Njoo, Unifuate
Mawazo ya Kuweka Akilini: Vitabu vya Kihistoria katika Agano la Kale


“Mawazo ya Kuweka Akilini: Vitabu vya Kihistoria katika Agano la Kale,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Nyumbani na Kanisani: Agano la Kale 2026 (2026)

“Vitabu vya Kihistoria katika Agano la Kale,” Njoo, Unifuate: Agano la Kale 2026

ikoni ya mawazo

Mawazo ya Kuweka Akilini

Vitabu vya Kihistoria katika Agano la Kale

Vitabu vya Yoshua hadi Esta kijadi hujulikana kama “vitabu vya kihistoria” vya Agano la Kale. Hii haimaanishi kwamba vitabu vingine katika Agano la Kale havina thamani ya kihistoria. Badala yake, vitabu vya kihistoria huitwa hivyo kwa sababu lengo kuu la waandishi wake lilikuwa kuonyesha mkono wa Mungu katika historia ya watu wa Israeli. Kusudi halikuwa kuweka muhtasari wa sheria ya Musa, kama Mambo ya Walawi na Kumbukumbu la Torati ifanyavyo. Haikuwa kutoa sifa au kuomboleza katika sura ya kishairi, kama vile Zaburi na Maombolezo yafanyavyo. Na haikuwa kuandika maneno ya manabii, kama vile vitabu vya Isaya na Ezekieli vinavyofanya. Badala yake, vitabu vya kihistoria vinasimulia hadithi.

Jambo la Mtazamo

Kwa kawaida, hadithi hizi zinasimuliwa kutokana na mtazamo fulani. Kama vile haiwezekani kutazama ua, mwamba, au mti kutoka pembe zaidi ya moja kwa wakati mmoja, ni lazima kwamba habari ya kihistoria itaonyesha mtazamo wa mtu au kikundi cha watu wanaoiandika. Mtazamo huu unajumuisha uhusiano wa waandishi wa kitaifa au wa kikabila na kanuni zao za kitamaduni na imani. Kujua hii kunaweza kutusaidia kuelewa kwamba waandishi na watunzi wa vitabu vya kihistoria walifokasi maelezo fulani wakati wakiacha mengine. Walifanya mawazo ambayo wengine hawangeweza kuwa wamefanya. Na walifikia hitimisho kulingana na maelezo na mawazo hayo. Tunaweza hata kuona mitazamo tofauti katika vitabu vya Biblia (na wakati mwingine ndani ya kitabu hicho hicho). Tunapojua zaidi mitazamo hii, ndivyo tunavyoweza kuelewa vitabu vya kihistoria.

Mtazamo mmoja wa kawaida kwa vitabu vyote vya kihistoria vya Agano la Kale ni mtazamo wa watoto wa Israeli, watu wa Mungu wa agano. Imani yao katika Bwana iliwasaidia kuona mkono Wake maishani mwao na katika mambo ya taifa lao. Wakati vitabu vya historia ya kilimwengu havielekei kuona mambo kwa njia hii, mtazamo huu wa kiroho ni sehemu ya kile kinachofanya vitabu vya kihistoria vya Agano la Kale kuwa vya thamani sana kwa wale ambao wanatafuta kujenga imani yao wenyewe katika Mungu.

Muktadha kwa ajili ya Sehemu Yote Inayobakia ya Agano la Kale

Vitabu vya kihistoria vinaanzia mahali ambapo kitabu cha Kumbukumbu la Torati kinaachia, pamoja na miaka ya Waisraeli ya kutangatanga jangwani inapokaribia kwishia. Kitabu cha Yoshua kinaonyesha wana wa Israeli wakiwa tayari kuingia Kanaani, nchi yao ya ahadi, na inaelezea jinsi walivyoitwaa. Vitabu ambavyo vinafuata, Waamuzi hadi 2 Mambo ya Nyakati, vinaonyesha uzoefu wa Israeli katika nchi ya ahadi, tangu wakati walipokaa mpaka wakati walipotekwa na Ashuru na Babeli. Vitabu vya Ezra na Nehemia vinaelezea juu ya kurudi kwa vikundi kadhaa vya Waisraeli katika mji wao mkuu, Yerusalemu, miongo kadhaa baadaye. Mwishowe, kitabu cha Esta kinaelezea hadithi ya Waisraeli walioishi uhamishoni chini ya utawala wa Uajemi.

Na hapo ndipo utaratibu wa kupanga miaka na matukio ya Agano la Kale unapoishia. Wasomaji wa Biblia wa mara ya kwanza wanashangaa kuona kwamba wamemaliza kusoma hadithi ya Agano la Kale kabla hawajasoma zaidi ya nusu ya kurasa zake. Baada ya Esta, hatupati habari nyingi juu ya historia ya Waisraeli. Badala yake, vitabu vinavyofuata—hususani vitabu vya manabii—vinafaa katika ratiba ambayo vitabu vya kihistoria viliwasilisha. Huduma ya nabii Yeremia, kwa mfano, ilifanyika wakati wa hafla zilizorekodiwa katika 2 Wafalme 22–25 (na habari inayofanana katika 2 Mambo ya Nyakati 34–36). Kujua hili kunaweza kuathiri jinsi unavyosoma hadithi zote za kihistoria na vitabu vya unabii.

Wakati Kitu fulani Kinapokuwa Hakifai.

Unaposoma Agano la Kale, kama ilivyo kwa historia yoyote, una uwezekano wa kusoma juu ya watu wanaofanya au kusema vitu ambavyo, kwa macho ya kisasa, vinaonekana kuwa vigeni au hata vya kusumbua. Tunapaswa kutarajia hii—waandishi wa Agano la Kale waliuona ulimwengu kwa mtazamo ambao, kwa njia zingine, ulikuwa tofauti kabisa na wetu. Vurugu, uhusiano wa kikabila, na majukumu ya wanawake ni baadhi tu ya masuala ambayo waandishi wa zamani wangeweza kuona tofauti na sisi leo.

Kwa hivyo tunapaswa kufanya nini tunapokutana na vifungu katika maandiko ambavyo vinaonekana kuwa vya kutatanisha? Kwanza, inaweza kusaidia kuzingatia kila kifungu katika muktadha mpana. Je! Inafaa katika mpango wa wokovu wa Mungu? Je! Inafaa katika kile unachojua juu ya asili ya Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo? Je! Inafaa katika ukweli uliofunuliwa katika maandiko mengine au na mafundisho ya manabii walio hai? Na inafaa vipi na minong’ono ya Roho kwa moyo wako na akili yako?

Katika hali zingine, kifungu kinaweza kuonekana kutokufaa vizuri na yo yote ya haya. Wakati mwingine kifungu kinaweza kuwa kama kipande cha chemsha bongo ambacho hakionekani kama kina nafasi kati ya vipande vingine ambavyo tayari umekusanywa. Kujaribu kulazimisha kipande kutosha sio njia bora. Lakini pia hakuna kukata tamaa kwa chemsha bongo yote. Badala yake, unaweza kuhitaji kuweka kipande kando kwa muda Unapojifunza zaidi na kuunganisha pamoja chemsha bongo, unaweza kuona vizuri jinsi vipande vinavyounganika pamoja.

Inaweza pia kusaidia kukumbuka kuwa kwa kuongeza kuwa na mipaka kwa mtazamo fulani, historia za maandiko zinakabiliwa na makosa ya kibinadamu.. Kwa mfano, kwa karne nyingi “vitu vingi vya wazi na vya thamani [vili] ondolewa kutoka katika [Biblia],” pamoja na ukweli muhimu kuhusu mafundisho, ibada na maagano (1 Nefi 13:28; ona pia mstari wa 29–40). Wakati huo huo, tunapaswa kuwa tayari kukubali kwamba mitazamo yetu wenyewe pia ina ukomo: daima kutakuwa na vitu ambavyo hatuelewi kabisa na maswali ambayo bado hatuwezi kujibu.

mtu akiweka chemsha bongo pamoja

Baadhi ya vifungu vya maandiko vinaweza kuwa kama vipande vya chemsha bongo ambavyo hatujui jinsi ya kuviweka pamoja na picha yote iliyosalia ya chemsha bongo.

Kupata Vito

Lakini kwa wakati huu, maswali ambayo hayajajibiwa hayapaswi kutuzuia kufikia vito vya thamani vya ukweli wa milele ambavyo vinapatikana katika Agano la Kale—hata kama vito hivyo wakati mwingine hufichwa kwenye ardhi ya miamba ya uzoefu wa kusumbua na uchaguzi mbaya uliofanywa na watu wasio wakamilifu. Labda thamani kubwa zaidi ya vito hivi ni hadithi na vifungu vinavyoshuhudia upendo wa Mungu—hususani vile vinavyoelekeza akili zetu kuelekea dhabihu ya Yesu Kristo. Vikitazamwa kutoka pembe yoyote, vito kama hivi vinaangaza hivi leo kama vile vilivyofanya wakati huo. Na kwa sababu maelezo haya yanaelezea juu ya watu wa Mungu wa agano—wanaume na wanawake ambao walikuwa na udhaifu wa kibinadamu na bado walimpenda na kumtumikia Bwana—vito vya ukweli viko katika vitabu vya kihistoria vya Agano la Kale.

jiwe la vito

Muhtasari

  1. Simulizi za kihistoria za Biblia tuliyonayo leo kimsingi ni kazi ya waandishi na watunzi wasiotajwa, ambao wakati mwingine walifanya kazi miaka mingi, hata karne nyingi, baada ya vipindi vya wakati wanavyoelezea. Walitegemea vyanzo anuwai vya kihistoria na walifanya maamuzi juu ya nini cha kujumuisha kwenye maelezo yao na nini cha kutokijumuisha.

  2. Kwa mfano, ingawa 1–2 Mambo ya Nyakati inajumuisha takriban kipindi kama hicho cha 1 Samweli 31 hadi mwisho wa 2 Wafalme, maelezo katika 1–2 Mambo ya Nyakati yanasisitiza maelezo ya kina tofauti na inatoa mtazamo tofauti, ukifokasi tu kwenye Ufalme wa Kusini wa Yuda na mara nyingi huacha hadithi hasi kuhusu Daudi na Sulemani (linganisha, kwa mfano, 2 Samweli 10–12 na 1 Mambo ya Nyakati 19–20 na 1 Wafalme 10–11 na 2 Mambo ya Nyakati 9). Njoo, Unifuate inasisitiza kusoma maelezo katika 1 na 2 Wafalme, ingawa kuna thamani katika kulinganisha habari hiyo na 1 na 2 Mambo ya Nyakati. Inaweza kusaidia kujua kazi hiyo katika 1 Samweli–2 Wafalme labda ilianza kabla ya ufalme wa Babeli kuishinda Yuda na kukamilika wakati wa uhamisho huko Babeli. Kumbukumbu ambayo ilikuja kuwa 1–2 Mambo ya Nyakati, kwa upande mwingine, ilikusanywa baada ya Wayahudi kurudi Yerusalemu kutoka uhamishoni kwao. Unaposoma, unaweza kuzingatia jinsi hali hizi tofauti ambavyo zingeweza kuathiri mitazamo ya watunzi wa matukio tofauti.

  3. Kuelekea mwanzo wa chanzo hiki utapata “Muhtasari wa Agano la Kale,” mpangilio wa wakati ambao unaonyesha jinsi huduma ya kila nabii inalingana na historia ya Israeli (na vile vile inaweza kuamua). Utaona kwamba vitabu vingi vya unabii vya Agano la Kale vinaangukia karibu na mwisho wa mstari huo wa muda—kabla tu na baada tu ya watoto wa Israeli kutekwa, kuhamishwa, na kutawanywa na maadui zao.

  4. Ona Makala ya Imani 1:8.