2025
Ukweli juu ya Maisha Yetu
Agosti 2025


“Ukweli juu ya Maisha Yetu,” Liahona, Agosti. 2025.

Ujumbe wa Kila Mwezi wa Liahona, Agosti 2025

Ukweli juu ya Maisha Yetu

Baba yetu wa Mbinguni mwenye upendo amefunua kweli juu ya maisha yetu ya zamani, ya sasa, na ya baadaye, ikijumuisha jinsi ya kupokea zawadi kuu zaidi ya zote.

Duka la N.K. Whitney & Co.

Juu ya ngazi katika chumba kidogo, kilichosongamana watu juu ya duka la Newel K. Whitney huko Kirtland, Ohio, Januari 22, 1833, wazee wa Kanisa walikusanyika pamoja na Nabii Joseph Smith. Mnamo Desemba mwaka uliokuwa umepita, Joseph alikuwa amepokea ufunuo ukimwelekeza kuanzisha shule kimsingi ili kuwaandaa viongozi wa ukuhani kwa ajili ya misheni.

“Na ninatoa kwenu amri” Bwana alitamka, “ya kuwa mfundishane mafundisho ya ufalme.

“Fundishaneni kwa bidii na neema yangu itakuwa pamoja nanyi, ili mpate kuelekezwa kiukamilifu zaidi katika nadharia, katika kanuni, katika mafundisho, katika sheria za injili, katika mambo yale yote yahusuyo ufalme wa Mungu, yale yaliyo muhimu kwenu kuyafahamu; …

“Ili mpate kuandaliwa katika mambo yote wakati nitakapowatuma tena kutukuza wito ambao nimewaitia, na huduma ambayo kwayo nimewapa mamlaka” (Mafundisho na Maagano 88:77–78, 80).

Hii “Shule ya Manabii,” kama ilivyoitwa, ilitoa mmiminiko wa ajabu wa kiroho. Viongozi wengi wa mwanzo wa Kanisa walifundishwa huko. Leo ulimwengu ni sehemu tofauti kabisa, lakini mwongozo ambao Bwana aliutoa wakati huo basi bado unatumika sana. Sisi, pia, lazima tutafute maarifa na ukweli “wa mambo kama yalivyo, na kama yalivyokuwa, na kama yatakavyokuwa” (Mafundisho na Maagano 93:24).

mwanamke akitafakari kitabu anachosoma

Utafutaji Wetu wa Ukweli

Katika kipindi hiki tunachoishi, maarifa zaidi yanapatikana kwetu kuliko hapo awali. Hapo awali, kama ulitaka kujua kitu fulani, ilibidi uende kwenye maktaba na ukitafute. Leo intaneti na vifaa vya mkononi vinatoa ufikiaji wa taarifa zisizo na mwisho tunazoweza kupata mara moja tu.

Bwana anafurahia tunapofanya matumizi ya busara ya nyenzo zinazopatikana kwetu, lakini Yeye ametoa ushauri huu usiopitwa na wakati: “Tafuteni kwa bidii na kufundishana maneno ya hekima; ndiyo, tafuteni kutoka kwenye vitabu vizuri maneno ya hekima; tafuteni maarifa, hata kwa kujifunza na pia kwa imani” (Mafundisho na Maagano 88:118). Yeye anatuhimiza tujifunze kuhusu ulimwengu unaotuzunguka (ona Mafundisho na Maagano 88:79; 93:53), lakini katika utafutaji wetu wa ukweli, ni lazima tumtegemee Mungu, “ajuaye vitu vyote, na vitu vyote viko mbele yake, … na yeye yu juu ya vitu vyote, na ndani ya vitu vyote, … na vitu vyote viko kwake, na ni vyake yeye” (Mafundisho na Maagano 88:41).

Miongoni mwa kweli ambazo Mungu ametupatia, mojawapo ya msingi kwa ajili ya maisha yetu hapa duniani ni kwamba Yeye ni Baba yetu wa Mbinguni. Sisi ni wana na mabinti Zake wa kiroho. Yeye anatujua na anatupenda kikamilifu. Na kama watoto Wake wa kiroho, tuna asili na hatima ya kiungu. Kuelewa na kukumbatia kweli hizi za milele hutupatia utambulisho, thamani, na kusudi ambalo lilitubariki na kutuelekeza katika maisha yetu kabla ya duniani na tutaendelea kufanya hivyo sasa na milele.

watu wakipita kwenye pazia

Tulikuwa pamoja na Baba hapo Mwanzoni

Tunapotafuta ukweli wa mambo “kama yalivyokuwa,” tunagundua maneno haya kutoka kwa Mwokozi wetu, Yesu Kristo: “Na sasa, amini ninawaambia, hapo mwanzo nilikuwepo kwa Baba, na Mimi ndiye Mzaliwa wa Kwanza;” na “ninyi pia mlikuwepo mwanzoni pamoja na Baba” (Mafundisho na Maagano 93:21, 23).

Kabla ya maisha yetu duniani, tulihudhuria baraza mbinguni ambapo Baba yetu wa Mbinguni aliwasilisha mpango Wake mkuu wa furaha. Nabii Joseph Smith alifundisha kwamba motisha ya Mungu kwa mpango Wake ni kutupatia “fursa ya kuendelea kama yeye mwenyewe [na] … kuinuliwa pamoja na yeye.” Kazi Yake na utukufu Wake ni “kuleta kutokufa na uzima wa milele wa mwanadamu” (Musa 1:39).

Tulitumia haki yetu ya kujiamulia na kuchagua kufuata mpango wa Baba Yetu wa Mbinguni. Tumebarikiwa kuzaliwa katika maisha haya, ambapo tunaendelea kuwa na haki ya kujiamulia na tunaweza kupata uzoefu wa maisha ya duniani, kujifunza, na kuendelea kuelekea uzima wa milele.

Wakati wa safari yetu duniani, tutapitia changamoto na vikwazo. Lakini hatuhitaji kukabiliana na dhiki ya maisha pekee yetu. Joseph Smith alifundisha kwamba Baba wa Mbinguni, “Mzazi Mkuu wa ulimwengu[,] anaangalia familia yote ya binadamu kwa utunzaji wa kibaba na kujali kwa mzazi.”

Baba yetu wa Mbinguni, “Baba wa rehema, na Mungu wa faraja yote,” atatubariki, atatuinua, na kutufariji “katika dhiki zetu zote ili nasi tupate kuwafariji wale walio katika dhiki za namna zote, kwa faraja hizo, tunazofarijiwa na Mungu” (2 Wakorintho 1:3–4). Kama sehemu muhimu ya mpango Wake, Baba wa Mbinguni ametupa njia ya sisi kurudi Kwake.

Bustani ya Gethsemane. Israeli

Njia ya kwenda kwa BabaYetu

Ukweli “wa mambo kama yalivyo” (Yakobo 4:13) ni wazi: hatuwezi kufikia uwezekano wetu kamili kama watoto wa Baba yetu wa Mbinguni pekee yetu. Yesu Kristo, Mwana Mzaliwa wa Kwanza wa Baba katika roho, alikubali kuwa Mwokozi na Mkombozi wetu.

Yesu Kristo, “Mwana wa Pekee wa Baba, aliyejaa neema na ukweli, hata Roho wa kweli, … alikuja na akakaa katika mwili, na akakaa miongoni mwetu” (Mafundisho na Maagano 93:11). Yeye alikuja kutuonyesha njia ya kupata furaha, maana, na shangwe katika maisha haya na katika umilele.

“Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe wa pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.

“Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye” (Yohana 3:16–17).

Uzoefu wa Mwokozi duniani ni muhimu. Yeye “hakupokea utimilifu mwanzoni, bali alipokea neema juu ya neema” (Mafundisho na Maagano 93:12). Yeye alikua hadi “akapokea utimilifu wa utukufu wa Baba” na “uwezo wote, mbinguni na duniani, na utukufu wa Baba ulikuwa pamoja naye, kwa maana alikaa ndani yake” (Mafundisho na Maagano 93:16–17). Mwokozi alifundisha:

“Ninayatoa kwenu ninyi maneno haya ili muweze kufahamu na kujua namna ya kuabudu, na kujua nini mnachokiabudu, ili muweze kuja kwa Baba katika jina langu, na kwa wakati wake mpokee utimilifu wake.

“Kwani ikiwa mnazishika amri zangu mtaupokea utimilifu wake, na kutukuzwa ndani yangu, kama Mimi ndani ya Baba; kwa hiyo, ninawaambia, mtapokea neema juu ya neema” (Mafundisho na Maagano 93:19–20).

Katika Bustani ya Gethsemane na msalabani, Yesu Kristo alijichukulia juu Yake dhambi za ulimwengu na kuteseka huzuni yote na “maumivu na mateso na majaribu ya kila aina” (Alma 7:11). Hii “ilisababisha [Yeye], … mkuu wa vyote, kutetemeka kwa sababu ya maumivu, na kutoka damu kwenye kila kinyweleo” (Mafundisho na Maagano 19:18). Ni kupitia kwa Yesu Kristo pekee na Upatanisho Wake na Ufufuko ndiyo wokovu na kuinuliwa kunawezekana.

Kupitia neema ya Mwokozi na dhabihu ya kulipia dhambi, tunaweza kukua mpaka tupokee utimilifu na siku moja tunaweza kuletwa kwenye ukamilifu. Kama tutafuata mfano wa Mwokozi na kutii amri Zake, Yeye atatuongoza na kutuelekeza kwenye njia yetu ya kurudi kwenye uwepo mtukufu wa Baba yetu wa Mbinguni.

picha ya kuchora ya Kristo akitembea njiani kuelekea Yerusalemu

Kristo akiwa Njiani kwenda Yerusalemu, na Michael Coleman, isinakiliwe

Je, Utapokea Zawadi Yake?

Miongoni mwa kweli “za kama mambo yatakavyokuwa” (Yakobo 4:13), tunajifunza kwamba uzoefu wetu katika umilele utaamuliwa na uchaguzi wetu wa kumfuata Yesu Kristo na kupokea zawadi anazotoa. Maandiko yanafundisha kwamba “tutafurahia kile ambacho [sisi] tuko radhi kukipokea.” Cha kusikitisha, baadhi “hawatakuwa tayari kufurahia kile ambacho wangelikipokea” (Mafundisho na Maagano 88:32).

Rais wangu wa misheni, Mzee Marion D. Hanks (1921–2011), ambaye alihudumu kama Sabini Kiongozi Mkuu Mwenye Mamlaka, aliwafundisha wamisionari wake kwamba kuuliza kile ambacho tuko radhi kupokea na kufurahia ni njia tunayoweza kujua pale tulipo katika safari yetu ya kiroho. “Kwani itamfaidia mtu nini kama zawadi imewekwa juu yake, na hapati zawadi hiyo?” Tunapopokea zawadi za Mwokozi kwa kumtafuta na kumfuata Yeye kwa bidii, tutafurahia katika tumaini la uzima wa milele na “katika yeye aliye mtoaji wa zawadi [ile]” (Mafundisho na Maagano 88:33). Kipawa hiki kilichotolewa kwa upendo “ni kipawa kikuu kati ya vipawa vyote vya Mungu” (Mafundisho na Maagano 14:7).

Mungu ni Baba yetu wa Mbinguni. Yeye anatujua na anatupenda. Tunapomgeukia Yeye katika utafutaji wetu wa ukweli, tunaweza kuambatana na akili, kupokea hekima, kukumbatia ukweli, kupenda wema, na kuambatana na nuru ambayo huja kutoka Kwake (ona Mafundisho na Maagano 88:40). Kisha tunaendelea katika maisha yetu yote hadi “siku itakuja [sisi] tutakayomjua Mungu, tukiwa tumehuishwa ndani yake na yeye mwenyewe” (Mafundisho na Maagano 88:49).

Hiyo itakuwa siku tukufu na ya furaha.

Muhtasari

  1. Teachings of Presidents of the Church: Joseph Smith (2011), 210, Maktaba ya Injili.

  2. Teachings: Joseph Smith, 39.