“Kujali: Mpango wa Ulimwengu wa Kuboresha Ustawi wa Wanawake na Watoto,” Liahona, Agosti. 2025.
Wanawake wa Agano
Kujali: Mpango wa Kimataifa wa Kuboresha Ustawi wa Wanawake na Watoto
Tunaleta upendo na faraja ya Yesu Kristo ulimwenguni kote tunapowatunza wale walio katika nyumba zetu, ujirani na jumuiya zetu wenyewe.
Kazi yenye mwongozo wa kiungu ya Muungano wa Usaidizi imekuwa na mizizi iliyozamishwa kwa kina katika kazi ya kibinadamu na kuwatunza wale walio na uhitaji tangu mwanzo wake mtakatifu mnamo 1842. Katika karne ya 20, akina dada wa Muungano wa Usaidizi walituma nafaka waliyokuwa wameihifadhi ili kusaidia kuwalisha wale walioathirika na majanga ya asili na njaa. Walianzisha hospitali, waliwasaidia wanawake kuhudhuria shule ya tiba, na wanawake waliofundishwa uuguzi na ukunga, kwa kiasi kikubwa kuboresha viwango vya vifo vya akina mama na watoto wachanga. Pia walikuza elimu kwa kuanzisha mashule na programu za kusoma na kuandika.
Leo, takribani akina dada milioni nane wa Muungano wa Usaidizi ulimwenguni kote wanabakia na msimamo wa kuwajali wale wenye uhitaji. Muungano wa Usaidizi unasaidia uzoefu kwa wanawake kuleta na kupokea faraja ya Mwokozi—kimwili na kiroho—kwa watoto wote wa Mungu. Wakati akina dada wanapotoa na kupokea faraja ya Mwokozi, wanakuwa zaidi kama Yeye, wanahisi upendo Wake, na wanatamani uhusiano wa kina, wa agano na Yeye.
Mpango wa Kanisa wa ulimwenguni kote wa kuboresha ustawi wa wanawake na watoto ni uzoefu—fursa ya kuleta faraja ya kimwili na kiroho kwa watoto wote wa Mungu. Tunafanya hivyo kwa Roho Yake, mamlaka Yake ya ukuhani yaliyonaibishwa, na nguvu Zake, ambazo tunazipokea kwa kushika maagano yetu na Yeye.
Kwa mradi huu tunatafuta kuleta matokeo makubwa iwezekanavyo katika kubariki maisha ya wanawake na watoto kupitia maeneo haya manne ya fokasi:
-
Lishe ya mtoto
-
Matunzo ya mama na mtoto mchanga
-
Chanjo
-
Elimu
Kwa nini tunafokasi nguvu zetu, mioyo, na rasilimali kwenye mpango wa kimataifa wa kuboresha ustawi wa wanawake na watoto? Kwa sababu tunaamini kwamba maendeleo ya ulimwengu huanza na wanawake na watoto. Rais Johnson anafundisha: “Unapombariki mwanamke, unabariki familia, jamii, taifa. Unapombariki mtoto, unawekeza katika siku za usoni.”
Kama sehemu ya mpango wa kimataifa, Urais wa Kwanza uliidhinisha mpango unaoongozwa na Kanisa wa dola milioni 55.8 kuharakisha uboreshaji wa lishe na huduma za afya katika nchi 12 zenye mahitaji makubwa. Kwa kushirikiana na mashirika makuu manane yasiyo ya kiserikali, Kanisa lilisaidia programu ambazo zilisaidia afya na ustawi wa zaidi ya watoto milioni 14 na kina mama wajawazito mnamo mwaka 2024.
Rais Camille N. Johnson akimtembelea mama wa watoto watatu katika hafla ya mchango wa chakula huko Costa Rica. “Alikuwa na shukrani sana kwa mlo kwa ajili ya watoto wake wenye njaa,” anasema Rais Johnson. “Nilimwambia nilimpenda na, muhimu zaidi, kwamba Mungu alimpenda.”
Sehemu ya Jambo Muhimu
Wakati mimi (Rais Johnson) niliposafiri kwenda Costa Rica mwaka jana, nilipata fursa ya kusaidia kwenye hafla ya mchango wa chakula. Niliguswa kukutana na wanawake wengi na watoto waliokuja kupokea chakula chenye afya. Nilipata msukumo wa kipekee kwamba tulikuwa tukifanya kile ambacho Mwokozi angetaka tufanye. Nilikutana na Yumana na watoto wake watatu warembo. Mwanamke huyu wa dhati alikuwa akiuza maua ya utepe aliyokuwa ametengeneza ili kukimu familia yake. Alikuwa na shukrani sana kwa chakula kwa ajili ya watoto wake wenye njaa. Nilimwambia nilimpenda na, muhimu zaidi, kwamba Mungu alimpenda. Yumana alipokea faraja ya kimwili na faraja ya kiroho alipohisi na kutambua upendo wa Mungu.
Tunaona mpango huu wa ulimwengu kama sehemu ya kazi ya wokovu na kuinuliwa. Watu wanapopokea faraja ya kimwili, tunatumaini na kutarajia watahisi upendo wa Bwana kwao na hamu ya kuingia au kuimarisha uhusiano wa agano na Yeye.
Juhudi za kuboresha afya na ustawi wa wanawake na watoto zinatimiza jukumu takatifu la kuwajali wale walio katika shida. Bado mpango huu hubariki watu kwa njia zingine:
-
Unaongeza uwezo wa kiakili na kimwili wa kizazi kinachoinukia, kuwasaidia pia kufikia uwezekano wao wa kiroho.
-
Unawafikia majirani na marafiki zetu, wengi wao ambao pia wanataka kujifunza jinsi ya kuwasaidia watoto wao wenyewe.
-
Unatoa kiini cha injili ambacho kinakuza huduma yenye maana na fursa za kuhudumu kwa wanawake, hasa wasichana wakubwa.
Kizazi cha sasa cha vijana wakubwa kinataka kuwa sehemu ya kusudi muhimu, sababu ambayo inaleta athari halisi na tofauti katika ulimwengu. Tunatumaini mpango huu wa ulimwengu utawasaidia dada zetu kuona kwamba tayari wao ni sehemu ya sababu kuu duniani: shirika takatifu la Bwana kwa wanawake katika Kanisa Lake lililorejeshwa, Muungano wa Usaidizi.
Tunaamini juhudi hii ya ulimwengu itawapa msukumo waumini na marafiki zetu kuhudumu katika jamii zao. Tunatumaini wataona kwamba:
-
Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho linatanguliza masuala ambayo yanaathiri wanawake na watoto na kujitolea rasilimali ili kuboresha afya zao na ustawi wao.
-
Kanisa na Muungano wake wa Usaidizi ni viongozi wa ulimwengu katika kushughulikia masuala ya kibinadamu.
-
Muungano wa Usaidizi unaongozwa na wanawake ambao wanaboresha maisha ya watu binafsi, familia na jamii.
Huu ni mwanzo tu wa kitu kisicho cha kawaida ambacho kitabariki maisha ya wengi ambao watatoa na kupokea msaada wa Mwokozi leo, na katika miaka ijayo, wakati mpango huu wa ulimwengu ukiendelea.
Mtaalamu wa matibabu anamchunguza mtoto huko Ufilipino. Lishe ya watoto ni mojawapo ya maeneo manne ya kufokasi kwa juhudi za Kanisa katika kuboresha ustawi wa wanawake na watoto.
Ndani ya maeneo yetu ya Ushawishi
Kwa kiwango cha ulimwengu, Kanisa ulimwenguni kote linamwakilisha kila mmoja wetu kama waumini katika kuleta pamoja mashirika ambayo ni wataalamu katika kushughulikia masuala makubwa katika maeneo ya mbali. Bado, labda ufikiaji bora wa kibinadamu unafanywa karibu na nyumbani unapovuka uzio wa nyumba yako au mtaani kwako. Mnaishi maagano yenu na mnashiriki katika kusudi letu la ulimwengu wakati mnapotenda kwa huruma kama ya Kristo na kwa upendo kuwajali wale walio katika familia zenu, ujirani na jamii zenu wenyewe.
Huenda usiweze kurekebisha paa la jirani au kusafiri kwenda nchi tofauti kusafisha nyumba za watu baada ya janga la kimbunga, lakini je, ungeweza kumsomea mtoto, kumsikiliza rafiki ambaye anahangaika au kutoa mchango wa matoleo ya mfungo? Kila juhudi ni ya thamani na muhimu katika kazi hii ya kuwajali wale walio katika shida. Asante kwa kuwa mfereji ambao wengine wanaweza kupokea faraja ya Mwokozi kwa kuwa mikono Yake ya upole, miguu Yake mizuri, masikio Yake ya kusikiliza, midomo Yake yenye ukarimu.
Kanisa linapoleta mashirika pamoja kushirikiana kwa ajili ya afya na ustawi wa wanawake na watoto katika nchi mbalimbali, kina dada wa Muungano wa Usaidizi huleta watu pamoja kutatua changamoto katika jamii zao wenyewe. Wanawake wa Muungano wa Usaidizi wanatambua uhitaji, hukusanya nyenzo na kusaidia kutatua changamoto. Na tunafanya hivyo kwa msaada wa Roho, kuleta upendo na faraja ya Yesu Kristo kwa watoto wote wa Mungu.
Kuona mahitaji ya wahamiaji huko Milan, Italia, kina dada wa Muungano wa Usaidizi waliandaa fursa ya huduma ya kuwapa mavazi na vyombo vya nyumbani. Baadhi ya akina dada walitoa mchango wa vitu vilivyotumika kwa ukunjufu wa moyo, wakati wengine walipanga na kusafisha vitu vilivyochangwa. Matoleo ya kila dada yalikuwa muhimu. Akina dada wa Muungano wa Usaidizi waliwasaidia wageni kuhisi upendo wa Yesu Kristo walipokuja kwenye kituo cha mchango. Monia, dada wa Muungano wa Usaidizi, alisema, “Kutokana na mambo madogo huja mambo makubwa. Na tunaweza kuwabariki watu ndani na nje ya Kanisa. Ni injili katika matendo.”
Akizungumza na Muungano wa Usaidizi uliokuwa umeanzishwa, Nabii Joseph Smith aliwaambia akina dada, “Sasa mmewekwa katika hali ambayo kwayo mnaweza kutenda kulingana na huruma hizo ambazo Mungu ameziweka vifuani mwenu.”
Akiwa Guadalajara, Mexico, Dada Yee alijifunza kuhusu na kuona mifano mingi ya ajabu ya kina dada wakitenda kulingana na huruma hizo walipotafuta kukidhi mahitaji ya eneo hilo.
Mmoja wa dada kama huyo alikuwa Dada Pulido, ambaye aliona hitaji katika hospitali ya eneo lile la kusaidia familia na watu ambao walitoka mbali na walihitaji chakula na nguo wakati wakisubiri kupata matibabu. Aliwakusanya akina dada 120 wa Muungano wa Usaidizi, wamisionari kadhaa na wengine katika jamii kutafuta michango ya chakula, maji, mablanketi na nguo. Takribani watu 1,500 walichangia bidhaa, na kina dada na wengine waliandaa chakula cha mchana na chakula kwa takribani watu 1,200. Bidhaa hizo zilitolewa kwa wale waliokuwa wakisubiri zamu yao ya matibabu hospitalini.
Dada huyu alisema alikuwa anafanya hivi kwa sababu alikuwa na huruma kwa watu hawa. Akiwa na machozi machoni mwake, alieleza kwa unyenyekevu kwamba alikuwa mmoja wa watu hao wanaosubiri hospitalini wakati mumewe alipokuja na kwenda kwa matibabu ya saratani. Alisema baraka yake kuu na hamu yake ni kuhudumu kama ambavyo Mwokozi angehudumu.
Kuleta Usaidizi wa Mwokozi
Akina dada, tumeaminiwa na kazi takatifu ya kuleta faraja ya Mwokozi—kimwili na kiroho—kwa ulimwengu wote. Na tunaweza kufanya hivyo kwa kuwahudumia wale walio katika maeneo yetu wenyewe ya ushawishi. Ni zawadi na baraka iliyoje. Kushiriki katika mradi huu wa ulimwenguni kote wa kuboresha ustawi wa wanawake na watoto ni mojawapo ya matukio mengi ambayo hutuleta karibu zaidi na Mwokozi. Tukitenda kama ambavyo Yeye angefanya, tunahisi upendo Wake; na hamu yetu, na kujitolea kwetu, kwenye uhusiano wa agano pamoja naye unaongezeka.
Asante kwa kutusaidia kuleta upendo na faraja ya Yesu Kristo kwa dada na kaka zetu kila mahali.
Katika kujaribu kumuiga Yesu Kristo, mahitaji muhimu zaidi kwetu kama wanafunzi Wake ni kutambua mahitaji ya haraka ya mtu binafsi karibu nasi na kujibu kwa subira na upendo.
Rais Russell M. Nelson alituambia katika Ibada ya Muungano wa Usaidizi duniani kote ya 2024, “Ninawabariki mtambue kwamba vipawa vyenu vya kiungu kama binti wa Mungu vinakupa nguvu siyo tu ya kubadilisha maisha bali kubadili ulimwengu!”
Hiyo ndilo jukumu letu kuu!
Ni kipindi kitukufu kuwa wanawake wa agano na washiriki wa jamii ambayo huleta faraja ya Mwokozi—kimwili na kiroho—kwa dada zetu na kaka zetu ulimwenguni kote. Lengo kuu katika kutoa msaada na kujitegemea ni kuandaa njia kwa ajili ya dada na kaka zetu kutamani na kupokea upendo na rehema inayopatikana kwa wale wanaofanya na kushika maagano na Mungu.
Tunatoa ushuhuda wetu kwamba Yesu Kristo ni faraja na kwamba faraja ambayo Yeye hutoa ni ya milele.