“Mei 25–31. ‘Bwana Akawainulia Mwokozi: Waamuzi 2–4; 6–8; 13–16,” Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Nyumbani na Kanisani: Agano la Kale 2026 (2026)
“Mei 25–31. ‘Bwana Akawainulia Mwokozi,’” Njoo, Unifuate: Agano la Kale 2026
“Hakika Nitakwenda pamoja nawe”—Debora Nabii Mke, na Des Leavitt
Mei 25–31: “Bwana Akawainulia Mwokozi”
Waamuzi 2–4; 6–8; 13–16
Wote tunajua kutenda dhambi ni nini, kuhisi vibaya kuihusu, na kisha kutubu na kuamua kubadilisha njia zetu. Lakini mara nyingi tunasahau azimio letu la awali, na, wakati majaribu yanapokuja, tunajikuta tunatenda dhambi hiyo hiyo. Mpangilio huu unaonekana mara kwa mara katika kitabu cha Waamuzi. Wakishawishiwa na imani na matendo ya kuabudu ya Wakanaani—ambao walipaswa kuwafurusha kutoka kwenye nchi—Waisraeli walivunja maagano yao na Bwana na kugeukia mbali na kuacha kumwabudu Yeye. Matokeo yake, walipoteza ulinzi Wake na kuangukia utumwani. Na bado kila mara jambo hili lilipotokea, Bwana aliwapa watu Wake wa agano nafasi ya kutubu na kuwainulia mwokozi, kiongozi wa kijeshi aliyeitwa “mwamuzi.” Si waamuzi wote katika kitabu cha Waamuzi walikuwa waadilifu, ila baadhi yao walikuwa na imani kuu katika kuwaokoa wana wa Israeli na kuwarejesha katika uhusiano wao wa kiagano na Bwana. Hadithi hizi zinatukumbusha kwamba pasipo kujali cho chote kilichotupeleka mbali kutoka kwa Yesu Kristo, Yeye ni Mkombozi wa Israeli na daima yupo tayari kutukomboa sisi na kutukaribisha tena Kwake.
Kwa ajili ya muhtasari wa kitabu cha Waamuzi, ona “Waamuzi, kitabu cha” katika Kamusi ya Biblia.
Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Nyumbani na Kanisani
Waamuzi 2:1–19; 3:5–12
Bwana hunisamehe mara kwa mara kadiri ninavyotubu
Kitabu cha Waamuzi kinaweza kuwa vyote onyo na himizo. Tafuta onyo hili na himizo unaposoma Waamuzi 2:1–19; 3:5–12. Ni kwa jinsi gani kuonywana kuhimizwa kunatumika kwako?
Kwa mfano, kama Waamuzi 2:19 ilikuwa juu yako na majaribu yako badala ya kuwahusu Waisraeli wa kale, ingeweza kusema nini? Kama Waamuzi 3:9 ilikuwa kuhusu kile Bwana alikuwa amefanya ili kukukomboa, ingeweza kusema nini?
Fikiria kusoma swali na jibu kwenye ukurasa wa 9 wa Kwa Ajili ya Nguvu kwa Vijana: Mwongozo wa Kufanya Chaguzi. Unahisi hii inatumika vipi kwa uzoefu wa Waisraeli katika kitabu cha Waamuzi? Hili linakufundisha nini wewe kuhusu Yesu Kristo?
Waamuzi 4:1–15
Ninaweza kuwashawishi wengine kuwa na imani katika Bwana.
Wakati mwingine imani ya mtu mmoja inaweza kuchochea imani katika wengine wengi. Katika Waamuzi 4, mtu huyo mmoja alikuwa Debora. Soma kumhusu yeye katika Waamuzi 4:1–15, na angalia ushawishi aliokuwa nao juu ya watu waliomzunguka. Haya ni baadhi ya maswali ya kukusaidia ufikirie jinsi uzoefu wake unavyoweza kutumika katika maisha yako:
-
Ni kwa jinsi gani ungeelezea hali ambazo Waisraeli walivyokuwa nazo wakati huo? (ona ona mstari wa 1–3). Ni mifanano gani unayoiona kwenye hali za leo—katika watu binafsi na jamii?
-
Ni maneno au matendo gani ya Debora yanakuonyesha wewe kuwa alikuwa na imani katika Bwana? Ni kwa jinsi gani imani yake iliwavutia watu wengine ? Nini kingine kinachokuvutia kumhusu yeye?
-
Unahisi Debora alimaanisha nini kwa swali lake katika mstari wa 14: “Je! Bwana hakutoka atangulie mbele yako?” Je, ni namna gani Bwana “huenda mbele yetu? (pia Mafundisho na Maagano 84:87–88).
Tafakari jinsi imani yako katika Yesu Kristo ingeweza kuwabariki wengine kwa njia ambayo imani ya Debora ilivyombariki Baraka na Waisraeli wengine. Ili kukusaidia kufikiria kuhusu hili, unaweza kujifunza ujumbe wa Mzee Neil L. Andersen ”Tunazungumza juu ya Kristo” (Liahona, Nov. 2020, 88–91). Pekua ujumbe huu kwa ajili ya (1) sababu za kuzungumza kwa uwazi zaidi kuhusu Mwokozi na (2) njia za kufanya hivyo.
Kisha ungeweza kutengeneza orodha ya vitu unavyovijua kuhusu Yesu Kristo—kutoka kwenye maandiko, kutokana na maneno ya manabii walio hai, na kutokana na uzoefu wako binafsi. Nani anahitaji kujua hili? Ni kwa jinsi gani utaweza kuishiriki?
Ona pia Mathayo 5:14–16; 1 Petro 3:15; ”Each Life That Touches Ours for Good,” Nyimbo za Kanisa, na. 293.
Alika kushiriki. Kama wewe ni mwalimu—nyumbani au kanisani—“wape wanafunzi fursa kushiriki wao kwa wao kile wanachojifunza kuhusu Mwokozi na injili Yake. Kufanya hili kutawasaidia kuzifanya kuwa zao kweli hizo wanazofundishwa na wao kuzielezea” (Kufundisha katika Njia ya Mwokozi, 26). Kwa mfano, mnapojifunza Waamuzi 4 kwa pamoja, ungeweza kumpa kila mwanafunzi kitu mahususi cha kutafuta katika sura hii na kisha waalike kushiriki wao kwa wao kile wanachokipata.
Waamuzi 6–8
Bwana anaweza kutenda miujiza nikiamini katika njia zake.
Unaposoma Waamuzi 6–8, andika hali ambapo Bwana alimwomba Gideoni kuamini kitu ambacho kingeweza kuonekana kuwa hakiwezekani. Je, Yeye amewahi kuomba kitu sawa na hicho kwako?
Je, unahisi Bwana anajaribu kukufundisha nini na hadithi hii? Ni kwa jinsi gani umeona Bwana akifanya kazi Yake katika njia iliyoonekana kutokuwa ya kawaida?
Waamuzi 13–16
Mungu huniimarisha ninapokuwa mwaminifu kwa maagano yangu.
Samsoni alipoteza vyote nguvu za kimwili na nguvu za kiroho kwa sababu alivunja maagano yake na Mungu, ikijumuisha yale ambayo mahususi yalihusikai kwa Wanazareti (kwa taarifa kuhusu Wanazareti, ona Hesabu 6:1–6; Waamuzi 13:7). Unaposoma kuhusu Samsoni katika Waamuzi 13–16, tilia maanani mistari inayoonyesha kwamba Bwana alikuwa pamoja na Samsoni, pamoja na mistari inayoonyesha kwamba Samsoni hakujitolea kikamilifu kwa Bwana.
Unaweza pia kutafakari maagano uliyofanya na Bwana. Ni kwa jinsi gani maagano haya yameleta nguvu Yake katika maisha yako? Unajifunza nini kutokana na uzoefu wa Samsoni kinacho kutia moyo kubaki mkweli kwenye maagano yako na Mungu?
Dada Ann M. Dibb alifundisha: “Samsoni alizaliwa na uwezekano mkubwa. Mama yake aliahidiwa, ‘Yeye ataanza kuwakomboa Israeli kutoka katika mikono ya Wafilisti’ [Waamuzi 13:5]. Lakini Samsoni alipokua, aliangalia zaidi majaribu ya ulimwengu kuliko mwelekeo wa Mungu. Alifanya chaguzi kwa sababu ‘zilimpendeza [yeye] vizuri’ [Waamuzi 14:3] badala ya chaguzi hizo kuwa zilikuwa sahihi. Kwa kujirudia, maandiko hutumia kirai kisemacho ‘basi akateremka’ [Waamuzi 14:7] wanaposimulia juu ya safari za Samsoni, matendo, na chaguzi zake. Badala ya kuinuka na kung’aa ili kutimiza uwezekano wake wa kuwa mtu muhimu, Samsoni alishindwa na ulimwengu, akapoteza nguvu aliyopewa na Mungu, na akafa kifo cha kutisha, kifo cha mapema” (“Arise and Shine Forth,” Liahona, Mei 2012, 118).
Ona pia Dallin H. Oaks, “Maagano na Majukumu,” Liahona, Mei 2024, 93–96; Ulisses Soares, “Kujiamini kwa Agano kupitia Yesu Kristo,” Liahona, Mei 2024, 17–21.
Mawazo kwa ajili ya Kuwafundisha Watoto
Kwa sababu Jumapili hii ni Jumapili ya kwanza ya mwezi, walimu wa Msingi wanahimizwa kutumia shughuli za kujifunza katika “Kiambatisho B: Kuwaandaa Watoto kwa Ajili ya Maisha yao Yote kwenye Njia ya Mungu ya Agano.”
Waamuzi 3:7–9, 12–15
Yesu Kristo ni Mkombozi wangu.
-
Waamuzi 3 inaelezea mpangilio ambao unafundisha kuhusu uwezo wa Mwokozi wa kutukomboa sisi kutokana na dhambi. Ili kuwasaidia watoto wako watambue mpangilio huu, ungeweza kuandika virai hivi: “alifanya uovu,” “alimlilia Bwana,” na “akamwinua mwokozi.” Kisha watoto wako wangeweza kutafuta virai hivi katika Waamuzi 3:7–9 na Waamuzi 3:12–15. Je, tunajifunza nini kuhusu Bwana kutoka kwenye mpangilio huu?
-
Ili kusisitiza kwamba Yesu Kristo ni Mkombozi wetu, ungeweza kukusanya picha kadhaa za watu, ikijumuisha picha ya Yesu, na kuziweka zikiangalia chini. Waache watoto wako wachukue zamu kugeuza hizo picha. Wanapoipata picha ya Yesu, imbeni wimbo kumhusu Yeye, kama vile “He Sent His Son” (Kitabu cha Nyimbo za Watoto, 34–35), na waambie watoto wako kuhusu jinsi Yeye alivyokukomboa.
Waamuzi 4:1–15
Ninaweza kuwashawishi wengine kuwa na imani katika Bwana.
-
Unaweza kutumia “Debora Nabii Mke” katika Hadithi za Agano la Kale, 92–95, ili kuwasimulia watoto wako hadithi katika Waamuzi 4. Shiriki na kila mmoja kile mnachopendezwa nacho kuhusu Debora. Ni kwa jinsi gani imani yake katika Bwana iliwabariki watu waliomzunguka? Tunaweza kufanya nini ili kuwasaidia wengine kuwa na imani zaidi katika Yesu Kristo?
2:9Deborah the Prophetess
Waamuzi 7:1–21
Bwana anaweza kutumia vitu vidogo kufanya kazi kubwa.
-
Tumia Waamuzi 7:4–7, ukurasa wa shughuli ya wiki hii, au “Jeshi la Gideoni” katika Hadithi za Agano la Kale, 96–99, ili kuwafundisha watoto wako kuhusu jinsi Bwana alivyolifanya jeshi la Israeli kuwa dogo zaidi. Kwa nini Bwana alitaka jeshi la Gidioni kuwa dogo sana? (ona Waamuzi 7:2).
2:37The Army of Gideon
-
Watoto wako wangeweza kuchora picha za upanga, ngao, tarumbeta, taa, na mtungi na kuzungumza kuhusu ni kitu gani kati ya vitu hivi wangekitaka katika vita. Kisha wangeweza kusoma Waamuzi 7:16 ili kujua kile ambacho Bwana aliliambia jeshi la Gidioni kutumia. Unaposoma kuhusu vita katika Waamuzi 7:19–21, shiriki na kila mmoja kile mnachojifunza kuhusu Bwana kutoka kwenye hadithi hii.
Samsoni Anaangusha Chini Nguzo, na James Tissot pamoja na wengine
Waamuzi 13:5
Kushika maagano kunanipa nguvu.
-
Maagano ya Samsoni na Bwana yalimpa nguvu, kama ambavyo maagano yetu yanavyotupatia nguvu za kiroho. Familia yako inaweza kufurahia kufanya baadhi ya mazoezi ya mwili na kujadili namna gani mazoezi hayo yanaweza kutusaidia kufanya miili yetu iwe yenye nguvu. Ni jinsi gani kushika maagano yetu hufanya roho zetu kuwa imara? (ona Mosia 18:8–10; Mafundisho na Maagano 20:77, 79).
Kwa ajili ya zaidi, ona toleo la mwezi huu la jarida la Rafiki .