Septemba 14–20. ‘Mungu Ndiye Wokovu Wangu’: Isaya 1–12,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Nyumbani na Kanisani: Agano la Kale 2026 (2026)
Septemba 14–20. ‘Mungu Ndiye Wokovu Wangu,’” Njoo, Unifuate: Agano la Kale 2026
Nabii Isaya Atabiri Kuzaliwa kwa Kristo, na Harry Anderson
Septemba 14–20: “Mungu Ndiye Wokovu Wangu”
Isaya 1–12
Hata ikiwa hii ni mara yako ya kwanza kusoma kitabu cha Isaya, unaweza kupata vifungu ambavyo vinaonekana kuwa vya kawaida. Hiyo ni kwa sababu, kati ya manabii wote wa Agano la Kale, Isaya ndiye anayenukuliwa mara nyingi katika vitabu vingine vya maandiko, pamoja na Mwokozi mwenyewe. Maneno ya Isaya pia huonekana mara nyingi katika nyimbo na muziki mwingine mtakatifu.
Kwa nini Isaya amenukuliwa mara nyingi? Hakika sababu moja ni kwamba Isaya alikuwa na kipawa cha kuelezea neno la Mungu kwa lugha ya wazi, ya kukumbukwa. Lakini ni zaidi ya hilo. Isaya amewatia moyo manabii wa vizazi vingi kwa sababu kweli alizofundisha zilivuka kizazi chake mwenyewe (kati ya mwaka 740 na 701 KK). Aliandika juu ya kazi kuu ya Mungu ya ukombozi, ambayo ni kubwa zaidi kuliko taifa moja au kipindi cha wakati mmoja. Kutoka kwa Isaya, Nefi alijifunza kwamba yeye na watu wake, ingawa walitengwa na Israeli ingine, bado walikuwa sehemu ya watu wa Mungu wa agano. Katika Isaya, waandishi wa Agano Jipya walipata unabii juu ya Masiya ambao ulitimizwa mbele ya macho yao. Na katika Isaya, Joseph Smith alipata mwongozo wa kiungu kwa ajili ya kazi ya kukusanya Israeli na kujenga Sayuni. Wewe unaposoma Isaya, utapata nini?
Kwa mengi kuhusu Isaya na maandiko yake, ona “Isaya” katika Kamusi ya Biblia. Kwa taarifa kuhusu muda ambao Isaya aliishi, ona 2 Wafalme 15–20 na 2 Mambo ya Nyakati 26–32.
Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Nyumbani na Kanisani
Isaya 1–12
Maneno ya Isaya yote yatatimizwa.
Mwokozi alifundisha kwamba “vitu vyote ambavyo alizungumza vimekuwa na vitakuwa, hata kulingana na maneno ambayo alisema (3 Nefi 23:3). Unapojifunza kitabu cha Isaya, fikiria kutengeneza chati ya unabii wenye vichwa vya habari kama hivi: Siku ya Isaya, Huduma ya Mwokozi duniani, na Siku za Mwisho. Kumbuka kwamba unabii mwingi wa Isaya unatimizwa kwa zaidi ya njia moja (ona Kamusi ya Biblia, “Isaya”).
Rais Dallin H. Oaks alifundisha: “Kitabu cha Isaya kina unabii mwingi ambao unaonekana kuwa na utimizwaji mwingi. Mmoja unaonekana kuhusisha watu wa siku ya Isaya au hali za kizazi kinachofuata. Maana nyingine, mara nyingi kiishara, unaonekana kurejelea matukio katika wakati wa meridiani, wakati Yerusalemu ilipoangamizwa na watu wake kutawanywa baada ya kusulubiwa kwa Mwana wa Mungu. Bado maana nyingine ya utimizwaji wa unabii huo huo unaonekana kuhusika na matukio yatanguliayo Ujio wa Pili wa Mwokozi. Ukweli kwamba wingi wa unabii huu unaweza kuwa na maana nyingi inadhihirisha umuhimu wa haja yetu ya ufunuo kutoka kwa Roho Mtakatifu hili kutusaidia kuutafsiri (“Scripture Reading and Revelation,” Ensign, Jan. 1995, 1995).
Kuelewa Isaya. Mwokozi alisema, “Yachunguzeni mambo haya kwa bidii; kwani maneno ya Isaya ni makuu” (3 Nefi 23:1; ona pia mistari 2–3). Walakini kwa wengi, Isaya inaweza kuwa vigumu kuielewa. Mawazo yafuatayo yangeweza kusaidia:
-
Tafakari ishara na sitiari alizotumia Isaya.
-
Jiulize, “Ninajifunza nini kuhusu Yesu Kristo? (ona 1 Nefi 19:23).
-
Tafuta mada ambazo zinaonekana kuhusika na wakati wetu.
-
Tumia visaidizi vya kujifunza vinapopatikana, kama vile kamusi, tanbihi ya Biblia, vichwa vya habari vya sura, na Mwongozo wa Maandiko.
Isaya 1; 3–5
Manabii wanaonya kuhusu dhambi na ahadi ya tumaini kupitia toba.
Kama manabii katika nyakati zote, Isaya daima aliwaonya watu kuhusu hali yao ya kiroho. Unaposoma Isaya 1; 3; 5, tafuta viraii ambavyo vinaelezea jinsi watu walivyokuwa wakifanya kiroho (ona, kwa mfano, Isaya 1:2–4, 21–23; 3:9, 16–17; 5:11–12, 20–23). Ni matatizo gani yanayofanana unayoyaona katika wakati wetu? Unaweza pia kutafuta mistari ambayo inaonya kuhusu matokeo ya hali ya kiroho ya Waisraeli (kama vile Isaya 1:7; 3:17–26; 5:5–7, 13–15).
Kwa kuongezea kwenye maonyo, Isaya alitoa jumbe za tumaini kwa ajili ya ukombozi kupitia Mwokozi (ona, kwa mfano, Isaya 1:16–19, 25–27; 3:10; 4). Je, unajifunza nini kumhusu Bwana kutoka kwenye jumbe hizi? Ni kwa jinsi gani ujumbe wa Bwana katika mistari hii ni tofauti na kile ambacho Shetani anataka tuamini?
Kama vile Isaya, manabii leo wanatuonya kuhusu dhambi na matokeo yake, na wanatoa jumbe za tumaini kupitia Yesu Kristo. Je, ni mifano gani unaweza kuifikiria? Unaweza kutaka kurejelea ujumbe kutoka kwenye mkutano mkuu uliopita, ukitafuta maonyo na ahadi kama hizo.
Isaya 2; 4; 11–12
Mungu atafanya kazi kuu katika siku za mwisho.
Unabii mwingi wa Isaya ni unabii ambao una maana maalum kwa ajili ya siku zetu. Ili kuupata, tafuta vitenzi vya wakati ujao (kama vile “vitakuwa” au “vitakwenda”). Kwa mfano, tafuta vitenzi hivi unaposoma Isaya 2; 4; 11–12. Unaweza hata kujaribu kuvibadilisha kwa vitenzi vya wakati wa sasa (kama ilivyo au unakwenda). Je, ni unabii gani maalumu ambao unakupatia wewe mwongozo wa kiungu? Unajifunza nini kutoka unabii huu kuhusu Sayuni, kujenga mahekalu, na kukusanya Israeli?
Isaya 2:2–3 inahusika hasa kwa Watakatifu wa Siku za Mwisho. Ni kwa jinsi gani unabii huu unatimia? Je, unajifunza nini kuhusu “njia” na “mapito” ya Bwana katika nyumba Yake? (mstari wa 3).
Ona pia Isaya 5:26; “Juu ya Mlima,” Nyimbo za Dini, na. 5.
Isaya 6
Manabii wanaitwa na Mungu.
Katika Isaya 6, Isaya alisimulia kuhusu wito wake wa kuwa nabii. Unaposoma sura hii, ni nini kinachokuvutia kuhusu uzoefu wa Isaya? Ni kwa jinsi gani sura hii inashawishi vile unavyofikiria kuhusu Bwana, manabii Wake, na kazi ambayo wameitwa kuifanya?
“Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, tumepewa mtoto mwanamume” (Isaya 9:6).
Isaya 7–9
Mungu aliahidi kumtuma Yesu Kristo kuwa Mwokozi wangu.
Wakati wa huduma ya Isaya, Israeli iliunda muungano na Syria ili kujilinda dhidi ya Ashuru. Israeli na Shamu zilitaka kumlazimisha Ahazi, mfalme wa Yuda, ili ajiunge nao. Lakini unabii wa Isaya kwamba umoja ungeshindwa na akamshauri Ahazi kumwamini Bwana (Isaya 7:7–9; 8:12–13).
Wakati Isaya alipomshauri Ahazi, alitoa unabii kadhaa maarufu, kama vile ule unaopatikana katika Isaya 7:14; 8:13–14; 9:2, 6–7. Ingawa haijulikani kabisa unabii huu ulimaanisha nini wakati wa Ahazi, ni wazi unatumika kwa Yesu Kristo (ona pia Mathayo 1:21–23; 4:16; 21:44; Luka 1:31–33). Kwa mfano, kwa nini “Imanueli” ni jina zuri kwa Mwokozi? (ona Mathayo 1:23). Ni kwa jinsi gani Yeye amekuwa “Mshauri” au “Mfalme wa Amani” kwakoi? (Isaya 9:7). Unajifunza nini kingine kumhusu Mwokozi kutoka kwenye mistari hii?
Kwa ajili ya zaidi, ona matoleo ya mwezi huu ya majarida ya Liahona na Kwa ajili ya Nguvu kwa Vijana..
Mawazo kwa ajili ya Kuwafundisha Watoto
Isaya 1:2–4, 16–19
Kwa sababu ya Yesu Kristo, ninaweza kutubu na kuwa safi.
-
Katika Isaya 1:2–4, wewe na watoto wako mngeweza kupata sababu ambazo Bwana hakuwa na furaha na watu wale. Tazama mfanano na wanyama katika mstari wa 3—“bwana” wetu ni nani? Ni kwa jinsi gani tunaonyesha kwamba tunamjua Yeye?
-
Ili kupiga taswira Isaya 1:16–18, wewe na watoto wako mngeweza kuangalia kitu chekundu sana na kitu safi cheupe. Au pengine mngeweza kufanya kazi pamoja kuosha kitu fulani. Ni kwa jinsi gani tunaweza kuwa wachafu kiroho? Ni kwa jinsi gani Yesu anatusaidia kuwa wasafi? Je, tunajifunza nini kuhusu Mwokozi kutoka kwenye mistari hii? Shiriki na watoto wako jinsi unavyohisi kumhusu Yeye na kile Yeye alichokufanyia.
Isaya 2:2–4
Ndani ya hekalu ninajifunza kuhusu Yesu Kristo.
-
Isaya aliona mapema wakati ambapo hekalu, “mlima wa nyumba ya Bwana,” litawavutia watu kutoka “mataifa yote” (Isaya 2:2). Ni kwa jinsi gani unaweza kuwasaidia watoto wako wahisi msisimko kuhusu kwenda kwenye nyumba ya Bwana? Ungeweza kuwaalika kuchora picha ya nyumba yao. Kisha someni pamoja Isaya 2:2, na waalike wao kuchora picha ya “nyumba ya Bwana,” ambayo ni hekalu. Someni Isaya 2:3 pamoja. Waalike waongeze kwenye picha zao watu wengi wakija hekaluni, ikiwa ni pamoja na familia zao.
-
Mngeweza pia kusoma Isaya 2:2–3 pamoja na kutambua kitu ambacho kinakutia msukumo wewe na watoto wako kwenda hekaluni. Kisha, baada ya kusoma Isaya 2:4 pamoja, mngeweza kujadili jinsi hekalu linavyowaletea amani. Fikirieni kuimba pamoja wimbo kuhusu hekalu, kama vile “I Love to See the Temple” (Kitabu cha Nyimbo za Watoto, 95). Wasaidie watoto wako kutafuta virai kutoka kwenye wimbo ambavyo vinafundisha hekalu ni nini na nini tunakifanya hekaluni.
Hekalu la Salt Lake
Isaya 7:14; 9:6–7
Yesu Kristo alikuja duniani kuwa Mwokozi wangu.
-
Ili kutambulisha unabii wa Isaya juu ya Kristo, wewe na watoto wako mngeweza kuzungumza kuhusu majina ya watu, kama rais, askofu, au mwalimu. Je, vyeo hivi hutuambia nini kuhusu watu hawa? Wasaidie watoto wako wapate majina ya Yesu Kristo katika Isaya 7:14 na 9:6–7 (ona pia ukurasa wa shughuli ya wiki hii). Je, kila moja ya majina haya linatufundisha nini kumhusu Yeye? Je, tunajifunza nini kingine kuhusu Yesu Kristo kutoka kwenye mistari hii?
-
Ungeweza pia kushiriki na watoto wako “Isaya Nabii” (katika Hadithi za Agano la Kale, 150–51). Simama mara kwa mara ili watoto waweze kuzungumza juu ya kile Isaya alichojua kuhusu Yesu Kristo miaka mingi kabla hajazaliwa. Kisha unaweza kutumia Mathayo 1:21–23; Luka 1:31–33 kuzungumza kuhusu jinsi unabii wa Isaya katika Isaya 7:14; 9:6–7 ilitimizwa.
1:18Isaiah the Prophet
Kwa ziada, ona toleo la mwezi huu la jarida la Rafiki .