“April 13–19. ‘Simameni Tu Mkauone Wokovu wa Bwana’: Kutoka 14–18,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Nyumbani na Kanisani: Agano la Kale 2026 (2026)
“April 13–19. “Simameni Tu, Mkauone Wokovu wa Bwana,’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi: Agano la Kale 2026
Kutoka 13-19: “Simameni Tu, Mkauone Wokovu wa Bwana”
Kutoka 14–18
Waisraeli walikuwa wako mtegoni. Bahari ya Shamu ilikuwa upande mmoja, na jeshi la Farao lilikuwa likiwasogelea upande mwingine. Kutoroka kwao kutoka Misri, ilionekana, kungekuwa kwa muda mfupi. Lakini Mungu alikuwa na ujumbe kwa ajili ya Waisraeli kwamba Yeye aliwataka kukumbuka kwa vizazi vingi: “Msiogope. … Bwana atapigana kwa ajili yenu” (Kutoka 14:13–14).
Tangu muda huo, wakati watu wa Mungu walipohitaji imani na ujasiri, wameelezea hadithi hii. Wakati Nefi alipotaka kuwashawishi kaka zake, alisema, “Tuwe hodari kama Musa; kwani aliyazungumzia maji ya Bahari ya Shamu na yakagawanyika sehemu mbili huku na huku, na mababu zetu wakapita, wakatoka utumwani, juu ya nchi kavu” (1 Nefi 4:2). Wakati mfalme Limhi alipowataka watu wake walio utumwani “kuinua vichwa [vyao], na kushangilia,” aliwakumbusha juu ya hadithi hii (Mosia 7:19). Vivyo hivyo Alma, alipotaka kushuhudia kwa mwanawe juu ya nguvu za Mungu (ona Alma 36:28). Na tunapohisi kuwa mtegoni—tunapohitaji imani zaidi “kuona wokovu wa Bwana”—tunaweza kukumbuka jinsi “Bwana alivyoiokoa Israeli siku ile” (Kutoka 14:13, 30).
Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Nyumbani na Kanisani
Kutoka 14; Kutoka 15:1–21
Bwana anaweza kufanya “kazi kuu” katika maisha yangu.
Unaposoma Kutoka 14:1–10, fikiria jinsi Waisraeli walivyohisi walipoona jeshi la Farao linawakaribia. Pengine unahisi kwamba unahitaji muujiza wa kupona changamoto ngumu unayokabiliana nayo. Je, unapata nini katika Kutoka 14:13–31 ambacho kinakuvutia kutafuta nguvu za Mungu katka maisha yako? Tafakari jinsi ulivoona nguvu Yake wakati uliopita. Umejifunza nini kumhusu Yeye kutokana na uzoefu huu?
Kutoka 15:1–19 ni wimbo wa sifa ambao Waisraeli waliimba baada ya Bwana kuigawanya Bahari ya Shamu. Ni virai gani katika wimbo huu unavyopata hususani vyenye maana? Pengine kuna wimbo ambao unahisi kama kuimba wakati Bwana amefanya kitu cha kushangaza kwako, kama vile “Mkombozi wa Israeli” (Nyimbo za Dini, na. 6). Fikiria kuimba au kuusikiliza kama sehemu ya kuabudu kwako leo
Ona pia Mafundisho na Maagano 8:2–3.
Kutoka 15:22–27; 16:1–15; 17:1–7
Bwana anaweza kufanya vitu vichachu kuwa vitamu.
Kusoma kuhusu safari ya Israeli kunaweza kukuongoza kufikiri kuhusu mambo katika maisha yako ambayo yalionekana kuwa “machungu” kama maji ya Mara (ona Kutoka 15:23–27). Ni kwa jinsi gani Bwana amefanya vitu vichungu katika maisha yako kuwa vitamu? Je, uzoefu huu umekuwa na thamani gani katika maisha yako?
Utaona mifano zaidi ya matukio machungu kwa Waisraeli katika Kutoka 16 na 17. Inajaribu kuelezea kwa kina manung’uniko yao au malalamiko, lakini unaposoma, fikiria kama umewahi kufanya jambo hilo hilo. Je, unajifunza nini kutokana na uzoefu wa Waisraeli ambacho kinaweza kukusaidia kupunguza kunung’unika na kumtumainia Mungu zaidi? Aya hizi zinakufundisha nini kuhusu Mungu?
Ona pia 1 Nefi 2:11–12.
Waisraeli wakikusanya mana. Fresco ya Neo-gothic, Trnava (maelezo ya kina)
Kutoka 16
Bwana hunipa chakula cha kiroho kila siku.
Kwa vile sote tunahitaji kula, Bwana mara nyingi hulinganisha vitu vya kiroho na chakula. Tafuta masomo Yake ya kiroho katika uzoefu wa Waisraeli na mana katika Kutoka 16. Kwa mfano, unapata nini katika maelekezo ya Bwana katika Kutoka 16:16, 19, 22–26 ambacho kinatumika kwenye lishe yako ya kiroho?
Ili kugundua masomo mengine ambayo Bwana anaweza kukutaka ujifunze kutokana na muujiza huu, tafakari maswali kama haya:
-
Ni nini Bwana anatupatia sisi ambacho ni kama mana ya kila siku ambayo Yeye aliwapa Waisraeli?
-
Ninaweza kufanya nini ambacho ni kama kukusanya mana?
Unaweza kupata umaizi wa ziada katika moja au zaidi ya video hizi: “Daily Bread: Pattern,” ”Daily Bread: Experience,” na “Daily Bread: Change” (Maktaba ya Injili).
Daily Bread: Pattern
Daily Bread: Experience
Daily Bread: Change
Fikiria juu ya vitu vingine, kando na kula, ambavyo unafanya kila siku. Kwa nini mambo fulani lazima yafanyike kila siku ili yawe yenye ufanisi? Je, nini unahisi kuvutiwa kufanya kutafuta uzoefu wa kiroho kila siku?
Ona pia Dieter F. Uchtdorf, “Urejesho wa Kila Siku,” Liahona, Nov. 2021, 77–79; “Daily Restoration” (video), Maktaba ya Injili.
Daily Restoration
Kutoka 17:1–7
Yesu Kristo ni mwamba wangu wa kiroho na ni maji ya uzima.
Fikiria kuhusu Mwokozi unaposoma Kutoka 17:1–7. Ni kwa jinsi gani Yesu Kristo ni kama mwamba kwako? (ona Zaburi 62:6–7; Helamani 5:12). Ni kwa jinsi gani Yeye ni kama maji? (ona Yohana 4:10–14; 1 Wakorintho 10:1–4; 1 Nefi 11:25).
Tafuta vitu vya kimwili ambavyo vinashuhudia juu ya Kristo. Wakati wowote maandiko yanapoelezea mambo ambayo yanaweza kuwa ishara ya Yesu Kristo, kama Kutoka 17:1–7 inavyofanya, inaweza kuwa fursa kwa somo la vitendo. Kuangalia au kugusa mwamba au maji kunaweza kurahisisha kuelewa jinsi vitu hivi ni kama Yesu Kristo. Ikiwa unaweza kuhusisha hisia nyingi katika kujifunza, itakuwa ya kukumbukwa zaidi na yenye kuleta matokeo.
Kutoka 17:8–16; 18:13–26
Wanafunzi wanasaidiana “kubeba mzigo” wa kufanya kazi ya Bwana.
Kunaweza kuwa na nyakati katika maisha yako unapoweza kuhusiana na Musa—wakati wengine wanapokutegemea, lakini “mikono yako [inahisi] kulemewa” (Kutoka 17:12). Nyakati zingine, unaweza kuwa zaidi kama Haruni, Huri, na Yethro, ambao walimuunga mkono Musa. Jiweke katika nafasi ya kila mmoja wa watu hawa unaposoma Kutoka 17:8–16; 18:13–26, na uone kile Bwana anachokufundisha kuhusu kazi Yake.
Ona pia Mosia 4:27; 18:8–9.
Kwa ajili ya zaidi, ona matoleo ya mwezi huu ya majarida ya Liahona na Kwa ajili ya Nguvu kwa Vijana. .
Mawazo kwa ajili ya Kuwafundisha Watoto
Kutoka 14:5–22
Bwana anaweza kufanya “kazi kuu” katika maisha yangu.
-
Wakati Bwana alipoigawa Bahari ya Shamu, Musa na Waisraeli waliona jinsi Yeye alivyo na nguvu. Acha watoto wako wakusaidie kufikiria njia ya burudani ya kufanya igizo la hadithi hii katika Kutoka 14:5–22 (ona pia “Pasaka” katika Hadithi za Agano la Kale, 70–74). Pengine ungeweza kupanga viti au blanketi na “gawanya” kama Bahari ya Shamu. Kisha mngeweza kushiriki na kila mmoja jinsi mlivyoona nguvu za Mungu katika maisha yenu.
2:54The Passover
-
Ni kipi Mafundisho na Maagano 8:2–3 inaongeza kwenye uelewa wetu wa hadithi katika Kutoka 14? Fikiria kuwasimulia watoto wako kuhusu uzoefu wakati Roho Mtakatifu alipokuambia kitu fulani katika akili yako au moyo wako na waalike kuzungumza kuhusu uzoefu wao. Mngeweza pia kuimba wimbo kuhusu Roho Mtakatifu, kama vile “Let the Holy Spirit Guide” (Nyimbo za Dini, na. 143).
Kutoka 3:22–25
Bwana anaweza kufanya vitu vichachu kuwa vitamu.
-
Pengine wewe na watoto wako mngeweza kunywa kitu kitamu na kitu kichungu wakati mkijifunza Kutoka 15:22–25 pamoja. Ni kwa jinsi gani Mwokozi amefanya matukio “machungu” katika maisha yetu “matamu”?
Kutoka 15:23–25; 16:14–15; 17:1–6
Yesu ni Maji yangu ya Uzima, Mkate wangu wa Uzima, na Mwamba wangu.
-
Wakati wewe na watoto wako mkisoma Kutoka 15:23–25; 16:14–15; 17:1–6, acha wakusaidie kupata vitu vya kusaidia kusimulia kila hadithi—kama tawi (kuponya maji huko Mara), chupa au chungu (kujaza mana), na jiwe (kwa ajili ya maji huko Horebu). Je, hadithi hizi zinatukumbusha nini sisi kuhusu kile Yesu Kristo anafanya kwa ajili yetu? Kama sehemu ya majadiliano yenu, mngeweza kusoma Mathayo7:24–27; Yohana 4:10–14; 6:29–35, 48–51; Helamani 5:12; Mafundisho na Maagano 20:77, 79.
Mmoja Mbele ya Mungu, na Joseph Brickey (maelezo ya kina)
Kutoka 17:8–16; 18:13–26
Ninaweza kusaidia “kubeba mzigo” wa kufanya kazi ya Bwana.
-
Unaposoma Kutoka 17:8–16, ungeweza kumwalika mtoto kunyanyua mikono yake angani. Wakati mtoto anapochoka, watoto wengine wangeweza kusaidia, jinsi Haruni na Huri walivyomsaidia Musa. Hadithi hii inafundisha nini kuhusu jinsi tunavyoweza kusaidia ufalme wa Mungu kufanikiwa? Ungeweza pia kusoma Kutoka 18:13–26 na kuzungumza kuhusu majukumu mazito ya watu wanaohudumu katika kata yako. Je, tunaweza kufanya nini leo kuwasaidia viongozi wetu wa Kanisa, kama vile Haruni na Huri walivyomsaidia nabii Musa?
Kwa ajili ya zaidi, ona toleo la mwezi huu la jarida la Rafiki .