“Ninajisikia Amani Moyoni Mwangu,” Liahona, Julai 2025.
Picha za Imani
Ninajisikia Amani Moyoni Mwangu
Kama mwanafunzi wa uuguzi, nilihisi kwamba sikuwa na muda kwa ajili ya wito wangu kanisani na masomo yangu. Lakini nilikuwa nimejifunza katika ujana wangu kwamba huduma na utiifu kwa amri za Mungu huongoza kwenye maisha ya furaha.
Picha na Christina Smith
Mwanzoni mwa ujana wangu, nilifikiria kuhusu kujitenga na Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho. Lakini wakati huo huo, niligundua kuwa sikuwa nikifuata mafundisho yote ya Kanisa. Niliamua kwamba kama nitakwenda kujitenga na Kanisa, nilitaka kujisikia vizuri kuhusu hilo.
Kwa hiyo, niliamua ningejaribu kutii kila kitu ambacho injili inafundisha. Kisha, kama nitajisikia ndani yangu kwamba mafundisho hayakuwa na maana, ningeweza kuondoka bila majuto yo yote.
Kwa “uwezo, akili na nguvu zangu zote” (Mafundisho na Maagano 4:2), nilijaribu kutii kile Bwana anachofundisha na kuangalia kile kitakachotokea. Kupitia uzoefu huo, nilipewa kipindi cha furaha kwa kiasi ambacho nilikuwa sijawahi kuona kabla ya kupitia uzoefu huo. Kwa kubaki Kanisani, nilihisi kwamba ningeweza kuishi maisha ya furaha, nikijua furaha ya kweli ni nini.
Baada ya uzoefu huo, niliamua kwenda misheni na kushiriki amani niliyojisikia moyoni mwangu. Bila kujali majaribu ambayo ningekabiliana nayo, nilikuwa nimejifunza kwamba kama nikiomba kwa Mungu, Yeye atanisaidia, atanipa matumaini, na kunisaidia kuelewa sababu ya matatizo yangu.
Je, Napaswa kufanya nini?
Baada ya misheni yangu, nilipokuwa nikijifunza kuwa muuguzi, nilitumia muda mwingi kila siku kufanya mafunzo kazini. Baadaye, ningefanya kazi za nyumbani hadi saa 8:00 au 9:00 alfajiri. Kisha ningelala kidogo kabla ya kufanya mafunzo-kazini zaidi siku inayofuata.
Wakati huo, nilikuwa nikihudumu kama rais wa Wavulana katika kata. Ilikuwa vigumu sana kwangu kujifunza na kutimiza wito wangu wa Kanisa. Nilijua kama ningeacha wito wangu, hata hivyo, nisingeweza kuwafundisha wavulana kuhusu umuhimu wa kufuata njia ya Mungu au kupokea baraka Yeye alizokuwa ameziweka kwa ajili yangu.
“Je, napaswa kufanya nini?” Nilimwuliza Baba wa Mbinguni. “Mwili na akili yangu iko katika hali ya vurumai, na sidhani kama ninafanya aina ya kazi ambayo Wewe ungependa nifanye.”
Baada ya sala yangu, nilipata faraja. Nilihisi kwamba Mungu alikuwa ananiambia, “Wakati huu unaotumia kufanya kazi kwa bidii ni muhimu kwako. Ratiba yako yenye shughuli nyingi inaweza kuwa ngumu, lakini kama utashinda jaribu hili sasa, nitakutumia kubariki na kuwasaidia wengine wengi katika siku zijazo.”
Jibu hili lilinipa hakikisho kwamba nilikuwa na kusudi, kwamba kama ningevumilia, ningeweza kufanya kazi maalum katika siku zijazo.
Nilikiri kwa wavulana jinsi gani shule ilivyokuwa ngumu kwangu. Lakini pia niliwaambia kwamba Kanisa na injili ni muhimu na inapaswa kuwa kitovu cha maisha yetu hata katikati ya matatizo. Nilionyesha upendo wangu kwao na kuwaambia nilikuwa nikijaribu kwa bidii kutimiza wito wangu kwa sababu ilikuwa muhimu kwangu kama iliivyo kwa masomo yangu. Walimwaga machozi wakati ukweli wa mambo haya ulipogusa mioyo yao.
Kubarikiwa kwa Kuhudumu
Nilipoendelea kuwahudumia wavulana na kuwafundisha injili, niliwaza sana kuhusu hisia zao ngumu za ujana wanapohudhuria kanisani na kujifunza injili. Nilifokasi kwenye afya yao ya akili na kuwasaidia katika mahitaji yao binafsi.
Kuwahudumia wavulana kulinisaidia kukuza uwezo wa kuangalia na kuona mabadiliko madogo kwa watu. Sasa kwa kuwa ninafanya kazi kama muuguzi na kutunza dazeni za wagonjwa, nimeinua uwezo huo wakati wa kuchangamana na wengine.
“Mgonjwa huyo anasema kweli unaelewa hisia zake,” wafanyakazi wenzangu wananiambia. Au mgonjwa anaweza kusema, “Naona kwamba wewe ni rahisi kuzungumza nawe.”
Kuhudumu katika miito ya Kanisa kumenibariki mimi nyumbani pia. Nimejifunza kumpa kipaumbele mke wangu nilipojifunza kutokuwa mchoyo.
“Kama ningekuwa Baba wa Mbinguni,” ninajiuliza mwenyewe, “Yeye angeendeleaje kuiimarisha familia hii, na ninapaswa kufanya nini ili kufanikisha hilo?”
Kwa sababu nimejifunza injili kwa moyo wangu wote, ninajua jinsi na kwa nini kuwafundisha watoto wangu kwamba Kanisa ni muhimu. Mimi na mke wangu tunajua jinsi ya kurutubisha familia yetu kiroho kwa sababu tunaweka msingi wa mafundisho yetu juu ya mafundisho ya Mwokozi.
Ninahisi matumaini na amani moyoni mwangu kwa kufuata mafundisho ya Bwana na kusikiliza ushawishi Wake. Yeye amekuwa kando yangu njia nzima, akinibariki kupitia utiifu wangu na miito ya kuwabariki na kuwasaidia wengine. Bila kujali majaribu, ninataka kuishi maisha yangu kwa njia ambayo ninaweza kufanya kile Yesu Kristo anatamani (ona 2 Nefi 32:3).