeza mke wake kuongeza mara mbili ya kiasi cha maganda ambayo alichanganya na unga ili kuzuia wasife na njaa. Pia alifanya kazi kwa bidii sana, akichimba mitaro ili kutoa maji kutoka kwenye ardhi ili kupunguza uwezekano wa shamba lake kuharibiwa na maji ya majira ya kuchipua na barafu ya majira ya kupukutika majani.

Baada ya miaka ya ugumu, Paavo hatimaye alipata mavuno mengi. Mke wake alishangilia, “Paavo, Paavo hizi ni nyakati za furaha! Ni wakati wa kutupa maganda, na kuoka mkate wa shayiri pekee.” Lakini kwa umakini Paavo aliutwaa mkono wa mke wake na kusema, “Changanya nusu ya unga na maganda, kwani mashamba ya jirani yetu yamefunikwa na barafu.” Paavo alitoa dhabihu mavuno yake na ya familia yake ili kumsaidia jirani masikini aliyekuwa anaangamia.

Somo la fumbo la Mwokozi la kondoo na mbuzi ni kwamba tunapaswa kutumia vipawa vyetu tulivyopewa—muda, talanta na baraka—kuwatumikia watoto wa Baba wa Mbinguni, hasa wale walio hatarini na wenye uhitaji.

Mwaliko wangu kwa yule mtoto wa Darasa la Watoto mwenye wasiwasi niliyemtaja hapo awali, na kwa kila mmoja wenu, ni kumfuata Yesu Kristo na kumtumainia Roho Mtakatifu kama vile ambavyo ungefanya kwa rafiki wa thamani. Wategemee wale ambao wanakupenda na wale wanaompenda Mwokozi. Utafute mwongozo wa Mungu ili kukuza uwezo wako wa kipekee, na wasaidie wengine, hata pale ambapo si rahisi kufanya hivyo. Utakuwa tayari kukutana na Mwokozi, na unaweza kuungana na Rais Nelson katika kuwa mwenye kutumainia mema kwa shangwe. Kwa kufanya hivyo, unasaidia kuutayarisha ulimwengu kwa ajili Ujio wa Pili wa Yesu Kristo, na utabarikiwa kwa tumaini la kutosha kuingia katika pumziko na shangwe ya Bwana, sasa na katika siku zijazo.

Kama tunavyoimba katika moja ya nyimbo zetu mpya:

Furahia! Na jitayarishe kwa ajili ya siku ile! …

Hakuna ajuaye siku na saa wakati Yeye atakapokuja tena,

Lakini Yeye atarudi kama maandiko yasemavyo; itakuwa siku ya shangwe

Wakati Mwokozi wetu mpendwa atakapokuja tena.

Katika jina la Yesu Kristo, amina.

Muhtasari

  1. Russell M. Nelson, “Bwana Yesu Kristo Atakuja Tena,” Liahona, Nov. 2024, 121.

  2. Hatuhitaji kuwa na wasiwasi, kwa sababu Yesu Kristo atatubadilisha sisi ili kwamba tuwe tayari kukutana Naye. Kadri kwa uthabiti tunavyoheshimu maagano yetu na kushika amri, ndivyo pole pole tunakuwa, kupitia neema Yake na baraka Zake, zaidi na zaidi kama Mwokozi. Na tunapofanya hivyo, tutajiandaa kwa ajili ya Ujio Wake wa Pili. Kama ilivyosemwa katika 1 Yohana 3:2–3:

    “Wapenzi, sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa: lakini twajua ya kuwa, atakapodhihirishwa, tutafanana naye; kwa maana tutamwona kama alivyo.

    “Na kila mtu aliye na tumaini hili kwake hujitakasa kama yeye alivyo safi.”

  3. Ujio wa Pili wa Bwana utatokea mwanzoni mwa kipindi cha milenia, wakati Yeye atakaporudi katika utukufu, na wote watakiri kwamba Yeye alikuwa na ni Masiya aliyeahidiwa (ona Isaya 45:23; Zekaria 12:10; Mafundisho na Maagano 88:104).

  4. Ona Russell M. Nelson, “Ujumbe wa Ufunguzi,” Liahona, Mei 2020, 6.

  5. Ona Tafsiri ya Joseph Smith, Mathayo 25:1 (katika Mathayo 25:1, tanbihi a); Mathayo 25:1–4, 6–13.

  6. Mafundisho na Maagano 45:56–57.

  7. Ona David A. Bednar, “Kuongoka kwa Bwana,” Liahona,, Nov. 2012, 109.

  8. Ona 2 Nefi 32:5.

  9. Mathayo 24:4–5.

  10. Ona Joseph Smith—Mathayo 1:5–6, 8–9, 21–22, 25–26.

  11. Ona Moroni 7:13, 15–17. Mafundisho katika Kitabu cha Mormoni yanaunganisha pamoja na kufafanua mafundisho ya biblia “kwa kufadhaisha mafundisho ya uwongo” (2 Nefi 3:12). Pengine hii ni sehemu ya urazini kwa ajili ya ufundishaji wa Rais Russell M. Nelson kwamba “Kitabu cha Mormoni ni chombo cha Mungu cha kuuandaa ulimwengu kwa ajili ya Ujio wa Pili” (“The Book of Mormon, the Gathering of Israel, and the Second Coming,” Liahona, Julai 2014, 27).

  12. Ona Russell M. Nelson, “Fikiria Selestia!,” Liahona, Nov. 2023, 119. Rais Russell M. Nelson alifundisha: “Usichafue [ushuhuda wako] na falsafa za uongo za wanaume na wanawake wasioamini” (Ushinde Ulimwengu na Upate Pumziko,” Liahona, Nov. 2022, 97). “Peleka maswali yako kwa Bwana na kwa vyanzo vingine vya uaminifu. … Sitisha kuongeza mashaka yako kwa kuyafanyia mazoezi pamoja na wenye shaka wengine”( “Kristo Amefufuka; Imani Kwake Itahamisha Milima,,” Liahona, Mei 2021, 103). Kama nabii Alma Mkubwa wa Kitabu cha Mormoni alivyoshauri, “Na msimwamini yeyote kuwa mwalimu wenu wala mhubiri wenu, ila tu awe mtu wa Mungu, anayetembea katika njia zake na kutii amri zake” (Mosia 23:14). Katika kipindi hiki, Mwokozi alitufundisha sisi kuwatengemea tu wale ambao roho zao zimepondeka, … lugha yao ni ya unyenyekevu na yenye kujenga, … [ambao] wanatetemekaye chini ya uwezo wangu, … na, … nao watazaa matunda ya sifa na hekima, sawa sawa na kweli na mafunuo ambayo nimewapa ninyi” (ona Mafundisho na Maagano 52:14–19).

  13. Ona Russell M. Nelson, “Bwana Yesu Kristo Atakuja Tena,” 121.

  14. Wakati ibada za wafu zimefanywa kwa niaba ya mababu wafu, mababu hao wanaamua kwa ajili yao wenyewe kama watakubali injili na kubaki waaminifu au la. Hata katika hali kama hizo, hakuna anayefanya maamuzi kwa ajili ya mwingine.

  15. Ona Mathayo 25:14–30.

  16. Ona Mwongozo wa Maandiko, “Talanta.” Talanta ilikuwa kiasi cha kale cha uzito au thamani ya pesa katika nyakati za Ugriki na Rumi. Ilikadiriwa kwamba talanta moja ilikuwa na thamani ya karibu denari 6,000, na kwa vile denari moja ilikuwa karibu sawa na mshahara wa siku moja kwa mfanyakazi, talanta moja ingekuwa karibu mshahara wa miaka 20 kwa mfanyakazi wa kawaida.

  17. Mathayo 25:21; ona pia mstari wa 23.

  18. Ona Mathayo 25:24–26.

  19. Kutanua fumbo hili, katika hali ya milele ya mambo, mara kila mmoja wa watumishi anapoingia katika shangwe ya bwana wake na kuwa mrithi wa vile vyote bwana alivyonavyo, dhahiri, tofauti ndogo katika kile kila mtumishi alichokuwa nacho hapo mwanzoni huwa na thamani ndogo sana.

  20. Cha ziada, Bwana analinganisha talanta zilizotajwa katika fumbo hili na hali nyingi za maisha na injili, ikijumuisha maarifa na ushuhuda (ona Ether 12:35; Mafundisho na Maagano 60:2, 13) vile vile mali na usimamizi (ona Mafundisho na Maagano 82:18).

  21. Ona Harold S. Kushner, Overcoming Life’s Disappointments (2006), 26.

  22. Kama ilivyoandikwa katika Hubiri Injili Yangu: Mwongozo wa Kushiriki Injili ya Yesu Kristo (2023), 48, “Yote yasiyo haki kuhusu maisha yanaweza kufanywa sawa kupitia Upatanisho wa Yesu Kristo.”

  23. Ona Mathayo 25:31–46.

  24. Mathayo 25:32–33.

  25. Ona Mathayo 25:37–39, 44.

  26. Mathayo 25:40; ona pia mstari wa 45.

  27. Ona Mosia 2:17. Tunashiriki katika misheni ya Mwokozi wakati tunaposhiriki injili Yake, kusaidia kuponya mioyo iliyovunjika (ona Isaya 61:1–3; Luka 4:16–21), kusaidia wanyonge, kuinua mikono iliyolegea, kuimarisha mogoti dhaifu (ona Mafundisho na Maagano 81:5).

  28. Sehemu ya ndani ya ganda kutoka kwenye mti wa mbetula ina baadhi ya kabohaidreti na nyuzi. Inaweza kuliwa kama hakuna chochote kingine.

  29. Ona Johan Ludvig Runeberg, “Högt Bland Saarijärvis Moar,” Idyll och epigram Dikter (1830), nummer 25; Suomen kansalliskirjallisuus (Helsinki, 1941), 9:50–52; sv.wikisource.org/wiki/Högt_bland_Saarijärvis_moar. Tafsiri ya Kiswidi ni yangu.

  30. Hii inawasilisha kile Mungu alichoelekeza kwa Israeli ya kale kufanya: “Kwa maana masikini hawatakoma katika nchi; kwa hiyo ninakuamuru na kukuambia, Mfumbulie kikweli mkono wako nduguyo, kwa masikini wako, na mhitaji wako” (Kumbukumbu la Torati 15:11).

  31. Ona Dallin H. Oaks, “Preparation for the Second Coming,” Liahona, May 2004, for a wonderful discourse about the Second Coming and ways to prepare for it.

  32. Ona Russell M. Nelson, “Ushinde Ulimwengu na Upate Pumziko,” 95–98. Rais Nelson alifundisha, “Kipengele kimoja muhimu katika ukusanyaji huu ni kuwaandaa watu ambao wanaweza, wako tayari, na wanastahili kumpokea Bwana wakati Yeye anapokuja tena, watu ambao tayari wamemchagua Yesu Kristo dhidi ya ulimwengu ulioanguka; watu ambao wanashangilia haki yao ya kujiamulia ili kuishi sheria za juu zaidi na takatifu zaidi za Yesu Kristo.”(“Ushinde Ulimwengu na Upate Pumziko,” 98).

  33. Ona Moroni 7:3. Rais Joseph F. Smith alifundisha: “Pumziko … lililorejelewa siyo pumziko la kimwili. … [Ni} pumziko la kiroho na amani ambayo huzaliwa kutokana na kusadiki kulikoamuliwa juu ya ukweli. … Tunaweza basi kuingia katika pumziko la Bwana leo, kwa kufikia uelewa wa kweli za injili. … [Wale walioingia katika pumziko hili ni wale] ambao akili zao zimeridhika, na wale ambao wamekaza macho yao juu ya alama ya wito wao wa juu kwa azimio lisiloonekana katika mioyo kuwa thabiti katika kweli, na wale ambao hukanyaga kwa unyenyekevu na haki njia iliyotiwa alama kwa jili ya … wafuasi wa Yesu Kristo. Lakini kuna wengi ambao, hawajafikia hali hii ya kusadiki kwa dhati, wanapelekwa huko na kule na kila upepo wa mafundisho, basi wasiweze kutulia, wanafadhaika, wakisukwasukwa huku na kule. Hawa ndiyo wale ambao wanavunjika moyo kwa sababu ya mambo yanayotokea Kanisani, na katika taifa, na katika vurugu za wanadamu. … Wanahifadhi hisia za shaka, vurugu, kutokuwa na uhakika. Mawazo yao yamevurugwa, na wanakuwa na furaha kwa badiliko dogo sana, kama mtu baharini ambaye amepoteza mwelekeo wake” (Gospel Doctrine, 5th ed. [1939], 126).

  34. “When the Savior Comes Again,” Hymns—For Home and Church, Gospel Library.