2025
Kile Ambacho Siyo Mungu
Agosti 2025


Ujumbe wa kila Mwezi Kwa Ajili ya Nguvu kwa Vijana, Agosti 2025

Kile Ambacho Siyo Mungu

Kweli 5 kuhusu Baba Yetu wa Mbinguni

Tunaweza kujifunza mengi kuhusu Mungu ni nani wakati tunapoelewa kile ambacho Yeye siyo.

rangi na brashi ya kupakia rangi

Kielelezo na Camila Gray

Mojawapo ya baraka kubwa za Urejesho ni kwamba Mungu amejifunua tena Yeye Mwenyewe na tabia Yake kama Baba wa Mbinguni mwenye upendo. Lakini wakati mwingine tuna fikra au mawazo kuhusu Mungu ambayo siyo ya kweli. Wakati hili linapotokea, tunaweza kujifunza mengi kuhusu Mungu ni nani kwa kuelewa kile ambacho Yeye siyo.

Mungu siyo mtu asiyejulikana kwenye kiti cha enzi mbali, mbali sana.

Yeye ni Baba yetu, wa kupendeza zaidi kuliko hata baba bora wa kidunia unayeweza kufikiria. Ingawa hatuwezi kukumbuka maisha yetu kabla ya kuja duniani pamoja Naye, Yeye anatujua kibinafsi na kikamilifu. Yeye ana mwili mkamilifu wa nyama na mifupa, na sisi tu katika mfano Wake.

Kama unahangaika kuvuta taswira ya jinsi Mungu alivyo, kuna mfano kamili: Mwanawe, Yesu Kristo. Kristo alisema, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi. Kama mngalinijua mimi, mngalimjua na Baba; tangu sasa mnamjua, tena mmemwona” (Yohana 14:6–7). Kwa maneno mengine, kama tunataka kujua Baba wa Mbinguni alivyo, tunaweza kujifunza kuhusu vile Yesu Kristo alivyo! Wameungana kikamilifu katika madhumuni.

Mungu siyo mtu mwenye shughuli nyingi za kushindwa kukushughulikia wewe.

Kwa kweli, kukusaidia kupata uzima wa milele ndiyo kazi Yake na utukufu Wake. Wewe ndiwe fokasi Yake Namba1! Yeye hafungwi na muda kama sisi tulivyo. Mfikie Yeye katika sala wakati wo wote. Kisha sikiliza njia nyingi Yeye anavyojibu.

Mungu siyo mtu anayekulazimisha kumfuata Yeye.

Mzee Dale G. Renlund wa Akidi ya Mitume Kumi na Wawili wakati mmoja alifundisha, “Lengo la Baba yetu wa Mbinguni katika malezi si kuwafanya watoto Wake wafanye yaliyo sahihi; bali kuwafanya watoto Wake wachague kufanya yaliyo sahihi na hatimaye kuwa kama Yeye.” Yeye atakualika, atashauriana nawe, na kukufundisha ukweli, lakini Yeye hataondoa haki yako ya kujiamulia kwa kukulazimisha kumfuata Yeye.

Mungu siyo mtu anayejaribu kukukamata ukifanya kitu kibaya ili Yeye aweze kukuadhibu.

Badala yake, kama Mzee Patrick Kearon wa Akidi ya Mitume Kumi na Wawili alivyosema, “Mungu yuko katika kuwatafuta ninyi bila kukoma,” ikimaanisha Yeye kamwe hatakata tamaa kujaribu kukusaidia wewe kurudi Kwake. Yeye anajua sisi sote kiuhalisia tutakumbana na mambo magumu wakati tunapofanya makosa. Hivyo Yeye hutoa njia kwa ajili yetu ya kufanywa kuwa safi kutokana na dhambi na kupata nguvu kupitia Upatanisho wa Mwanawe.

Mungu siyo mtu anayekusubiri uwe “wa kutosha” au “mkamilifu” kabla Yeye hakupende.

Upendo Wake kwa ajili yako hauna kikomo. Yeye anakupenda hivi sasa, vivyo hivyo ulivyo na mapungufu! Rais Jeffrey R. Holland, Kaimu Rais wa Akidi ya Mitume Kumi na Wawili, anatoa ufafanuzi wenye nguvu kuhusu ukweli huu: “‘Njoo kama ulivyo,’ Baba mwenye upendo husema kwa kila mmoja wetu, lakini Yeye anaongeza, ‘Usipange kukaa kama ulivyo.’ Tunatabasamu na kukumbuka kwamba Mungu amedhamiria kutufanya sisi zaidi ya tulivyodhani tungeweza kuwa.” Kwa upendo mkamilifu na kutia moyo, Baba wa Mbinguni anajaribu kukusaidia kuwa kama Yeye na kupokea vyote Yeye alivyonavyo, hatua moja kwa wakati mmoja.

Mungu NI Nani

Njia bora ya kumjua Baba yako wa Mbinguni ni kuendelea kuwa na uzoefu naye. Kwa jinsi gani? Jifunze kumhusu Yeye na Mwanawe kutoka kwenye maandiko na maneno ya manabii walio hai. Sali Kwake. Zitii Amri Zake Kaa kimya, wakati binafsi wa kumwabudu Yeye kanisani, hekaluni, na katika sehemu zingine takatifu. Fanya na shika maagano na Mungu. Yeye atakusaidia kumjua Yeye ni nani na jinsi Yeye anavyojisikia kukuhusu wewe.