12.
Yesu Kristo huleta shangwe
Baba yako wa Mbinguni ni mwenye shangwe. Anakutaka wewe, mtoto Wake, uwe na shangwe tele iwezekanavyo. Hii ndio sababu Alitayarisha mpango wa furaha. Alimtuma Mwanawe, Yesu Kristo, kuwa Mwokozi wako na kufundisha injili Yake. Neno injili linamaanisha “habari njema,” na habari njema ni kwamba kwa sababu ya Yesu Kristo, unaweza kuwa na furaha katika maisha haya na utimilifu wa shangwe milele.
Kweli za Milele
Umekusudiwa kuwa na furaha na shangwe. Hilo ndilo kusudi la maisha yako. Ni kusudi la mpango wa furaha wa Baba wa Mbinguni. Hii haimaanishi kwamba kamwe hutahuzunika au kuwa na nyakati ngumu. Lakini inamaanisha kwamba Mwokozi anaweza kukusaidia kuvuka nyakati ngumu na kupata shangwe.
Shangwe haitoki katika hali zako; huja kutokana na kumfuata Yesu Kristo. Unaweza kuwa na siku mbaya, wiki mbaya, au mwaka mbaya. Lakini shangwe siyo kukosekana kwa huzuni katika maisha yako; ni uwepo wa Kristo katika maisha yako.
Shangwe ya Mwokozi ni kubwa na ya kudumu zaidi kuliko kitu kingine chochote. Shetani atakushawishi kutafuta burudani na kuridhika katika njia za ubinafsi au kutokana na anasa za kidunia. Chochote kilicho kinyume na Yesu Kristo na amri Zake hakiwezi kukuletea shangwe na furaha ya kweli, na ya kudumu. Kumbuka kwamba vitu vya dunia hii ni vya muda. Injili ya Yesu Kristo hutoa shangwe na furaha ambayo ni ya kina, takatifu, na ya kudumu milele.
Mialiko
Chagua shangwe. Ingawa ni kweli kwamba kuna huzuni na ugumu katika ulimwengu huu, Baba wa Mbinguni pia ameujaza ulimwengu kwa mambo mengi mazuri, vitu vya kuburudisha. Vitafute. Jaribu kutambua sababu za kufurahi kila siku—labda hata kuziandika. Hizi ni zawadi kutoka kwa Baba yako wa Mbinguni mwenye upendo.
Leta shangwe na furaha kwa wengine. Yesu Kristo alipata utimilifu wa shangwe katika kutuletea shangwe. Unaweza kufuata mfano Wake kwa kupata shangwe na furaha katika kuwatumikia wengine. Msaidie mtu kuhisi anapendwa. Toa pongezi ya dhati. Mtie moyo mtu ambaye anapambana. Kama umewahi kuhisi unahitaji shangwe zaidi katika maisha yako, jaribu kuleta shangwe kwa mtu mwingine.
Kuwa mwenye shangwe katika kumwabudu Bwana. Unapokwenda kanisani, fokasi kwenye shangwe ambayo Yesu Kristo anakupatia, na msifu Yeye kwa hilo! Fanya sehemu yako kwa kuchangia kwenye roho ya shangwe katika mikutano yako ya Kanisa. Fanya muziki mtakatifu kuwa sehemu ya kuabudu kwako nyumbani na kanisani.
Baraka Zilizoahidiwa
Unaweza kuhisi shangwe hata kama maisha ni magumu. Unaweza kujiuliza hii inawezekanaje, lakini ni kweli. Imani yako katika Yesu Kristo, nguvu Yake ya uponyaji, na ahadi Zake za milele zinaweza kukupa shangwe endelevu. Shangwe yake hufunika huzuni na kuleta amani ambayo hupita uelewa wote.
Utimilifu wa shangwe unakungoja katika ufalme wa Mungu wa selestia. Yesu Kristo alishinda vitu vyote ambavyo vingeweza kukuzuia kupokea shangwe ya milele. Unapomtumaini Yeye na kumfuata Yeye, shangwe hii itakuwa yako.
Maswali na Majibu
Kama injili ni yenye shangwe, kwa nini ninajisikia huzuni sana? Kujisikia huzuni siyo ishara kwamba hauishi injili. Maisha ya kila mtu yanajumuisha dhiki, majaribu, na huzuni. Kumfuata Yesu Kristo hakubadilishi hili, lakini kunakuunganisha na Mwokozi ambaye anaweza kukufariji na kukusaidia kupata shangwe na furaha.
Kwa nini kuna mateso mengi sana ulimwenguni? Baadhi ya mateso ulimwenguni huja kwa sababu watu hutumia haki yao ya kujiamulia kufanya chaguzi mbaya. Hii inaweza kusababisha mateso kwa ajili yao wenyewe na kwa watu wengine. Katika visa vingine, mateso si kosa la mtu—ni matokeo tu ya kuishi katika ulimwengu usio mkamilifu. Kwa sababu iwayo yoyote ile, inaweza kuwa yenye kuvunja moyo kumwona mtu akiteseka, hasa mtu unayempenda. Kuwa na uhakika kwamba Mungu pia ana huzuni wewe unapoteseka. Anaruhusu majaribu ya maisha ya duniani yakusaidie kukua na kujiandaa kwa furaha ya milele pamoja Naye, lakini yeye hakuachi kuteseka peke yako. Alimtuma Yesu Kristo kujichukulia juu Yake maumivu yako ili aweze kukusaidia. Yesu Kristo ni nguvu yako! Na Yeye anakualika, kama mmoja wa wafuasi Wake, kufanya kile unachoweza ili kusaidia kupunguza mateso ya wengine.
Ona Zaburi 16:11 (katika uwepo wa Mungu ni utimilifu wa shangwe); 95:1 (imba kwa Bwana); Yohana 16:33 (jipeni moyo; Yesu Kristo aliushinda ulimwengu); Wagalatia 5:22 (tunda la Roho ni furaha); Waebrania 12:2 (Yesu alivumilia mateso Yake kwa sababu ya furaha ya kuwaokoa watoto wa Mungu); 2 Nefi 2:25 (Mungu anataka uwe na shangwe); Alma 26:15–16 (kufanya kazi ya Mungu huongoza kwenye shangwe); Mafundisho na Maagano 18:15–16 (itakuwa shangwe kubwa kiasi gani kwako wakati unapowasaidia wengine kuja kwa Kristo).
Maswali ya Kibali cha Hekaluni
-
Je, una ushuhuda juu ya Upatanisho wa Yesu Kristo na wa jukumu Lake kama Mwokozi na Mkombozi wako?