Njoo, Unifuate
Mawazo ya Kuweka Akilini: Kusoma Agano la Kale


“Mawazo ya Kuweka Akilini: Kusoma Agano la Kale,” Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Nyumbani na Kanisani, Agano la Kale 2026 (2026)

“Kusoma Agano la Kale,” Njoo, Unifuate: 2026

ikoni ya mawazo

Mawazo ya Kuweka Akilini

Kusoma Agano la Kale

Wakati Nefi alipotaka kuwatia moyo ndugu zake kumwamini Bwana, alishiriki hadithi kuhusu Musa na mafundisho kutoka kwa Isaya. Wakati Mtume Paulo alipotaka kuwatia moyo Wakristo wa mwanzo kuwa na imani katika ahadi za Mungu, aliwakumbusha kuhusu imani ya Nuhu, Ibrahimu, Sara, Rahabu, na wengine. Na wakati Yesu Kristo alipowaambia viongozi wa Wayahudi “kupekua maandiko,” akielezea kwamba “yananishuhudia” (Yohana 5:39), maandiko Yeye aliyokuwa akiyazungumzia ni maandiko tunayoyaita Agano la Kale.

Kwa maneno mengine, unaposoma Agano la Kale, unasoma maneno ambayo yanawashawishi, kuwafariji, na kuwatia moyo watu wa Mungu kwa maelfu ya miaka.

Lakini je, kitu ambacho kiliandikwa muda mrefu sana uliopita kinakusaidia kupata suluhisho kwa matatizo ya leo? “Ndiyo, inawezekana! Hususani kama unakumbuka ni nani hasa Agano la Kale linamhusu.

Ushuhuda juu ya Yesu Kristo

Changamoto zo zote ambazo wewe na familia yako mnakabiliana nazo, jibu daima ni Yesu Kristo. Hivyo kupata majibu katika Agano la Kale, mtafute Yeye. Haitakuwa rahisi kila wakati. Unaweza kuhitaji kutafakari kwa uvumilivu na kutafuta mwongozo wa kiroho. Nyakati zingine marejeleo Kwake huonekana moja kwa moja, kama vile katika tamko la Isaya “Kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, tumepewa mtoto mwanamume: … naye ataitwa jina lake … Mfalme wa Amani” (Isaya 9:6). Katika mahali pengine, Mwokozi amewakilishwa kwa ustadi zaidi, kupitia alama na mifanano—kwa mfano, kupitia maelezo ya dhabihu za wanyama au hadithi ya Yusufu akiwasamehe kaka zake na kuwaokoa kutokana na baa la njaa.

Yesu Kristo amesimama juu ya mwamba ulioitazama bahari

Nuru ya Ulimwengu, na Scott Summer

Kama unatafuta kuwa na imani kubwa zaidi katika Mwokozi unaposoma Agano la Kale, utaipata. Pengine hili lingeweza kuwa kusudi la kujifunza kwako mwaka huu. Omba kwamba Roho akuongoze ili kupata na kufokasi juu ya vifungu vya maneno, hadithi, na unabii ambao utakuleta karibu zaidi na Yesu Kristo.

Yalihifadhiwa Kiungu

Usitegemee Agano la Kale kuwasilisha historia safi na sahihi ya mwanadamu. Hicho sio kitu ambacho waandishi na wakusanya taarifa wa mwanzo walikuwa wakijaribu kukitengeneza. Wasiwasi wao mkubwa zaidi ulikuwa ni kufundisha kitu fulani kuhusu Mungu—kuhusu mpango Wake kwa ajili ya watoto Wake, kuhusu inamaanisha nini kuwa watu Wake wa agano, na kuhusu jinsi ya kupata ukombozi wakati tunapokuwa hatuishi kulingana na maagano yetu. Wakati mwingine walifanya hivyo kwa kuhusisha matukio ya kihistoria kadiri wao walivyoelewa ikijumuisha hadithi kutoka katika maisha ya manabii wakubwa. Kitabu cha Mwanzo ni mfano wa hili, vile vile vitabu kama Yoshua, Waamuzi, na 1 na 2 Wafalme. Lakini waandishi wengine wa Agano la Kale hawakukusudia hii kuwa ya kihistoria kabisa. Badala yake, walifundisha kwa njia ya matendo ya kisanii kama vile mashairi na fasihi andishi. Zaburi na Methali zinaingia katika kundi hili. Na kisha kuna maneno ya thamani ya manabii, kutoka Isaya hadi Malaki, ambao walinena maneno ya Mungu wa kale wa Israeli—na, kupitia muujiza wa Biblia, bado ananena kwetu leo.

Je, manabii wote hawa, watunga mashairi, na wakusanya habari walijua kwamba maneno yao yangekuja kusomwa na watu ulimwenguni kote maelfu ya miaka baadae? Sisi hatujui. Lakini tunastaajabia kwamba hili ndilo haswa lililotokea. Mataifa yaliibuka na kuanguka, majiji yalitekwa , wafalme waliishi na kufa, lakini Agano la Kale limedumu kuliko vyote, kutoka kizazi hadi kizazi, kutoka mwandishi hadi mwandishi, kutoka tafsiri hadi tafsiri. Ndiyo baadhi ya vitu vilipotea au kubadilishwa, lakini bado kwa kiasi fulani mengi sana kimiujiza yalihifadhiwa.

nabii wa kale akiandika kwenye hati ya kukunja

Nabii wa Agano la Kale, na Judith A. Mehr (kwa undani)

Haya ni baadhi ya mambo machache tunayoyaweka akilini tunaposoma Agano la Kale mwaka huu. Mungu alihifadhi maandishi haya ya kale kwa sababu Yeye anakujua wewe na yale unayoyapitia. Yeye ameandaa ujumbe wa kiroho kwa ajili yako katika maneno haya, ambayo yatakuvuta wewe karibu zaidi Kwake na kujenga imani yako katika mpango Wake na Mwanawe Mpendwa. Pengine atakuongoza kwenye kifungu cha maneno au umaizi ambao utambariki mtu fulani unayemjua—ujumbe unaoweza kushiriki na rafiki, mwana familia, au Mtakatifu mwenzako. Kuna uwezekano mwingi sana. Je, hii haisisimui kufikiria hivyo?

Nefi alisema, “Nafsi yangu hufurahia katika maandiko” (2 Nefi 4:15). Pengine utahisi vivyo hivyo unaposoma maneno mengi sawa na yale Nefi aliyoyasoma —yale tunayoyaita sasa Agano la Kale.

Vitabu katika Agano la Kale

Katika matoleo mengi ya tafsiri za Kikristo ya Agano la Kale, vitabu vimepangwa tofauti kutokana na jinsi vilivyokuwa vimepagwa wakati mwanzoni vilipokuwa vimekusanywa katika mkusanyiko mmoja. Hivyo basi wakati Biblia ya Kiebrania imepanga vitabu hivyo katika makundi ya aina tatu—sheria, manabii, na maandishi—Biblia nyingi za Kikristo zinapanga vitabu hivyo katika makundi ya aina nne: sheria (Mwanzo–KumbuKumbu la Torati), historia (Joshua–Esta), vitabu vya mashairi (Ayubu–Wimbo wa Sulemani), na manabii (Isaya–Malaki).

Kwa nini hizi aina za makundi ni muhimu? Kwa sababu kujua aina ya kitabu unachosoma inaweza kukusaidia wewe kuelewa jinsi ya kujifunza kitabu hicho.

Hapa kuna kitu cha kukiweka akilini unapoanza kusoma “sheria,” au vitabu vitano vya kwanza vya Agano la Kale. Vitabu hivi, ambavyo vinadhaniwa kuwa ni vya Musa, pengine vimepita kupitia mikono ya waandishi wengi na wakusanya habari wengi kwa muda mrefu. Na tunapojua kwamba, kwa karne nyingi, “sehemu nyingi ambazo ni wazi na zenye thamani kubwa” ziliondolewa kutoka kwenye Biblia (ona 1 Nefi 13:23–26). Bado, vitabu hivi vya Musa ni neno la Mungu lenye mwongozo wa kiungu, hata kama ni—kama kazi nyingine yoyote iliyopitishwa kupitia kwa mwanadamu—unategemea mapungufu ya mwanadamu (ona Musa 1:41; Makala ya Imani 1:8). Maneno ya Moroni, yakiashiria Kitabu Kitakatifu cha Mormoni kumbukumbu ambayo alisaidia kuikusanya, ni zenye msaada hapa: “Kama kuna makosa ni hitilafu ya wanadamu; kwa hivyo, usilaumu vitu vya Mungu” (ukurasa wa jina la Kitabu cha Mormoni). Katika maneno mengine, kitabu cha maandiko hakihitaji kuwa bila hitilafu za kibinadamu ili kuwa neno la Mungu.

Mihutasari

  1. Ona 1 Nefi 4:2–3; 17:23–43; 19:22–23.

  2. Ona Waebrania 11.

  3. Ona Russell M. Nelson, “Jibu Daima Ni Yesu Kristo,” Liahona, Mei 2023. 127–28.

  4. Ona Mambo ya Walawi 1:3–4.

  5. Ona Mwanzo 45–46.

  6. Rais M. Russell Ballard alisema: “Siyo kwa bahati au jambo lililotokea kulingana na jingine kwamba tunayo Biblia leo. Watu wenye haki walisukumwa na Roho kuandika vyote viwili mambo matakatifu waliyoyaona na maneno yenye mwongozo wa kiungu waliyoyasikia na kunena. Watu wengine waaminifu walishawishika kulinda na kuhifadhi kumbukumbu hizi” (“Muujiza wa Biblia Takatifu,” Liahona, Mei 2007, 80).